· Rais Mhe. Dkt. Mwinyi aahidi ushirikiano
· Ampongeza Jaji Mkuu na kumtakia kila la kheri katika utekelezaji wa majukumu yake
· Apongeza pia maboresho ya
Mahakama ya Tanzania
·
Asema Mahkama ya Zanzibar ina mengi
ya kujifunza kutoka Mahakama ya Tanzania
Na
MARY GWERA, Mahakama-Zanzibar
Jaji
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ya leo tarehe 22
Juni, 2026 amemtembelea Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi na kufanya naye mazungumzo mafupi.
Mhe.
Masaju na ujumbe wake waliwasili Ikulu ya Zanzibar iliyopo Mnazi Mmoja majira
ya Saa 4 Asubuhi na kupokelewa na Maafisa wa Ikulu ambao walimuongoza Jaji Mkuu
kwenye ukumbi maalum ulioandaliwa kwa ajili ya mazungumzo kati ya Rais wa Zanzibar
na mgeni wake Jaji Mkuu wa Tanzania.
Katika
mazungumzo yao, Rais Mwinyi amempongeza Jaji Mkuu kwa kushika wadhifa huo na amemuhakikishia
ushirikiano sambamba na kupongeza ushirikiano uliopo baina ya Mahkama ya
Zanzibar na Mahakama ya Tanzania na kusisitiza umuhimu wa kuuendeleza ili
kuimarisha utekelezaji wa majukumu ya pamoja kwa manufaa ya wananchi.
“Nami
nichukue kwanza fursa hii kukupa pongezi ya kuwa Jaji Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, hongera sana na tunataka kukuhakikishia ushirikiano wetu,
bahati nzuri tayari tuna ushirikiano mzuri sana kati ya Majaji Wakuu wa pande
mbili na Watendaji wa Mahakama vilevile wana ushirikiano mzuri tu, na mimi
nimepata fursa mara kadhaa kukutana nao na nashukuru na ninafurahi kusema
kwamba kuna mambo mengi ambayo tunapata msaada kutoka Mahakama ya Jamhuri,”
amesema Mhe. Dkt. Mwinyi.
Rais
Mwinyi amesema, Mahkama ya Zanzibar imekuwa ikipata msaada kutoka Mahakama ya
Tanzania katika maeneo mengi ikiwemo matumizi ya Teknolojia ya Habari na
Mawasiliano (TEHAMA) katika utendaji wa Mahakama na kwamba ni eneo muhimu
linalopaswa kupewa kipaumbele ili kuharakisha upatikanaji haki na kuongeza
ufanisi.
“Eneo
la TEHAMA ni eneo ambalo watu wetu huku wamekuwa wakijifunza sana upande wa
pili na hatua mliyopiga wanataka na wenyewe waweze kufikia na wanapata
ushirikiano wa kutosha,” amesema Mhe. Dkt. Mwinyi.
Amesema
Mahkama ya Zanzibar ina fursa ya kujifunza kutokana na mafanikio yaliyofikiwa
na Mahakama ya Tanzania katika matumizi ya TEHAMA, kwa lengo la kuhakikisha
wananchi wanapata haki kwa wakati na kupunguza gharama za kiutendaji.
Aidha,
amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeweka mkazo katika matumizi ya TEHAMA
na uimarishaji wa miundombinu ya Mahakama katika ngazi zote, ili wananchi
wapate huduma za haki kwa wakati, katika mazingira bora na karibu na maeneo
wanayoishi.
Akizungumzia
ujenzi wa miundombinu ya Mahakama, Rais Dkt. Mwinyi amesema ujenzi wa jengo la
Mahakama ya Rufani Pemba ni hatua muhimu itakayowezesha Majaji kutekeleza
majukumu yao katika mazingira bora na kuimarisha huduma za kimahakama kisiwani
humo.
“Lakini
vilevile, kuna eneo la Ujenzi wa Miundombinu ya Mahakama, ukiacha ile ngazi ya
Rufani tayari tuna Mradi mkubwa kule Pemba, umefikia hatua nzuri na matarajio yetu
muda si mrefu tuukamilishe ili tuweze kutoa nafasi nzuri ya Majaji wa Rufani wanapokuja
upande wa pili basi wawe na mazingira ya kufanyia kazi yanayoendana na kazi
wanazozifanya, kwahiyo nashukuru kwamba ushirikiano ni mzuri, mahusiano ni mazuri,
kinachotakiwa ni kuyaendeleza,” amesisitiza. Rais Dkt. Mwinyi.
Ameongeza
kwa kuishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kutambua kazi nzuri zinazofanywa na
Serikali ya Zanzibar ambapo amesema, “Nashukuru kwamba angalau kuna jambo
ambalo na sisi mmeona mjifunze kutoka kwetu, hii ni hatua kubwa kwetu kwa
sababu sisi tumeshaweka hiyo ngazi ya rufaa ambayo ni fanisi zaidi kuliko
ilivyokuwa awali.”
Kadhalika,
Mhe. Dkt. Mwinyi amemshukuru Jaji Mkuu kwa kufika kujitambulisha kwake rasmi na
amempongeza na kumtakia kila la kheri Jaji Mkuu wa Tanzania katika utekelezaji
wa majukumu yake.
Kwa
upande wake, Jaji Mkuu amepongeza ushirikiano unaotolewa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Mahakama ya Zanzibar.
“Mhe.
Rais nashukuru kwa fursa hii ya kukuona, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa
kukuwezesha kuwa, Rais wetu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi, yanayofanyika huku tunayaona, mwenye macho haambiwi
tazama, hongera sana,” amesema Mhe. Masaju.
Aidha,
amesema uamuzi wa kujenga Mahakama ya Rufani Pemba ni wa busara na kuahidi
kusimamia ujenzi huo ili ukamilike kwa wakati, kwa lengo la kuwapatia wananchi
huduma bora za haki na kuwapunguzia gharama za kufuatilia mashauri yao.
Aidha,
Jaji Mkuu amemueleza Rais Mwinyi kuwa, amefika kumuona kwa kuwa tangu ateuliwe
kuwa Jaji Mkuu alikuwa hajafika kumuona ili amfahamu na endapo ana ushauri
wowote amshirikishe ili ayazingatie anapokuwa anatekeleza majukumu yake ya Jaji
Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Nafahamu
kwamba kama Jaji Mkuu pia ndio Mkuu wa Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania ambayo ni Mahakama ya Muungano, yanaweza kuwepo mambo mengine
ambayo ungependa kunishirikisha ili ninapotekeleza majukumu yangu nitekeleze
kwa namna ambayo ni ya ufanisi sana kuimarisha muungano wetu lakini zaidi pia
kuharakisha maendeleo ya Zanzibar kupitia maamuzi ya Mahakama, yaani katika
kutekeleza majukumu yetu tutekeleze kwa namna ambayo hasa kwa mashauri ya Zanzibar
pia yanachelewa kupata uamuzi, yapate uamuzi mapema na haki ipatikane mapema
ipasavyo,” amesema Mhe. Masaju.
Jaji
Mkuu amemueleza Rais Mwinyi kuwa, kwa sasa kuna vikao vya Mahakama ya Rufani
vinaendelea Nchi nzima ikiwemo Zanzibar, na kwamba Mahakama ya Tanzania
inashukuru kwa kupata ushirikiano mzuri kutoka kwa Jaji Mkuu wa Zanzibar na
kumekuwa na mahusiano ya karibu.
“Tunajifunza
mengi kutoka Zanzibar, wenzetu kuna maeneo mengine wamepiga hatua zaidi kuliko
ilivyo kwa Bara na kwa mfano huku Zanzibar pia kuna Mahakama ya Mkoa, kule hakuna
Mahakama ya Mkoa kuna Mahakama inaitwa Mahakama ya Hakimu Mkazi ina mamlaka sawa
na Mahakama ya Wilaya, tunaona kwamba hiyo sio sawa, haiwezekani kwa mfano Mkuu
wa Wilaya akawa na mamlaka sawa na Mkuu wa Mkoa na unakuta hawana kazi pale
wanapangiwa kazi na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Wilaya, kwahiyo tunataka
kurekebisha sheria,” amesema Mhe. Masaju.
Aidha,
Jaji Mkuu amebainisha kwamba, Muswada umeshaandaliwa baada ya kuwa wamejifunza kutoka
Zanzibar ambapo Mahakama hiyo haitaitwa tena Mahakama ya Hakimu Mkazi bali itaitwa
Mahakama ya Mkoa ili pamoja na kuwa na majukumu yake ya msingi iweze pia kusikiliza
rufaa zinazotoka Mahakama ya Wilaya.
Mhe.
Masaju amemshukuru Rais Mhe. Dkt. Mwinyi na kusema kuwa, uamuzi wa Serikali ya
Mapinduzi Zanzibar kuwa na Mahkama Kuu Pemba ni uamuzi wa Hekima na mzuri kwa
sababu inawapunguzia watu umbali wa kuja kupata haki, inawapunguzia gharama,
wanapata huduma katika eneo ambalo wamelizoea.
“Mhe.
Rais nikuhakikishie kwamba tuko makini kuhakikisha kwamba ule Mradi unakamilika
mapema ipasavyo ili Mahakama ile ianze kufanya kazi vizuri ikitumia sasa lile
jengo la kisasa ambalo unaweza kuweka hata miundombinu mingine ikiwemo miundombinu
ya TEHAMA. Mhe. Rais anakusudia alizindue hili jengo kwa pamoja atakapokuwa
anazindua hili jengo atakuwa anatumia hiyo fursa kuzindua majengo mengine nane
ambayo yamejengwa nchi nzima, kwahiyo ni Mradi mkubwa sana na hatua kubwa sana
katika ushirikiano wa hizi Serikali mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,” ameeleza Jaji Mkuu.
Katika
hatua nyingine, Mhe. Masaju amesema matumizi ya TEHAMA ni muhimu sana kwa kuwa tuko
katika Uchumi wa Kidijitali (
Digital Economy).
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi akisisitiza jambo alipokuwa akizungumza na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 22 Juni, 2026 alipomtembelea Rais Mhe. Dkt. Mwinyi Ikulu ya Zanzibar.







Hakuna maoni:
Chapisha Maoni