Na MARY GWERA & HALIMA MNETE, Mahakama-Dodoma
·
Jaji Mruma ampa Wasia Hakimu huyo kutoa maamuzi
yanayozingatia Mila na Desturi za Jamii husika
·
Naye Jaji Tiganga amtaka kutoa haki kwa kuzingatia misingi
ya Katiba, Sheria za Nchi
Katika jitihada za kuendelea kuimarisha utoaji haki nchini
kupitia kuongezwa kwa watumishi wenye weledi na uadilifu, Jaji Mkuu wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju leo tarehe 24 Juni, 2026
amemuapisha Mhe. Rose Baltazar Ngero kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo.
Uapisho huo umefanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jaji
Mkuu, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, katika hafla iliyobeba
uzito wa kiutumishi na kisheria, ikionesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania ya
kuendelea kuimarisha Mhimili wa utoaji haki kuanzia ngazi za chini kabisa
zinazogusa wananchi moja kwa moja.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Viongozi mbalimbali Waandamizi wa
Mahakama akiwemo Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir
Mruma, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe.
Joachim Tiganga, baadhi ya Naibu Wasajili, watendaji pamoja na watumishi
wengine wa Mahakama.
Akitoa wasia kwa Hakimu huyo mpya mara baada ya uapisho,
Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma amemsisitiza
juu ya umuhimu wa kuzingatia sheria sambamba na mila na desturi za jamii husika
katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama.
“Katika kiapo chako umeahidi kusimamia sheria, mila na
desturi. Ni muhimu kuelewa kwamba mashauri mengi katika Mahakama ya Mwanzo
yanahusu maisha halisi ya jamii, hivyo uelewe mazingira na desturi za watu
unaowaamria,” amesema Mhe. Mruma.
Jaji Mruma amesema mashauri mengi yanayofikishwa katika
Mahakama za Mwanzo huhusisha masuala ya kijamii kama mirathi, talaka na
migogoro ya kifamilia ambayo mara nyingi huongozwa na mila na desturi za jamii
husika, hivyo ni muhimu kwa Hakimu kuwa na uelewa mpana wa mazingira
anayofanyia kazi ili kutoa uamuzi wenye haki na unaokubalika kijamii.
Mhe. Mruma amebainisha kuwa, uwezo wa Hakimu kuelewa na
kutafsiri Sheria za Kimila kwa usahihi unaweza kusaidia Mahakama kutoa maamuzi
yanayozingatia haki huku yakibaki karibu na uhalisia wa jamii, jambo
linaloongeza imani ya wananchi kwa mhimili wa Mahakama.
“Wakati mwingine suluhisho la mgogoro haliishii kwenye
vifungu vya sheria pekee, bali linahitaji pia uelewa wa historia, utamaduni na
namna jamii husika inavyoendesha maisha yake. Hapo ndipo busara ya hakimu
inapokuwa muhimu,” amesisitiza.
Aidha, Mhe. Mruma amemtaka Hakimu huyo kuzingatia maadili ya
kazi na kulinda heshima ya taaluma ya sheria.
“Jiepushe na mazingira au mienendo inayoweza kushusha hadhi
ya kazi yako. Uadilifu wako binafsi ndio msingi wa wananchi kuendelea kuiamini
Mahakama,” amesisitiza.
Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania
Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, amesema kazi ya utoaji haki ni
dhamana kubwa inayopaswa kutekelezwa kwa kuzingatia misingi ya Katiba, Sheria
za Nchi pamoja na maadili ya Viongozi wa Mahakama.
Amesema, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka
wazi mamlaka ya Mahakama kama Mhimili huru wenye jukumu la kutafsiri sheria na
kusimamia utoaji haki kwa usawa kwa wananchi wote.
“Kazi ya uamuzi si kazi ya kawaida; ni kazi inayogusa maisha
ya watu moja kwa moja. Katiba imeweka mamlaka huru ya Mahakama kutafsiri
sheria, hivyo kila uamuzi unaofanya unapaswa kuzingatia haki, sheria na maslahi
mapana ya taifa,” amesema Mhe. Tiganga.
Mhe. Tiganga ameongeza kuwa, pamoja na kuongozwa na sheria,
mtumishi wa Mahakama anapaswa kuwa na uadilifu, hofu ya Mungu na kujiepusha na
tamaa zinazoweza kuathiri utoaji haki.
“Hii ni kazi ya Kimungu. Fedha isikuharibu wala tamaa
isikupoteze, unapaswa kuwa na hofu ya Mungu kwa sababu wakati mwingine maamuzi
yako yanaweza kubadili maisha ya mtu milele,” amesema.
Sambamba na hilo, amesisitiza umuhimu wa ushirikiano,
nidhamu ya kiutumishi na kuheshimu mamlaka ndani ya Taasisi ya Mahakama, huku akibainisha
kuwa, hata wale walio na umri mdogo lakini wakabeba dhamana za kiuongozi
wanastahili kupewa heshima inayostahili.
“Mahakama inajengwa kwa ushirikiano. Waheshimu wenzako,
shirikiana nao na jifunze kila siku. Maarifa yapo mengi, hata kupitia Katiba,
miongozo na hotuba mbalimbali zinazopatikana katika tovuti za Mahakama,”
amesisitiza.
Uapisho wa Mhe. Rose Baltazar Ngero unaongeza nguvu katika
jitihada zinazoendelea za Mahakama ya Tanzania za kujenga mfumo wa utoaji haki
ulio karibu zaidi na wananchi, wenye ufanisi, unaozingatia maadili na
unaoendelea kujenga imani ya umma kwa mhimili wa Mahakama. Kupitia watumishi
wenye weledi, uadilifu na utayari wa kulitumikia taifa, Mahakama inaendelea
kutekeleza wajibu wake wa msingi wa kusimamia haki na kulinda utawala wa sheria
nchini.
Dhamira ya Mahakama ya Tanzania ni kuhakikisha wananchi
wanaendelea kupata huduma za kimahakama mapema ipasavyo, kwa weledi na kwa
kuzingatia misingi ya sheria, haki na usawa. Mahakama za Mwanzo zina nafasi
muhimu katika mfumo wa utoaji haki nchini kwa kuwa ndizo ngazi za mwanzo
zinazopokea na kusikiliza mashauri mengi yanayohusu maisha ya kila siku ya
wananchi, hususan migogoro ya kifamilia, ardhi, mirathi na masuala mengine ya
kijamii.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akimuapisha Mhe. Rose Baltazar Ngero kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mhe. Rose Baltazar Ngero akisaini hati ya kiapo mara baada ya kuapa kuwa Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mwanzo leo tarehe 24 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.














Hakuna maoni:
Chapisha Maoni