Jumatatu, 8 Juni 2026

MAHAKAMA KUU MBEYA YAZINDUA MPANGO WA MALEZI YA KITAALUMA KWA MAHAKIMU

Na. MUKSINI NAKUVAMBA- Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles Tiganga, amezindua rasmi Mpango wa Malezi ya Kitaaluma kwa Mahakimu (Mentorship Program) hivi karibuni. Mpango huo unalenga kuimarisha utendaji kazi wa Mahakimu na kuongeza imani ya wananchi kwa Mahakama pamoja na huduma zinazotolewa mahakamani.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Tiganga alisema kuwa, mpango huo umeanzishwa kwa lengo la kuwajengea Mahakimu uwezo zaidi wa kiutendaji kupitia ushauri, mwongozo na malezi kutoka kwa viongozi na watendaji wenye uzoefu mkubwa katika tasnia ya sheria na utoaji wa haki.

“Ukimpata mtu wa kukwambia madhaifu yako, huyo anakujenga. Utafakari ushauri huo na kuufanyia kazi akisisitiza umuhimu wa kupokea ushauri kwa lengo la kujiboresha kitaaluma na kiutendaji,” alisema Mhe. Tiganga.

Aidha, Mhe. Tiganga aliongeza kuwa Mahakama inatarajia mpango huo kuzalisha viongozi bora wenye uwezo wa kuongoza, kukua binafsi na kuwainua wengine katika taaluma yao.

“Tunatarajia kuwa, baada ya kumalizika kwa programu hii, tutakuwa na viongozi wazuri wanaotambua vyema dhana ya uongozi, kukua na kukuza wengine kitaaluma na kiutendaji,” alisisitiza Mhe. Tiganga.

Kwa upande wao, baadhi ya Mahakimu walioshiriki katika uzinduzi wa Mpango huo wamepongeza hatua hiyo, wakieleza kuwa mpango huo utakuwa chachu ya kuboresha utendaji kazi wao na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za kimahakama.

“Tumelipokea jambo hili kwa mikono miwili na tunaamini kuwa litatunufaisha sana sisi Mahakimu na kuboresha utendaji kazi wetu. Tunatarajia kujifunza zaidi na kufikia viwango vya juu zaidi vya utendaji kazi katika vituo vyetu vya kazi,” alisema Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Paul Ntumo.

Uzinduzi huo, ulihusisha Mahakimu kutoka maeneo mbalimbali, ambapo sehemu yao walishiriki kupitia mfumo wa mkutano mtandao (video conference), jambo lililowezesha ushiriki mpana wa watumishi wa Mahakama ndani ya Masjala Ndogo ya Mbeya.

Mpango wa Malezi ya Kitaaluma kwa Mahakimu unatarajiwa kuwa nyenzo muhimu katika kuimarisha uwezo wa watumishi wa Mahakama, kuongeza ubora wa utoaji wa haki na kuendeleza dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya kutoa huduma bora kwa wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (Katikati) akiongoza uzinduzi huo, kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo, na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (kulia).

Sehemu ya Mahakimu walioshiriki katika kikao cha uzinduzi huo.

Sehemu ya Mahakimu walioshiriki katika uzinduzi huo kwa njia ya Mtandao (Video conference).


Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo (wa kwanza kushoto), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi Laizer (katikati), Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba (kulia) wakifuatilia kwa karibu kikao cha uzinduzi wa program ya Malezi kitaaluma.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni