Jumatano, 10 Juni 2026

MTENDAJI MKUU APONGEZA MAFANIKIO YA TIMU ZA MICHEZO ZA MAHAKAMA


·        Zaibuka na Vikombe Vinne katika Mashindano ya Mei Mosi 2026

Na. JAMES BUSANYA & HALIMA MNETE – Mahakama, Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, amewapongeza watumishi wa Mahakama walioshiriki kuiwakilisha Taasisi hiyo katika Mashindano ya Michezo ya Mei Mosi mwaka 2026.

“Nawaagiza ama kutoa maelekezo kwa viongozi wa Mahakama katika ngazi mbalimbali kuhakikisha wanawapa watumishi muda wa kufanya mazoezi ili kuendeleza vipaji vyao, kuimarisha afya na kuongeza ushindani wa timu za Mahakama,” amesema Mtendaji Mkuu.

Prof. Ole Gabriel ametoa maagizo leo tarehe 10 Juni, 2026, katika hafla ya kupokea rasmi vikombe vinne vya ushindi vilivyotwaliwa na timu za Mahakama ambazo ni timu ya Karata, Timu ya kamba wanawake, timu ya Baiskeli na timu ya mchezo wa bao kwenye mashindano ya Mei Mosi mwaka 2026 yaliyoshirikisha timu 51 kutoka taasisi mbalimbali za Serikali.

Mashindano hayo yalianza tarehe 13 Aprili, 2026 mkoani Njombe na kufunguliwa na aliyekuwa Naibu Waziri wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi Ajira na Mahusiano, Mhe. Rahma Kisuo na kufungwa rasmi Mei 1, 2026 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika hafla hiyo ya kupokea vikombe na zawadi za mashindano, Prof. Ole Gabriel amesema anawasilisha salamu za pongezi kutoka kwa Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju, na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani kwa wanamichezo wote waliowakilisha Mahakama kwa mafanikio.

“Hayo ni matokeo ya kujituma, nidhamu na mshikamano mkubwa miongoni mwa wanatimu. Mmeitangaza vyema Mahakama na kutuletea heshima kubwa,” amesisitiza Mtendaji Mkuu.

Katika mashindano hayo, timu ya wanawake ya Mahakama ilifanya vizuri kwa kuibuka mshindi wa kwanza katika mchezo wa karata, mshindi wa pili katika mbio za baiskeli, na kushika nafasi ya tatu katika michezo ya kamba na bao. Mafanikio hayo yaliifanya Mahakama kuwa miongoni mwa taasisi zilizofanya vizuri katika mashindano hayo ya kitaifa ya wafanyakazi.

Akitolea ufafanuzi wa taarifa ya Katibu wa Timu ya Michezo ya Mahakama iliyobainisha changamoto za ukosefu wa muda wa mazoezi na uhaba wa vifaa vya michezo, Mtendaji Mkuu aliiagiza Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu (DARHM) kushughulikia changamoto hizo.

“Viongozi wa utawala wanapaswa kuhakikisha wanatoa ushirikiano unaohitajika kwa wanamichezo wetu. Suala la vifaa vya michezo litazingatiwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027,” aliongeza Prof. Ole Gabriel.

Aidha, Prof. Gabriel alieleza kufurahishwa na ushiriki wa Mahakimu katika timu hiyo, akisisitiza kuwa michezo haina mipaka ya kada wala cheo. Mahakama ina watumishi takribani 7,000. Hiyo ni hazina kubwa ya vipaji ambayo vinaweza kutuwezesha kujenga timu imara zitakazoshindana na timu kubwa nchini kama Simba na Yanga katika miaka ijayo. Mtendaji Mkuu huyo alisisitiza umuhimu wa nidhamu kwa wanamichezo, akibainisha kuwa wao ni mabalozi wa taasisi wanayoitumikia na mfano kwa jamii.

Akitoa mfano wa uzoefu wake binafsi, alisema aliwahi kuwa mchezaji bora wa mpira wa wavu mwaka 1992, jambo linalompa uelewa wa kina kuhusu mchango wa michezo katika maendeleo ya mtu binafsi na taasisi.

“Michezo huimarisha afya ya mwili na akili, hujenga mahusiano ya kijamii na ustawi wa kiroho, na huongeza mshikamano mahali pa kazi kwa kuwaondoa watumishi katika mipaka ya vyeo na kada wanapokuwa uwanjani. Aliongeza kuwa Serikali hii chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuhimiza ushiriki wa michezo kama sehemu muhimu ya maendeleo ya afya na ustawi wa wananchi,” amebainisha Prof. Ole Gabriel.

Vilevile, Prof. Ole Gabriel aliwashukuru viongozi na wasaidizi wake akiwemo Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu pamoja na Mkurugenzi wa Mipango na Uratibu, kwa mchango wao wa kusaidia timu. Uongozi utaendelea kutoa ushirikiano na msaada unaohitajika ili kuimarisha maendeleo ya michezo. Akawahimiza watumishi kuifanya michezo kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku na si kwa ajili ya mashindano pekee.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa makabidhiano rasmi ya vikombe vya ushindi na pongezi kwa wanamichezo walioiwakilisha Mahakama kwa mafanikio katika Mashindano ya Mei Mosi ya mwaka 2026.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza wakati wa kuwapongeza watumishi wa Mahakama walioshiriki kuiwakilisha Taasisi katika Mashindano ya Michezo ya Mei Mosi mwaka 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe leo tarehe 10 Juni, 2026 katika ukumbi wa mikutano ndani ya Jengo la Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akikabidhiwa Kikombe na mmoja ya mchezaji na washiriki wa mashindano ya mei mosi 2026 leo tarehe 10 Juni, 2026 Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, (kulia) akitoa cheti cha pongezi kwa mtumishi wa Mahakama aliyeshiriki mashindano ya Mei Mosi mwaka 2026 mkoani Njombe.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa amepozi kwenye picha na vikombe alivyokabidhiwa na timu ya Mahakama Sports
Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports mara baada ya hafla ya kukabidhi vikombe na tunzo walizoshinda kwenye mashindano ya Mei Mosi ya Mwaka 2026 yaliyofanyika mkoani Njombe, wengine Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu (DARHM) Beatrice Patrick (kulia) na kushoto ni Mkurugenzi wa Mipango na Uratibu Bw. ErasmusUisso

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha -Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni