Na ARAPHA RUSHEKE, Mahakama-Dodoma
Mahakama Kuu ya
Tanzania Masjala Ndogo Dodoma imefanya hafla ya kuwakaribisha Majaji
pamoja na Watumishi waliohamia katika Mahakama hiyo na kuwaaga
waliohamishwa kutoka Mahakama hiyo.
Hafla
hiyo ilifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita katika Ukumbi wa 'Royal
Village' jijini Dodoma na kuwakutanisha Majaji, Wasajili, Viongozi na
Watumishi wa Mahakama kutoka katika Vituo mbalimbali vya Mahakama Dodoma
ililenga kuwaaga watumishi waliopata uhamisho pamoja na kuwakaribisha wale
waliopangiwa kuanza majukumu katika Mahakama hiyo.
Miongoni mwa
Viongozi waliohudhuria hafla hiyo walikuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe.
Dkt. Juliana Masabo ambaye alikuwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma aliagwa
kufuatiwa kuteuliwa kwake kuwa Jaji wa Rufani, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu
Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga aliyekaribishwa baada ya kuhamia Dodoma kuwa
Mfawidhi wa Masjala hiyo, Jaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya
Biashara, Mhe. Evarist Longopa ambaye aliagwa baada ya
kuhamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Biashara Dar es Salaam.
Viongozi wengine
waliohudhuria sherehe hiyo ni Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma,
Mhe. Biswalo Mganga, Mhe. Suleiman Hassan, Mhe. Irene Musokwa pamoja
na Viongozi wengine wa Mahakama hiyo.
Kulikuwa pia na
Watumishi wa kada mbalimbali ambao wameagwa na kukaribishwa,
watumishi hao ni pamoja na wa Kada za Watunza kumbukumbu, Wasaidizi wa Ofisi,
Madereva, Mwandishi Mwendesha Ofisi pamoja na Wasaidizi wa Sheria.
Shughuli za hafla
zilianza kwa kuwasili kwa wageni waalikwa na wageni rasmi, zikafuatiwa na dua
fupi, utambulisho wa wageni, kukata keki na shughuli mbalimbali za kijamii
zilizolenga kuimarisha mshikamano na ushirikiano miongoni mwa watumishi wa
Mahakama pamoja na wadau .
Aidha, wageni
walipata fursa ya kutoa salamu za pongezi na shukrani, kutoa zawadi kwa
wahusika pamoja na kusikiliza nasaha na hotuba zilizosisitiza umuhimu wa
kudumisha maadili, uwajibikaji na ushirikiano katika utoaji wa huduma za haki
kwa wananchi.
Hafla hiyo
ilipambwa na shamrashamra pamoja na muziki kutoka Bendi ya Magereza Dodoma
ambao ni Wadau wakubwa wa Mahakama.
Hafla hiyo
ilihitimishwa kwa kupata chakula cha pamoja na burudani ya muziki, ambapo
washiriki walipata nafasi ya kuendelea kujenga mahusiano mema na kuimarisha
umoja ndani ya familia ya Mahakama.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt Juliana Masabo (kulia) akisikiliza kwa makini ujumbe wa zawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma ambayo iliwasilishwa kwake na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga wakati wa sherehe ya kuwaaga na kuwakaribisha Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma iliyofanyika katika ukumbi wa Royal Village jijini Dodoma.
Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe.Dkt Juliana Masabo wa kwanza kulia akisikiliza kwa makini ujumbe wa zawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma ambayo iliwasilishwa kwake na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Dodoma Mhe Joachim Tiganga wakati wa sherehe hiyo.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masajala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (kulia) akipokea dhawadi yake kutoka kwa Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma iliyowasilishwa kwake na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Biswalo Mganga wakati wa sherehe hiyo.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)






Hakuna maoni:
Chapisha Maoni