Na. Christopher Msagati – Mahakama, Manyara
Aliyekuwa
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara, Mhe. Ilvin
C. Mugeta amekabidhi ofisi kwa Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo
ya Manyara, Mhe. Dkt. Adam Mambi leo tarehe 24 Juni, 2026 ikiwa ni baada ya Mhe.
Mugeta kuhamishwa kuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora.
Mhe.
Dkt. Mambi ambaye kabla ya kuja Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara, alikuwa
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Tabora. Katika
hafla ya makabidhiano, Majaji hao walipata wasaa wa kuzungumza na watumishi
pamoja na wadau wa Mahakama, ambapo Mhe. Mugeta alitumia nafasi hiyo kuagana na
wanamanyara, huku Mhe. Dkt Mambi akitumia wasaa huo kujitambulisha na
kuwatambua watumishi wa Mahakama katika Masjala hiyo.
Akitoa
shukrani wakati wa kuagana na watumishi Mhe. Mugeta alisema kuwa, ushirikiano
alioupata toka Masjala Ndogo ya Manyara usiishie hapo mara baada ya kuondoka kwake
bali uendelee kwa Kiongozi huyo mpya na hata Viongozi wengine watakaoendelea
kuja kwenye Masjala hiyo.
“Leo
ni siku yangu ya pekee ambayo imechanganyikana na hisia za furaha pamoja na
huzuni, nalazimika kuagana na watumishi niliokuwa nao tangu mwaka 2025
nilipohamia Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara nikitokea Mahakama Kuu
Masjala Ndogo ya Arusha, watumishi hawa wamenipa heshima kubwa sana…
…Viongozi hawawezi kufanya kazi peke yao
isipokuwa kwa ushirikiano na umoja wetu. Mhe Jaji Mambi, ninakuachia watumishi
hodari ambao wana moyo wa kufanya kazi kwa bidii pasipo kushurutishwa au
kusimamiwa kwa nguvu,” alisema Mhe. Mugeta.
Naye,
Mhe. Dkt. Mambi alipokea kwa mikono miwili ukaribisho aliyoupata kwa watumishi
wa Masjala hiyo, huku akisisitiza kuwa ofisi yake ipo wazi kwa yeyote mwenye
mawazo ya kuboresha. Alisisitiza kuwa yeye ni mtu wa kazi na anavutiwa zaidi na
wachapa kazi.
“Nashukuru
kwa uongozi wa Mahakama kwa kuona kuwa mimi naweza kuendeleza kazi njema ambayo
ameifanya Mhe Jaji Mugeta katika Masjala hii ya Manyara, kasi ya utendaji kazi
iliyokuwepo naamini tutaiendeleza na kushirikiana vema ili tuweze kuwahudumia
wananchi kwa namna ambayo inastahili,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.
Katika hafla hiyo, watumishi wa Kada
mbalimbali waliweza kutoa maneno ya kumkaribisha na kumpokea Mhe. Dkt. Mambi
anayehamia Manyara na pia kumuaga Mhe. Mugeta.
Miongoni mwao alikuwa ni Msaidizi wa
Sheria wa Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Thobias Kavishe
John alisema kuwa, wataendelea kutoa ushirikiano kwa Mhe. Dkt. Mambi ili aweze
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa. Pia Mhe. John alimtakia majukumu
mema Mhe. Mugeta katika majukumu yake mapya anayokwenda kuyaanza katika Kituo
chake Kipya cha Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora.
Naye, Msaidizi wa Hesabu wa Mahakama ya
Wilaya ya Babati Bw. Sixbert Hongoli aliahidi kuendeleza ushirikiano kutoka kwa
watumishi wa Kada nyingine ambao wote kwa ujumla wao wameonesha nia na utayari
wa kuyapokea maelekezo toka kwa Kiongozi huyo mgeni aliyeripoti Mahakama Kuu
Masjala Ndogo ya Manyara.
Kwa
namna ya pekee wanamanyara watamkumbuka Mhe. Mugeta kwa kuwa ndiye Jaji
Mfawidhi wa pili tangu kuanzishwa kwa huduma za Mahakama Kuu katika Masjala
Ndogo ya Manyara mnamo Mwezi Novemba mwaka 2022.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Mahakama Kuu
Tabora Mhe. Ilvin Mugeta (kulia) na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Manyara Mhe Jaji Dkt. Adam Mambi wakiwa katika tukio la kupeana hati
ya makabidhiano ya Ofisi ya Ufawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
akitoa neno la shukrani kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara
kwa mapokezi waliyompatia mara baada ya kuwasili kituoni hapo.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya
Tabora Mhe. Ilvin Mugeta akitoa neno la shukrani kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Manyara kwa kumuuga vizuri.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya
Tabora Mhe. Ilvin Mugeta (kulia) na Jaji Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) wakionesha hati za makabidhiano kwa
watumishi waliofika kushuhudia tukio hilo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Bi. Nyanzobe Hemedi akimkabidhi Zawadi ya ua Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayehamia Masjala Ndogo ya Tabora, Mhe. Ilvin Mugeta ikiwa ni Ishara ya kumuaga kutoka kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.
Watumishi
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara wakiendelea na zoezi la kujitambulisha wakati wa zoezi la Makabidhiano ya Ofisi kati ya Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara anayeondoka Mhe. Ilvin Mugeta na Jaji
Mfawidhi mpya Mhe Dkt Adam Mambi.
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
akisaini vitabu vya wageni katika Ofisi yake mpya mara baada ya kuripoti
kituoni hapo.
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
akisalimiana na baadhi ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara
mara baada ya kuripoti kituoni hapo.
Jaji
Mfawidhi mpya wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
akipokea Zawadi ya ua ikiwa ni Ishara ya Ukaribisho kutoka kwa Watumishi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni