Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masijala ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, jana
tarehe 25 Juni, 2026 amefanya kikao na Madalali na Wasambaza Nyaraka wa
Mahakama katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya, kwa
lengo la kukumbushana majukumu yao ya kila siku, kubaini changamoto
zinazowakabili na kujadili mapendekezo ya namna ya kuboresha utendaji kazi ili
kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi kwa wakati mapema ipasavyo.
Akizungumza
wakati wa kikao hicho, Mhe. Mtulya aliwataka Madalali kuendelea kudumisha
umoja, mshikamano na ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu yao huku
wakizingatia kikamilifu taratibu, sheria na kanuni zinazoongoza kazi zao.
Mhe.
Mtulya alisisitiza kuwa, utekelezaji wa majukumu kwa kuzingatia misingi ya
taaluma na maadili utasaidia kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma za
Mahakama.
Aidha,
Mhe. Mtulya alieleza kwamba, ni muhimu kwa kila mdau kutekeleza wajibu wake kwa
mujibu wa mipaka ya mamlaka aliyopewa, akibainisha kuwa Mawakili wanapaswa
kuheshimu majukumu ya Madalali na kuepuka kuingilia utekelezaji wa kazi
zinazowahusu Madalali na wasambaza nyaraka za Mahakama ili kuimarisha
uwajibikaji na ufanisi katika mfumo wa utoaji haki.
Kwa
upande wake, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith
Lyimo aliwashauri Madalali kufanya vikao vya ndani kwa lengo la kujadili
changamoto mbalimbali zinazowakabili katika utekelezaji wa majukumu yao na
kuziwasilisha rasmi katika Ofisi ya Naibu Msajili ili zipatiwe ufumbuzi kwa
wakati na kwa utaratibu unaostahili.
Nao, Madalali
na Wasambaza nyaraka za Mahakama, walieleza kuwa moja ya changamoto kubwa
wanazokutana nazo ni uelewa mdogo wa baadhi ya wananchi pamoja na viongozi wa
Serikali za Mitaa kuhusu nafasi, umuhimu na majukumu ya Madalali wa Mahakama. walisema
kuwa, hali hiyo wakati mwingine husababisha ugumu katika utekelezaji wa
majukumu yao na kuchelewesha baadhi ya hatua za utekelezaji wa amri za
Mahakama.
Akijibu
hoja hiyo, Mhe. Mtulya alisisitiza umuhimu wa kuwashirikisha wadau mbalimbali
katika vikao vijavyo, ikiwemo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ili
kusaidia kutoa elimu kwa viongozi wa Serikali za Mitaa, Halmashauri na Manispaa
kuhusu nafasi na umuhimu wa Madalali katika kusaidia Mahakama kutekeleza
majukumu yake ya utoaji haki kwa wananchi.
Kikao
hicho ni sehemu ya jitihada za Mahakama za kuendelea kuimarisha ushirikiano na
wadau wake muhimu, kuboresha mazingira ya utendaji kazi na kuongeza ufanisi
katika utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
Mhe, Fahamu Mtulya (kushoto) akiongoza kikao cha Madalali Mbeya, kulia ni Naibu
Msajili Mahakama kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo.
Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia
kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani)
Sehemu ya washiriki katika kikao hicho wakimfuatilia
kwa makini Mwenyekiti wa kikao hicho Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala
Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya Mhe. Fahamu Mtulya (hayupo pichani)
Mmoja wa Madalali wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala
Ndogo Mbeya akichangia jambo katika kikao hicho.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni