Jumatano, 1 Julai 2026

KITUO JUMUISHI TEMEKE, MFUKO WA FIDIA KWA WAFANYAKAZI WABADILISHANA UZOEFU

  • Waweka mikakati kuboresha utoaji haki kwenye mashauri ya mirathi, madai ya fidia

Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Temeke

Mahakama Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke hivi karibuni kilishiriki mafunzo ya kubadilishana uzoefu na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ili kuongeza ufanisi katika kuwahudumia wananchi, hasa katika utoaji wa haki zinazohusu fidia katika mashauri ya mirathi.

Mafunzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Destiny Hall ulioko Kibaha katika Mkoa wa Pwani yalifunguliwa rasmi Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mhe. Mwanabaraka alisisitiza kuwa lengo la mafunzo hayo ni kutatua changamoto za ucheleweshaji wa haki kwa warithi na kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji kati ya Taasisi hizo mbili. 

Katika Kikao hicho, mada ziliwasilishwa kuhusu Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi, Taratibu na changamoto za madai ya fidia kwa wafanyakazi pamoja na taratibu za ufunguaji na uendeshaji wa mashauri ya mirathi.

Bw. Deo Victor Ngowi kutoka Idara ya Huduma za Sheria WCF, akiwasilisha mada kuhusu sheria inayoongoza fidia kazini, alitoa ufafanuzi kuwa fidia hutolewa na WCF kutokana na ajali au vifo kazini na hivyo haiwezi kudaiwa kama sehemu ya mirathi na wasimamizi wa mirathi.

Alieleza pia kuwa fedha hizo hazilipwi kwenye akaunti ya mirathi, bali huenda moja kwa moja kwenye akaunti binafsi za wanufaika sahihi.  Bw. Ngowi alichambua makundi muhimu yanayolipwa na WCF ambayo ni wenza na watoto wenye umri chini ya miaka 18.

Aidha, alieleza kuwa madai yote ya fidia ni lazima yawasilishwe WCF ndani ya miezi 12 tangu kutokea kwa ajali au kifo kwa mnufaika wa WCF.

Bw. Ngowi aliwaelimisha washiriki pia juu ya nani hufaa kuwa wanafaika wa WCF kwa kusema kuwa, “WCF haihusiki na wafanyakazi wa sekta isiyo rasmi kama mikataba ya chini ya siku 30, wafanyakazi wa kujitolea, pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama.”

Meneja Msimamizi wa Ulipaji Fidia, Bi. Rehema Mwakabongo, alipokuwa akiwasilisha mada, alieleza faida mbalimbali zitolewazo na mfuko huo, ikiwemo gharama za matibabu ya ulemavu wa muda au wa kudumu, msaada wa matibabu nje ya nchi, na fao la mazishi.

Alieleza changamoto zinazojitokeza katika ulipaji wa fidia kama udanganyifu kutoka kwa wanufaika, ikiwemo uwepo wa nyaraka zaidi ya moja ya cheti cha kifo, changamoto ya utofauti wa majina ya walipwaji, hivyo kusababisha uwepo wa ‘deed poll’ za udanganyifu.

Bi. Rehema alielezea pia changamoto ya waajiri na waajiriwa kuchelewa kuwasilisha nyaraka muhimu kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wakati, hivyo kuomba ushirikiano mkubwa na Mahakama pale inapohitajika.

Katika kikao hicho, mada kuhusu utaratibu wa ufunguaji mashauri ya mirathi, uendeshaji hadi kufungwa zilitolewa na  Mahakimu, Mhe. Stephanie Kagaruki Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Mwanzo, kwa kushirikiana na Mhe. Mhangwa Yunge, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya.

Mahakimu hao walifafanua mada juu ya taratibu za ufunguaji na uendeshaji wa mashauri ya  mirathi, taratibu na mamlaka za Mahakama kulingana na ngazi zake.

Mahakama za Mwanzo husikiliza mirathi ya kiislamu na ile ya mila na desturi, Mahakama za Wilaya na Mahakama Kuu husikiliza mirathi ya kikristo na asili ya kiasia.

Pia watoa mada walieleza juu ya nyaraka zinazoweza kutumika ili WCF itoe malipo, nyaraka za Mahakama kama vile fomu namba 80 kwa Mahakama Kuu na Wilaya pamoja na Fomu No.5 kwa Mhakama ya Mwanzo zinazoonyesha orodha ya mali za marehemu.

Fomu No.81 kwa Mahakama Kuu na Wilaya pamoja na Fomu No. 6 kwa Mahakama ya Mwanzo zinazoonyesha hesabu za mali ya marehemu ikiwaonyesha wanufaika na walichopewa.

Watoa mada walisema muhtasari wa kikao cha familia sio takwa la kisheria bali hutumika kama utaratibu wa kujiridhisha. Walieleza pia hukumu inaweza kuwa nyaraka muhimu, lakini sio inayowataja warithi halisi, hivyo ni muhimu kuthibitisha wanaostahili kulipwa.

Watoa mada walieleza kuwa hakuna haja ya msimamizi wa mirathi kuagizwa hati ya kiapo cha uthibitisho kwa kuwa hati ya usimamizi wa mirathi kutoka mahakamani ni uthibitisho tosha kuwa ameteuliwa na Mahakama.

Washiriki wa mafunzo hayo walipata nafasi ya kujadili juu ya mada zilizowasilishwa na kuibua maswali muhimu kama vile stahiki za watoto waliozidi miaka 18 wenye changamoto maalumu za kuwafanya kuwa chini ya uangalizi wa wazazi wao.

Mfuko wa WCF uliahidi kuifanyia kazi changamoto hiyo kwa kuwa kwa sasa watoto wa kuanzio umri huo sio wanufaika wa mfuko.

Kuhusu maboresho ya sheria, washiriki waliishauri WCF kuona namna ya kurahisisha michakato, ikiwemo kuheshimu nyaraka za Mahakama bila kuweka ulazima mkubwa wa cheti cha kifo pale ambapo Mahakama imeshathibitisha vifo hivyo.

Kikao kazi hicho kilifungwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Gladys Barthy, ambaye aliishukuru WCF kwa fursa hiyo ya kujengeana uwezo. Ili kuhakikisha makubaliano hayo yanafanyiwa kazi kwa vitendo, Mahakama imeahidi kuteua mtu maalum (focal person) atakayekuwa kiunganishi cha haraka kati ya Mahakama Kituo Jumuishi Temeke na WCF ili kuharakisha huduma kwa wananchi.

Jaji Mfawidhiwa Mahakama Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa, akifungua mafunzo ya kubadilishana ujuzi katika ukumbi wa Destiny Hall Kibaha Pwani.

Washiriki wa mafunzo hayo wakisikiliza hotuba kutoka kwa Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu Wa WCF, Bw. Abrahamu Siyovelwa.

Majaji Kutoka Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke walioshiriki katika kikao mafunzo wakifuatilia mada zilizokuwa zinawasilishwa.

Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhe. Stephani Kagaruki,  akitoa mada juu ya taratibu za ufunguaji wa mirathi Mahakama za Mwanzo  katika kutoa haki kwa wananchi.

Hakimu Mkazi Mwandamizi, Mhe. Mhangwa Yunge, akitoa ufafanuzi juu ya mada za Usimamizi wa mashauri ya mirathi katika Mahakama ya Wilaya na Mahakama Kuu Temeke.

Meneja Malipo toka WCF, Bi Rehema Kabongo, akitoa mada kuhusu taratibu za fidia kwa wafanyakazi.

Jaji wa Mahakama Kuu Kituo Jumuishi Temeke, Mhe. Gladies Barthy akihitimisha rasmi mafunzo hayo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Singida.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni