Ijumaa, 31 Julai 2026

JAJI KAHYOZA ATETA NA MAWAKILI MASJALA NDOGO GEITA

Na DOTTO NKAJA, Mahakama - Geita

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza, Julai 28, 2026, amekutana na kufanya mazungumzo na Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea mkoani Geita katika kikao kilichofanyika kwenye Ukumbi wa Mafunzo wa Mahakama Kuu Geita kwa lengo la kujengeana uwezo na kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa haki.

Akifungua kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa kuitikia wito na kueleza kuwa mkutano huo ulilenga kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama na wadau wa sheria, kujadiliana masuala yanayohusu utoaji wa haki, kubadilishana uzoefu kuhusu matumizi ya mifumo ya Mahakama pamoja na kufahamiana, kwa kuwa yeye ni mgeni katika Masjala Ndogo ya Geita.

Alisema uwepo wa wadau wengi wa sheria mkoani Geita ni fursa muhimu ya kuendeleza utoaji wa haki kwa ufanisi na kuongeza kuwa Mahakama ya Geita imeendelea kuwa mstari wa mbele katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha utoaji wa huduma za Mahakama.

Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa mifumo mbalimbali ya TEHAMA kusomana na kufanya kazi kwa pamoja ili kuongeza ufanisi na kuboresha huduma kwa watumiaji. Aidha, aliwahimiza mawakili kuanza kutumia Kiapo cha Ushahidi (Witness Statement), hususan katika mashauri ya madai, akieleza kuwa utaratibu huo unasaidia kuharakisha usikilizaji na utoaji wa maamuzi ya mashauri.

Pia aliwataka mawakili kuendelea kutoa taarifa na mapendekezo wanapokutana na changamoto katika matumizi ya mifumo ya Mahakama ili zipatiwe ufumbuzi kwa wakati.

Kwa upande wake na kwa niaba ya mawakili, Wakili Marina Mashimba aliipongeza Mahakama ya Geita kwa maboresho ya mifumo ya kidijiti ambayo imepunguza gharama na muda wa uwasilishaji wa mashauri. Alipendekeza pia kuimarishwa kwa ushirikiano wa mifumo ya Mahakama na taasisi nyingine za utoaji wa haki, ikiwemo Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) pamoja na Mabaraza ya Ardhi.

Aidha, aliomba mafunzo ya mara kwa mara kwa mawakili ili kuwaongezea uwezo wa kitaaluma na kuwawezesha kupata alama za maendeleo endelevu ya taaluma kupitia chama chao cha kitaaluma.

Naye, Wakili George Alfred aliipongeza Mahakama kwa maboresho ya huduma, huku akiainisha baadhi ya changamoto zinazojitokeza katika matumizi ya mfumo wa kielektroniki. Alieleza kuwa, baadhi ya kampuni hazionekani wakati wa usajili wa mashauri, baadhi ya vijiji havipo kwenye mfumo, na wakati mwingine mfumo humtambua wakili anayesajili shauri kama mlalamikaji badala ya mwakilishi wa mlalamikaji. Alisisitiza umuhimu wa kuwawezesha mawakili kutumia kikamilifu mifumo ya kielektroniki ili kupunguza matumizi ya karatasi na kuongeza ufanisi.

Akijibu hoja hizo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna, alisema changamoto zote zilizowasilishwa zimepokelewa na zitafanyiwa kazi. Alieleza kuwa, changamoto zinazohusu mashauri ya mirathi, nyaraka kutokuonekana kwenye mfumo pamoja na usajili wa kampuni zitawasilishwa kwa wajenzi wa mfumo ili zipatiwe ufumbuzi.

Akihitimisha kikao hicho, Mhe. Kahyoza aliwashukuru mawakili kwa ushiriki wao na maoni yao yaliyolenga kuboresha huduma za Mahakama. Aliwahimiza kuendelea kutoa taarifa kuhusu changamoto wanazokutana nazo, kuimarisha ushirikiano na Mahakama, pamoja na kutumia huduma za usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa haki.

Aidha, aliwakumbusha mawakili umuhimu wa kufanya mazoezi na kushiriki michezo mbalimbali ili kuimarisha afya ya mwili na kuongeza ufanisi katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Projestus Kahyoza (katikati mbele) akiwakaribisha Mawakili wa Serikali na Mawakili wa Kujitegemea katika kikao kazi hicho cha kujadili mambo mbalimbali ya kiutendaji.


Wakili wa Serikali  Wakili Msomi George Alfred (aliyesimama) akichangia hoja.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Geita, Mhe. Fredrick Lukuna akijibu maswali na hoja mbalimbali zilizoibuliwa na Mawakili katika kikao kazi hicho.

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Geita Bi. Masalu Kisasila aliyesimama akitoa shukurani kwa ushirikiano mzuri katika uendeshaji wa shughuli za kiutawala baina ya Mawakili na Uongozi wa Mahakama. 


Wakili wa Serikali Bw. Robert Neophitus (aliyesimama) akitoa maoni juu ya Mfumo wa kielektroniki wa kusimamia Mashauri (e-CMS).

(Habari Hii Imehaririwa na INNOCENT KANSHA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni