Jumapili, 28 Juni 2026

MAFUNZO YA UKATILI WA KIJINSIA YAHITIMISHWA

  • Jaji Kihwelo asisitiza uadilifu

Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo, ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, amehitimisha mafunzo ya siku tatu yaliyolenga kuimarisha uwezo wa Mahakimu katika kushughulikia mashauri ya unyanyasaji na ukatili wa kijinsia kwa kuzingatia utu, heshima na ustawi wa waathirika.

Akifunga mafunzo hayo tarehe 24 Juni, 2026 yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Dodoma, Mhe. Dkt. Kihwelo alisisitiza umuhimu wa Mahakimu kuzingatia uadilifu, weledi na misingi ya haki wakati wa kushughulikia mashauri ya ukatili wa kijinsia ili kuhakikisha waathirika wanapata haki bila kuongeza maumivu ya kisaikolojia.

Jaji Kihwelo alisema mafunzo hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha uelewa wa namna bora ya kuhudumia waathirika wanaofika mahakamani kutafuta haki. Aliwataka washiriki kutumia maarifa waliyojifunza katika utendaji wao wa kila siku ili kuendelea kujenga imani ya wananchi kwa mhimili wa Mahakama.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, aliwashukuru wawezeshaji na washiriki kwa ushiriki wao mzuri na kusisitiza umuhimu wa kuendeleza mafunzo ya aina hiyo ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki kwa makundi yenye uhitaji maalum.

Mafunzo hayo yalihitimishwa kwa ugawaji wa vyeti kwa washiriki, zoezi lililoongozwa na Jaji Kihwelo, kabla ya Viongozi na washiriki kupiga picha ya pamoja kuashiria kufungwa rasmi kwa mafunzo hayo.

Mafunzo hayo yanatarajiwa kuimarisha utoaji wa haki unaozingatia utu wa binadamu, kuongeza uadilifu na weledi katika usikilizaji wa mashauri ya ukatili wa kijinsia, pamoja na kuimarisha ulinzi wa haki za waathirika ndani ya mfumo wa Mahakama.

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt Paul Kihwelo, akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya unyanyasaji wa kijinsia. .

 

Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo, (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wakufunzi wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Joachim Tiganga. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Upendo Ngitiri.


 

Meza kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki. wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri.


 

 Baadhi ya washiriki waliohudhuria mafunzo hayo ya ukatili wa kijinsia wakifuatilia kwa makini mafunzo hayo.

Meza kuu ikiongozwa na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto, ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe, Dkt Paul Kihwelo, (aliyekaa katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo. Aliyeketi kushoto kwake ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Joachim Tiganga, kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Upendo Ngitiri.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni