Jumatano, 24 Juni 2026

JAJI MTULYA ATETA NA WADAU WA MAHAKAMA MASJALA NDOGO YA MBEYA

 Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya amefanya mazungumza na wadau wa haki jinai na madai wa Masjala Ndogo ya Mbeya kwa lengo la kujitambulisha na kutambuana baina ya wadau hao kufuatia mabadiliko ya uongozi katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

Akizungumza katika kikao kilichofanyika jana tarehe 23 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Mtulya aliwaasa wadau kudumisha ushirikiano uliopo baina yao na Mahakama mbali na masuala ya kiofisi hata katika mambo mbalimbali ya kijamii ikiwemo michezo.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu alitumia nafasi hiyo kuwaaga wadau hao kufuatia uhamisho wake wa kwenda Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es salaam huku akiwashukuru wadau hao kwa kuwa kinara wa kuhakikisha kuwa mashauri yanayamalizika mahakamani mapema ipasavyo kupitia ushirikiano wao wa karibu na Mahakama.

Naye, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo alitoa pongezi zake kwa wadau hao kwa namna walivyokuwa na ushirikiano mzuri kwa Mahakama na kutumia nafasi hiyo pia kuwaaga kufuatia uhamisho wake wa kuhamia Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Morogoro.

Nao wadau wa Mahakama waliahidi kudumisha ushirikiano uliopo baina yao na kueleza matumaini yao juu ya usimamizi thabiti kutoka kwa viongozi wa Mahakama huku wakitoa shukrani zao kwa Waheshimiwa Naibu Wasajili kwa muda wote walioshirikiana kwa pamoja katika shughuli mbalimbali za kiofisi na kijamii hadi kufikia uhamisho wao kwenda kwenye vituo vyao vipya vya kazi.

Aidha Mhe. Mtulya alihitimisha kikao hicho kwa kuahidi kushughulikia changamoto zote zilizowasilishwa na kuahidi kuwa mlezi bora kwa kuwajenga na kuwaweka katika mstari mnyoofu ili kufanikisha malengo ya kutoa haki kwa wakati mapema ipasavyo ili kukidhi matamanio ya wananchi wanaowahudumia.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya (aliyesimama) akifafanua jambo wakati wa kikao chake na Wadau wa Mahakama wa haki jinai na madai, kikao kilichofanyika jana tarehe 23 Juni, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Kulia ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Lyimo.

Sehemu ya wadau  wa haki jinai na madai waliohudhuria wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali katika kikao hicho.

Sehemu ya wadau  wa haki jinai na madai waliohudhuria wakifuatilia kwa makini hoja mbalimbali katika kikao hicho.

Mmoja wa wadau akizungumza na kuchangia mada kuhusu eneo lake la kazi katika kikao hicho.


Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Aziza Temu  (aliyesimama) akitoa neno wakati wa majadiliano na wadau hao wa Mahakama Masjala Ndogo ya Mbeya.

Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni