Jumatatu, 22 Juni 2026

MTENDAJI MKUU AHAIDI KUENDELEZA MAGEUZI YA MAHAKAMA KWA UELEDI, UADILIFU NA UWAJIBIKAJI

Na. HALIMA MNETE – Mahakama

       Apongeza mchango wa Prof. Ole Gabriel, asema ueledi, uadilifu na uwajibikaji vitakuwa msingi wa uongozi wake.

Mtendaji Mkuu mpya wa Mahakama ya Tanzania, Dkt. John Anthony Jingu, ameahidi kuendeleza na kuimarisha mafanikio yaliyofikiwa na Mahakama ya Tanzania kwa kusimamia misingi ya weledi, uwajibikaji na uadilifu katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi.

Dkt. Jingu ametoa kauli hiyo leo tarehe 22 Juni, 2026 katika hafla ya kumpokea kumkaribisha na kumkabidhi rasmi Ofisi ya Mtendaji Mkuu, iliyofanyika katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, ambapo pia alitoa salamu za shukrani kwa Mtendaji Mkuu anayestaafu, Prof. Elisante Ole Gabriel, kwa mchango wake mkubwa katika mageuzi na maendeleo ya Mahakama.

Aidha, Dkt. Jingu, ambaye aliapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 19 Juni 2026 jijini Dar es Salaam, alisema uteuzi wake ni heshima kubwa pamoja na dhamana nzito inayohitaji ushirikiano wa pamoja ili kuhakikisha Mahakama inaendelea kutekeleza wajibu wake wa kikatiba kwa ufanisi.

“Nitumie fursa hii kumshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani aliyonionesha ya kuniteua kushika nafasi hii. Ninaamini kwa kushirikiana na watumishi wote wa Mahakama tutaendelea kuisaidia taasisi hii kutekeleza majukumu yake kwa kiwango kinachotarajiwa na wananchi,” alisema Dkt. Jingu.

Alisisitiza kuwa mafanikio ya Mahakama yanategemea mshikamano wa watumishi wake pamoja na kujengwa kwa utamaduni wa kazi unaozingatia maadili ya utumishi wa umma.

“Kwa kushirikiana kwa pamoja tutafanya kazi kwa weledi, uwajibikaji na uadilifu. Hizi ndizo nguzo zitakazoongoza utendaji wetu katika kuhakikisha huduma za haki zinaendelea kutolewa kwa ubora na ufanisi,” aliongeza.

Akizungumzia mchango wa mtangulizi wake, Dkt. Jingu alimpongeza Prof. Ole Gabriel kwa uongozi wake madhubuti uliowezesha Mahakama kufikia hatua kubwa ya maendeleo ya kiutendaji na kiutawala.

Mtendaji Mkuu huyo mpya, alisema kabla ya kuanza rasmi majukumu yake, alifanya tathmini ya kina kuhusu utendaji wa Mahakama ya Tanzania pamoja na kulinganisha na mifumo ya Mahakama za nchi nyingine, ambapo alibaini kuwa Mahakama ya Tanzania imefikia kiwango cha juu cha utendaji.

“Nilipata nafasi ya kufanya tathmini kuhusu Mahakama ya Tanzania na mifumo ya Mahakama katika nchi nyingine. Kwa hakika, Mahakama ya Tanzania ipo katika kiwango cha juu sana cha utendaji, jambo linaloonesha kazi kubwa iliyofanywa na uongozi uliopita,” alisema Mtendaji Mkuu Dkt. Jingu.

Aidha, Dkt. Jingu alisema, uzoefu na maarifa ya Prof. Ole Gabriel yataendelea kuwa rasilimali muhimu kwa Mahakama hata baada ya kustaafu, akieleza umuhimu wa kuendelea kupata ushauri wake wa mara kwa mara unapohitajika.

“Prof.  Ole Gabriel ni hazina ya uzoefu na maarifa. Tutaendelea kuhitaji ushauri wake, nasaha zake na mchango wake katika safari ya kuijenga Mahakama imara zaidi. Tunaamini ataendelea kuwa karibu nasi,” aliongeza Mtendaji Mkuu.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Mahakama akiwemo  Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania  Mhe. Eva Nkya, wajumbe wa menenjimenti ya Mahakama pamoja na watumishi kutoka idara na vitengo tofauti, waliomkaribisha Dkt. Jingu na kuonesha utayari wa kuendelea kushirikiana naye katika kuimarisha utoaji wa huduma za haki nchini.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni