Na. ELIUD KIWANGA – Mahakama, Songwe
Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe, hivi
karibuni ilifanya kikao cha kusukuma Mashauri ya Jinai, kikilenga kutathimni na
kuimarisha usimamizi na ufanisi wa utoaji wa haki katika Masjala ya Songwe.
Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Mahakama
ya Hakimu Mkazi Songwe na kuongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata, Naibu Msajili wa Mahakama
Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde na Jaji wa Mahakama Kuu
ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha na kuhudhuriwa na
wadau wa Haki Jinai kutoka Taasisi mbalimbali Mkoa wa Songwe.
Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe
Mhe. Joyce Minde alisoma taarifa ya mwenendo wa Mashauri ya Haki Jinai Masjala ya
Songwe kuanzia tarehe 30, Machi, 2026 mpaka tarehe 26 Juni, 2026 kwa kuainisha
mashauri yote yaliyofunguliwa, mashauri yaliyomalizika na mashauri
yaliyoendelea kusikilizwa.
Mhe. Minde aliaainisha changamoto zinazoathiri
usikilizwa wa mashauri ya jinai na baadae zilipatiwa ufumbuzi. “Tunaomba ushirikiano
wa wenu kwa Mahakama na sisi tunajitahidi kadri tunavyoweza ili kuhakikisha
mashauri aliyosalia yanamalizika kwa wakati,” alisistiza.
Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Malata alisisitiza
kwamba, kikao hicho kinajikita katika mikakati ya kuhakikisha mashauri ya jinai
kwa ngazi ya Mahakama Kuu yanasikilizwa haraka ili kuepuka mlundikano wa Mashauri
huku tukiendelea kuwahimiza wadau kila mmoja wetu kutimiza wajibu wake katika
mnyororo wa haki jinai ili kusaidia Mahakama kutekeleza jukumu lake la msingi
ipasavyo.
Kwa upande wake, Mwakilishi
wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Tawi la Songwe, Bw. Moses Mwampashi amesema, idadi ya Mawakili mkoani
Songwe haitoshi ukilinganisha na uhitaji wa wananchi katika
uwakilishi wa Mawakili mahakamani Songwe, aliendelea kubainisha kuwa uhitaji wa Mawakili ni mkubwa
ukilinganisha na idadi ya mashauri yaliyopo mkoani humo.
Wakili huyo, ameliomba jukwaa la Haki Jinai
Mkoa wa Songwe kusaidia ongezeko la Mawakili ili kutoa huduma ya kisheria na uwakilishi mzuri wa wananchi mahakamani kwa wakati, hatua hiyo itaiwezesha Mahakama
kumaliza mashauri mapema ipasavyo.
Katika kikao hicho, Wadau wa Haki Jinai pamoja Mahakama
Kuu Masjala Ndogo ya Songwe waliazimia kuwa Wafungwa na Mahabusu wafikishwe kwa
wakati, Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea wafike mahakamani saa moja kabla
ya muda ulioandikwa kwenye Summons, kujiridhisha kwa kina juu ya mashahidi wanaofika
kutoa ushahidi mahakamani.
Vilevile, wadau waliazimia kwamba, ikiwa wakili
atashindwa kuendelea kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wake arudishe doc
brief ili wakili mwingine aweze kupangiwa shauri hilo, pia uongozi wa TLS
uwakumbushe mawakili majukumu yao kisheria ikiwemo kuwatembelea mahabusu kabla
ya kuletwa mahakamani, Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea kujiandaa
ipasavyo kabla ya kuingia mahakamani. Vyombo vya haki jinai kuzingatia taratibu
za kisheria zinazosimamia masuala yote ya haki jinai.
Mhe. Malata aliwashukuru wadau wote waliofika katika
kikao hicho na kuwasisitiza kutimiza na kutekeleza maazimio yote
waliyokubaliana kwa kuzingatia sheria za haki jinai zinavyotaka, aliomba
ushirikiano ili kuboresha utoaji wa haki jinai kwa wananchi.
Kikao hicho cha Wadau wa Haki Jinai Songwe kilihudhuriwa na wajumbe kutoka Ofisi ya Mkuu wa
Magereza, Polisi, Ofisi ya Upelelezi Mkoa, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS),
Ustawi wa Jamii, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Ofisi ya Uangalizi Mkoa wa Songwe na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe.
Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu
ya Tanzania Masjala, Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati), Jaji wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha
(kushoto) na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe
Mhe. Joyce Minde (kulia) wakiwa kwenye kikao cha kusukuma mashauri ya jinai.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe.
Stephano Minja akifuatilia kikao hicho.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala
Ndogo ya Songwe Mhe. Gabriel Malata (katikati), Jaji wa Mahakama Kuu ya
Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Abubakar Mrisha (kushoto) na Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Songwe Mhe. Joyce Minde
(kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Wadau wa Mahakama mara baada ya
kuhitimisha kikao cha kusukuma mashauri ya jinai.
Sehemu ya wawakilishi wa baadhi ya Taasisi zilizoalikwa za haki jinai mkoani Songwe.
Kaimu Mtendaji wa Mahakama ya Tanzania Masjala Ndogo
ya Songwe Bw. Mohamed Kimungu Rajabu akifuatilia kikao hicho.
Sehemu ya Wadau wa Mahakama waliohudhuria kikao hicho
akiwemo Bi.Tea Mshana, Bi. Maria Sanga kutoka NPS-Songwe pamoja na Bi. Geladina
Theobard kutoka Ofisi ya Uangalizi-Songwe.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni