Alhamisi, 11 Juni 2026

VIONGOZI WA MAHAKAMA KUU KATAVI WAFANYA ZIARA YA KIMAHAKAMA GEITA

Na DOTTO NKAJA – Mahakama, Geita

Viongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Katavi, wakiongozwa na Jaji Mfawidhi, Mhe. Godfrey Isaya, tarehe 9 Juni 2026 walitembelea Masjala Ndogo Geita kwa lengo la kubadilishana uzoefu katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Viongozi hao walipokelewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Geita, Mhe. Kevin Mhina, ambaye alimshukuru Mhe. Isaya kwa kuona umuhimu wa kuambatana na Watumishi wa Mahakama hiyo katika ziara ya mafunzo.

Alisema kuwa Mahakama Geita hufarijika na kupata hamasa kubwa inapopokea wageni kutoka maeneo mbalimbali, kwani hali hiyo huchochea ubunifu unaosaidia kurahisisha utoaji wa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu.

Mhe. Mhina alieleza kuwa ili Taasisi yoyote ifanikiwe kufikia malengo yake, ni muhimu kuzingatia mambo mawili makuu, ambayo ni kujitoa kwa dhati katika kutekeleza majukumu ya kazi, na kuwa na usimamizi madhubuti, ufuatiliaji endelevu pamoja na utoaji wa motisha kwa watumishi.

Alisisitiza umuhimu wa mafunzo ya ndani na nje ya Taasisi kwa lengo la kuongeza uwezo na ufanisi wa watumishi.

Kwa upande wake, Mhe. Isaya alisema kuwa mafanikio yanayoonekana Geita yametokana na namna Watumishi walivyoithamini kazi yao na kujituma katika utekelezaji wa majukumu yao.

Aliongeza kuwa Mhe. Mhina ni Kiongozi mwenye uwezo mkubwa wa kupanga, kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa shughuli mbalimbali za Mahakama.

“Nawaomba Watumishi wa Mhakama Katavi tujifunze kila jambo tuliloliona hapa Geita na kuangalia namna Watumishi wa Geita walivyoamua kufanya kazi kwa kutambua kuwa kazi yao ni wito wa kuhudumia Mwananchi,” alisema Mhe. Isaya.

Naye Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Katavi, Bi. Silivia Lushasi, aliwashukuru Viongozi na Watumishi wa Geita kwa maandalizi mazuri ya mafunzo hayo pamoja na uwasilishaji wa mada mbalimbali zilizokuwa na manufaa makubwa kwa washiriki.

“Kwa kweli nimejionea jinsi wawasilishaji wa mada walivyo na uelewa mkubwa katika maeneo yao ya kazi. Hali hiyo imetufanya tukose hata maswali ya kuuliza kwa sababu kila jambo limeelezwa kwa uwazi na kwa ufasaha mkubwa,” alisema. Aidha, aliahidi kuwa watakwenda kutekeleza mafunzo hayo mara watakaporejea katika vituo vyao vya kazi.

Katika mafunzo hayo, mada mbalimbali ziliwasilishwa na wakuu wa vitengo tofauti. Miongoni mwao alikuwa Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, ambaye aliwasilisha mada kuhusu matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri (E-Case Management System) na kueleza namna mfumo huo unavyosaidia kukabiliana na changamoto za usimamizi na ufuatiliaji wa kesi katika ngazi zote za Mahakama.

Pia, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Geita, Mhe. Devotha Kasebele, kwa niaba ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Mujuni Muchunguzi, aliwasilisha mada iliyosisitiza kuwa mafanikio ya matumizi ya TEHAMA yanategemea ushirikiano mzuri kati ya Viongozi na Watumishi.

Kwa upande mwingine, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Nyankumbu, Mhe. Ally Mgomba, alieleza jinsi Mahakama za Mwanzo Geita zilivyofanikiwa kuondokana na matumizi makubwa ya karatasi kwa kubuni mfumo maalum wa kidijitali unaorahisisha utendaji wa kazi katika Mahakama.

Mada nyingine iliwasilishwa na Mtendaji wa Mahakama, Bi. Masalu Kisasila, ambaye alifafanua matumizi ya TEHAMA katika uendeshaji wa shughuli za kiutawala.

Naye Afisa Mtunza Kumbukumbu, Bi. Anitha Mwanilunga, alieleza namna dirisha la KIOSK linavyowasaidia wateja wasio na Mawakili na wasiojua kusoma kusajili na kufuatilia mashauri yao kwa urahisi.

Aidha, Afisa TEHAMA, Bw. Dotto Nkaja, aliwasilisha mada kuhusu mfumo wa kuhifadhi taarifa za Mahakama za Mwanzo, akieleza jinsi mfumo huo unavyosaidia kuondoa changamoto za kuitisha majalada kutoka Mahakama za chini pindi yanapohitajika katika Mahakama za juu.

Ziara hiyo imekuwa fursa muhimu ya kujifunza na kubadilishana uzoefu, huku ikionesha dhamira ya Mahakama ya Tanzania katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA kwa lengo la kuboresha utoaji wa haki nchini.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Geita, Mhe. Kevin Mhina, akitoa historia fupi ya maendeleo ya TEHAMA Geita kwa Watumishi Mahakama Kuu Katavi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Geita akitoa ufafananuzi juu ya matumizi ya mifumo Geita.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Katavi, Mhe Godfrey Isaya, (wa kwanza kushoto) akitoa pongezi Kwa Jaji Mfawidhi Geita juu ya maendeleo ya TEHAMA.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Katavi, Mhe Silivia Lushasi akichangia hoja juu ya mada iliyowasilishwa wakati wa ziara hiyo.

Watumishi wa Mahakama Kuu Katavi wakisikiliza taarifa fupi inayohusu mafanikio ya TEHAMA wakati wa ziara hiyo.

Picha ya pamoja ya Watumishi wa Mahakama Kuu Geita na Katavi wakati wa ziara hiyo iliyofanyika Mahakama Kuu Geita.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Arusha.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni