Jumatano, 29 Julai 2026

TMJA DODOMA YAKUTANA, YASISITIZA UMOJA, KUSHIRIKI MAFUNZO NA KUJIBIDIISHA KIELIMU

Na ARAPHA RUSHEKEMahakama-Dodoma

Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma chini ya Mwenyekiti wake, Mhe. Faisal Kahamba hivi karibuni walifanya kikao cha wanachama wote kilicholenga kujadili maendeleo ya tawi hilo, kuimarisha mshikamano wa wanachama pamoja na kujengeana uwezo katika utekelezaji wa majukumu ya kimahakama

Kikao hicho kilichohudhuriwa na wanachama wa TMJA kutoka Mahakama mbalimbali za Mkoa wa Dodoma kilifanyika kwenye Ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma.

Miongoni mwa ajenda muhimu za kikao hicho ilikuwa ni kuwapokea Wanachama wapya 11 wakiongozwa na Mlezi mpya wa TMJA Dodoma ambae ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga ambaye amehamishiwa katika Kituo hicho hivi karibuni akitokea Mahakama Kuu Masjala Ndogo Mbeya.

Akizungumza wakati akitoa salamu zake, Jaji Mfawidhi na Mlezi wa TMJA Dodoma, Mhe. Tiganga alisema, “ninafurahi kuwa sehemu ya familia hii lakini pia niwashukuru Viongozi kwa kuandaa kikao hiki muhimu kwangu mimi ni kikao muhimu sana kwani karibia wanachama wote mmekuja na tumeonana, niwapongeze kwa umoja huu sio kitu rahisi kupata wajumbe wengi namna hii, wote tunafahamu umuhimu wa kuwa na chama kilicho hai na chenye malengo yanayotekeleza wanachama wenye utayari wa kutekeleza malengo hayo.”

Amesisitiza kuwa, pamoja na mafunzo wanayoyaandaa Wanachama hao wajitahidi kuhudhuria mafunzo wanapopata nafasi kwa kuwa ni muhimu lakini pia kila mmoja aendelee kujiongezea elimu na kujifunza kwani elimu haina mwisho.

Vilevile Mhe. Tiganga aliendelea kusema, “kila mmoja wetu ajitahidi kujibidiisha lengo ni kwamba pamoja na kuhakikisha kazi za Mwajiri zinakwenda vizuri tujiandae kukua kitaaluma pia ni vizuri kutambua tunao Mfumo unaotupima JOPRAS, mpimaji anajaza eneo dogo sana hasa la maadili kwa kiasi kikubwa mfumo wenyewe unakupima kutokana na utendaji wako wa kazi unachakata zile taarifa za kwenye mfumo kwahiyo niwakumbushe na tuendelee kufahamu kwamba kujibidiisha ndipo kutafanya tuonekane kuwa utendaji kazi wetu umebadilika mnatakiwa mfahamu kuwa hatutakiwi kumuacha mtu yoyote nyuma hivyo tushirikiane kwa muda wote ushauri na kila kitu kama mlezi na kiongozi wenu wa sasa napenda ushirikiano na ninapenda kila mmoja wenu asonge mbele.”

Jaji Mfawidhi huyo amewahakikishia Wana TMJA Tawi la Dodoma kuwa ataendelea kuwa mlezi na mshauri lakini pia atatekeleza wajibu wake kama Mwanachama kama ambavyo Katiba inamtaka pamoja na miongozo inavyotaka huku akisisitiza suala la uhai wa Chama liwe la msingi sana na kuhakikisha chama hicho kinakuwa imara.

Kikao hicho kiliambatana na mafunzo kuhusu mbinu za uchukuaji wa ushahidi wakati wa usikilizaji wa mashauri ya jinai, yaliyowasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Suleiman Hassan.

Katika Mafunzo hayo Viongozi na Wajumbe mbalimbali walichangia, akiwemo Mhe. Tiganga, Mhe. Biswalo Mganga (Jaji), Mhe. Irene Msokwa (Jaji).

Washiriki walieleza kuwa mafunzo hayo yameongeza uelewa na yatachangia kuboresha utoaji haki kwa kuzingatia misingi ya sheria na weledi.

Mbali na mafunzo hayo, Wanachama walijadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya Tawi, hususan namna ya kuendelea kuimarisha umoja, mshikamano na upendo miongoni mwa Wanachama.

Akizungumza wakati wa kufunga mjadala huo, Mwenyekiti wa TMJA Dodoma, Mhe. Faisal Kahamba, aliwahimiza wanachama kuendelea kutekeleza maazimio ya vikao vya TMJA na kushiriki kikamilifu katika shughuli zote za Chama kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na mafanikio ya Tawi.

Vilevile, wanachama walikumbushwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia kaulimbiu ya Mahakama ya Tanzania isemayo "Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji," ambayo ndiyo msingi wa utoaji wa huduma bora za haki kwa wananchi.

Katika kikao hicho pia, wajumbe walihimizwa kushiriki kwa wingi katika ziara ya Bagamoyo inayotarajiwa kufanyika mwezi Septemba, 2026 ambayo itaambatana na Bonanza la kuimarisha afya, ushirikiano na mahusiano miongoni mwa Wanachama wa TMJA.

Kwa upande mwingine, Wanachama walitoa pongezi kwa uongozi wa TMJA Dodoma kwa kuendelea kusimamia matendo ya huruma katika jamii. Kupitia programu hiyo, tawi limefanikiwa kutoa misaada mbalimbali ikiwemo vyakula, nguo, magodoro na vifaa tiba kwa taasisi zenye uhitaji katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Dodoma katika kipindi cha mwaka 2024 hadi 2026.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa wito uliotolewa kwa Wanachama kuendelea kudumisha mshikamano, kuongeza ushirikiano na kutekeleza majukumu yao kwa weledi ili kuendeleza mafanikio ya TMJA Dodoma na Mahakama ya Tanzania kwa ujumla.


 Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa  Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyesimama katikati mstari wa mbele) na Viongozi na Wajumbe wa TMJA mkoani huo mara baada ya kikao.

 

Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa  Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akiwasilisha hotuba yake kwa wajumbe wa TMJA Dodoma wakati wa kikao chao kilichofanyika hivi karibuni.


Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba akiwasilisha hotuba ya ufunguzi wa kikao wakati wa kikao hicho.

  Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TMJA Tawi la Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma ambapo pia ni Wanachama wa TMJA, aliyesimama kushoto ni Mhe. Biswalo Mganga, katikati ni Mhe. Irene Musokwa na kulia ni Mhe. Mhe. Suleiman Hassan. Walioketi na Jaji Mfawidhi kushoto  ni Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba na kulia ni Katibu wa Chama hicho, Mhe Getrude Misana. 

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi  wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TMJA Tawi la Dodoma,  Mhe. Joachim Tiganga (aliyeketi katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na 
Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Bw. Bedson Mariba (aliyesimama). Walioketi kushoto ni Mwenyekiti wa Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Dodoma, Mhe. Feisal Kahamba na kulia ni Katibu wa Chama hicho, Mhe. Getrude Misana. 


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni