Jumamosi, 13 Juni 2026

JENGO LA MAHAKAMA YA MWANZO MASUMBWE LAZINDULIWA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, tarehe 11 Juni, 2026, alizindua Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe baada ya ujenzi wake kukamilika, hatua inayotarajiwa kuboresha upatikanaji wa huduma za haki kwa Wananchi wa Wilaya ya Mbogwe na maeneo jirani.

Uzinduzi huo ulipokelewa kwa shangwe na Wananchi wa Masumbwe kutokana na kusogezwa karibu kwa huduma za Mahakama ambazo kwa muda mrefu zilikuwa zikitolewa katika jengo la Ofisi ya Tarafa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, Jaji wa Mahakama Kuu  Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje, Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya, Watumishi wa Mahakama, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mbogwe, Viongozi wa Taasisi mbalimbali pamoja na Wananchi.

Akizungumza katika hafla hiyo, Jaji Mhina alimshukuru Jaji Kahyoza kwa kushiriki uzinduzi huo na kueleza kuwa ushiriki wake unaakisi historia ya usimamizi wa shughuli za Mahakama katika eneo hilo, ambalo hapo awali lilikuwa chini ya Wilaya ya Kahama kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Geita.

Alisema kuwa Mahakama ya Mwanzo Masumbwe ilianzishwa mwaka 1998 wakati eneo hilo likiwa chini ya Wilaya ya Kahama, Mkoa wa Shinyanga, na imeendelea kutoa huduma za haki licha ya kukosa jengo rasmi kwa kipindi kirefu.

“Kwa miaka mingi, Mahakimu na Watumishi wa Mahakama walifanya kazi katika mazingira yasiyokuwa rasmi, huku Wananchi wakipata huduma katika maeneo yenye changamoto za miundombinu. Hata hivyo, hali hiyo haikuwazuia kutekeleza wajibu wao wa msingi wa kusimamia haki,” alisema Jaji Mhina.

Alisisitiza kuwa uwekezaji katika miundombinu ya Mahakama ni msingi wa kuimarisha amani, utulivu na maendeleo ya Taifa, akieleza kuwa haki ndiyo nguzo muhimu ya maendeleo ya jamii.

Aidha, alieleza kuwa ujenzi wa jengo hilo uliwezeshwa kwa kiasi kikubwa na uzalendo wa aliyekuwa Diwani wa Kata ya Masumbwe, Mhe. Shimo Kasheto, ambaye alitoa eneo la ekari mbili kwa ajili ya mradi huo. Pia aliwapongeza Evarist Gervas na wadau wengine waliochangia hatua za awali za ujenzi.

Kwa mujibu wa Jaji Mhina, juhudi za kukamilisha ujenzi ziliongezeka baada ya kuanzishwa kwa Mahakama Kuu Geita mwaka 2023, ambapo uongozi wa Mahakama ulianza kutenga sehemu ya fedha za uendeshaji wa ofisi kwa ajili ya kukamilisha mradi huo.

Katika hafla hiyo, pia ulizinduliwa mfumo wa kidijitali wa kuhifadhi taarifa na majalada ya Mahakama za Mwanzo unaojulikana kama GEITA Repository Database, ambao sasa umeanza kutumika katika Mahakama zote za Mwanzo zilizopo Kanda ya Geita.

Jaji Mhina alisema mfumo huo ulifanyiwa majaribio katika Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu na kuthibitishwa kuwa tayari kwa matumizi rasmi. Alifafanua kuwa mfumo huo utasaidia kuhifadhi taarifa za mashauri, kuzuia upotevu wa majalada na kupunguza ucheleweshaji wa mashauri unaotokana na kusubiri kumbukumbu za mahakama.

Kwa upande wake, Jaji Kahyoza aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu Geita pamoja na Wananchi wa Masumbwe kwa ushirikiano uliowezesha kukamilika kwa mradi huo.

Aliahidi kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama na Wananchi ili kuboresha huduma za Mahakama na kutatua changamoto zilizopo katika Mahakama za Mwanzo.

Naye mMakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Mbogwe alisema Serikali imefanikisha ujenzi wa barabara inayofika katika Mahakama hiyo na kuahidi kusimamia utekelezaji wa mradi wa umeme katika mwaka wa fedha 2026/2027 ili eneo la Mahakama pamoja na makazi ya jirani yaweze kupata huduma ya umeme.

Alieleza kuwa upatikanaji wa umeme utarahisisha utoaji wa huduma za Mahakama na kuchochea maendeleo ya Wananchi wa eneo hilo.

Wananchi waliohudhuria hafla hiyo walieleza kuridhishwa na ubora wa jengo hilo la kisasa na kuomba Serikali pamoja na Mahakama kuendelea kujenga majengo ya Mahakama yenye gharama nafuu katika maeneo ya vijijini na maeneo yenye changamoto za miundombinu ili kusogeza huduma za haki karibu zaidi na Wananchi.

Uzinduzi wa Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe unaonekana kuwa hatua muhimu katika kuimarisha upatikanaji wa haki, kuboresha mazingira ya kazi kwa Watumishi wa Mahakama na kuongeza ufanisi wa utoaji wa huduma za ki,ahakama katika Mkoa wa Geita.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe Kevin Mhina, akikata utepe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, pamoja na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, wakifungua Jiwe la Msingi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, akiutangazia Umma juu ya kuanza kutumika kwa jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, akitoa shukurani kwa uongozi Mahakama Kuu Geita na Wananchi wa Masumbwe kwa kushirikiana kikamilisha mradi huo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, akiwakaribisha wageni katika hafla hiyo.

Wananchi wa Masumbwe wakiongonzwa na ugeni katika zoezi la kukagua mradi wa jengo hilo.

Picha ya pamoja katika Jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe, wakatikati ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Kevin Mhina, wa pili kushoto ni Jaji Mfawidhi wa MahaKama Kuu Shinyanga, Mhe. John Kahyoza, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama kuu Geita, Mhe. Griffin Mwakapeje.

Picha ya pamoja katika jengo la Mahakama ya Mwanzo Masumbwe ngoma ya jadi na wageni katika hafla hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni