Na. MUKSINI NAKUVAMBA - Mahakama, Mbeya.
Watumishi
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliandaa hafla
maalumu ya kuwaaga viongozi wao waliowahi kufanya kazi nao kwa karibu,
wakielezea shukrani zao kwa mchango mkubwa walioutoa katika kuimarisha utendaji
kazi, ustawi wa watumishi na maendeleo ya Taasisi.
Hafla
hiyo iliyofanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
iliwakutanisha viongozi na watumishi mbalimbali katika mazingira yaliyojaa
hisia za furaha na huzuni kwa wakati mmoja.
Aidha, furaha
ilitokana na kuwatakia viongozi hao kila la heri na mafanikio katika majukumu
yao mapya, huku huzuni ikitokana na kuondoka kwa viongozi ambao walijijengea
heshima na upendo mkubwa miongoni mwa watumishi kutokana na uongozi wao wenye
busara, ushirikiano na kujali maslahi ya watumishi.
Viongozi
walioagwa ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe.
Aziza Emily Temu, Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Judith
Timoth Lyimo na Mtendaji wa Mahakama kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis
Fransis Miti, ambao kwa nyakati tofauti walipokea pongezi na maneno ya shukrani
kutoka kwa watumishi waliopata fursa ya kufanya kazi chini ya uongozi wao.
Kwa
upande wao, viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya pamoja na watumishi
waliopata nafasi ya kuzungumza walieleza kuwa viongozi hao wameacha alama kubwa
katika taasisi kutokana na uadilifu, uwajibikaji na moyo wa kujali watu
waliouonesha katika kipindi chote cha utumishi wao.
Miongoni
mwa shughuli zilizofanyika katika hafla hiyo ni utoaji wa maneno ya shukrani
kwa waagwa, utoaji wa zawadi maalum kama ishara ya kuthamini mchango wao,
kukata keki pamoja na kula chakula cha pamoja, matukio yaliyoongeza mshikamano
na kuacha kumbukumbu ya pekee kwa washiriki wote.
Hafla
hiyo ilihitimishwa kwa dua na salamu za heri, ambapo watumishi walisisitiza kuwa
milango ya Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya itaendelea kuwa wazi kwa viongozi
hao na kwamba mchango wao utaendelea kukumbukwa kwa muda mrefu kutokana na
athari chanya waliyoiacha katika taasisi na kwa watumishi kwa ujumla.
Waagwa wakiwa kwenye picha ya Pamoja katika hafla hiyo
kushoto ni Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe.
Aziza Temu, (katikati) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi.
Mavis Fransis Miti na kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo
Viongozi waagwa katika hafla hiyo wakikata keki kwa
Pamoja ikiwa ni Ishara ya upendo na mshikamano
Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa wamebeba zawadi zilizoandaliwa kwa ajili ya Viongozi wanaoagwa (hawapo pichani).
Naibu Msajili Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Aziza Temu akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
Mhe. Fahamu Mtulya akizungumza katika hafla hiyo.
Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya
Mhe. Paul Dandi Ntumo akitoa neno la shukurani katika hafla hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
Mhe. Fahamu Mtulya akikabidhi Zawadi kwa Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo
ya Mbeya Mhe. Judith Timoth Lyimo.
Viongozi wa Mahakama Kuu masjala Ndogo ya Mbeya kushoto
ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Mussa Pomo, Jaji wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Said Kalunde (wa pili kushoto), Jaji Mfawidhi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Fahamu Mtulya (wa pili kulia) na kulia ni Jaji wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe, Angaza Mwipopo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
Mhe, Fahamu Mtulya akimlisha keki Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya, Bi. Mavis Fransis Miti.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni