Na. MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Mahakama
ya Rufani ya Tanzania imefanya kikao cha tathmini ya utekelezaji wa shughuli za
usikilizaji wa mashauri ya Rufaa za madai katika Masjala Ndogo ya Mbeya, ikiwa
ni sehemu ya maandalizi ya kuhitimisha rasmi kikao cha Mahakama hiyo
kilichoanza Juni 18, 2026 na kinachotarajiwa kumalizika Julai 17, 2026.
Kikao
hicho kiliongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Winfrida
Korosso, na kuhudhuriwa na Waheshimiwa Majaji wa Rufani walioambatana naye
katika kikao hicho ambao ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe, Dkt. Mary
Levira, Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe Agnes Mgeyekwa, na Viongozi
wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.
Kutoka Mahakama
Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliohudhuria ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu,
Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo
ya Mbeya Mhe. Said Kalunde, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe.
Mussa Pomo.
Wengine
ni Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo, Naibu
Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Kaimu Mtendaji wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bi. Sarah Lossi na wadau wengine wa haki
madai.
Akiwasilisha
taarifa ya utekelezaji wa kikao hicho, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani ya
Tanzania, Mhe. Agatha Chugulu alisema kuwa, kati ya mashauri 48 yaliyopangwa
kusikilizwa, mashauri 32 sawa na asilimia 67 yameshasikilizwa. Kati ya hayo,
mashauri 23 yameshapatiwa maamuzi, huku mashauri tisa (09) yakisubiri kutolewa
maamuzi kwa mujibu wa taratibu za Mahakama.
Aidha,
alieleza kuwa, mashauri 16 yaliahirishwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo
wito wa Mahakama kutowafikia baadhi ya wadaawa kwa wakati kwa mujibu wa matakwa
ya sheria, mapungufu katika maandalizi ya kumbukumbu za rufaa pamoja na
kutokuwapo kwa baadhi ya nyaraka muhimu, hali iliyolazimu wahusika kuongezewa
muda wa kufanya masahihisho.
Katika
tathmini hiyo, ilibainika kuwa baadhi ya mawakili hawakutumia ipasavyo mamlaka
ya Ofisi ya Msajili na Naibu Wasajili wa Mahakama ya Rufani kutatua changamoto
za mashauri yao kabla ya tarehe za usikilizaji. Vilevile, baadhi yao
hawakufanya maandalizi ya kutosha mapema, jambo lililosababisha kasoro ambazo
zingeweza kubainika mapema au kujitokeza wakati wa usikilizaji na hivyo
kuchelewesha utoaji wa haki kwa wakati.
Aidha,
pamoja na changamoto hizo, kikao kilieleza kuridhishwa na mafanikio
yaliyopatikana, ikiwemo kusikilizwa kwa mashauri 32 kati ya 48 yaliyopangwa
pamoja na ushirikiano mzuri uliooneshwa na Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea
waliohudhuria kwenye vikao hivyo kwa wakati. Mafanikio hayo yameendelea
kuimarisha juhudi za Mahakama ya Rufani ya Tanzania za kuongeza ufanisi katika
usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa wakati mapema
ipasavyo.
Jopo
la Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Rufani wakiwa kwenye kikao cha tathmini ya
uendeshaji wa mashauri ya madai 48 yaliyendeshewa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya, katikati ni Mwenyekiti wa Jopo hilo Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Winifrida Beatrice Korosso, kulia ni Jaji
wa Mahakama ya Rufani Mhe. Agnes Zephania Mgeyekwa na kushoto ni Jaji wa
Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Mary Calorine Levira.
Jaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde (katikati) akizungumza
jambo katika kikao hicho, kulia ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, na kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya
Mbeya Mhe. Mussa Pomo.
Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Mhe.
Agatha Chugulu (aliyesimama) akiwasilisha taarifa katika kikao hicho, kulia ni Naibu
Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo
Sehemu
ya Wadau walioshiriki katika kikao hicho cha tathmini ya uendeshaji mashauri ya
rufaa za Madai Masjala Ndogo Mbeya
Sehemu ya Wadau walioshiriki katika kikao hicho cha tathmini ya uendeshaji mashauri ya rufaa za Madai Masjala Ndogo Mbeya.
Naibu
Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer (kushoto), na kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi
Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Tedy Mlimba waikifuatilia kikao hicho.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni