Na. CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara
Mahakama
Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara kupitia Mahakama ya Wilaya ya Babati imeendelea
kuwapokea Wanafunzi wa vyuo mbalimbali vya Usimamizi wa Wanyamapori ikiwa ni pamoja
na wanafunzi kutoka Chuo cha Wanyamapori Pasiansi cha jijini Mwanza waliofika
mahakamani hapo kwa ajili ya mafunzo ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu Wanyamapori.
Katika
mafunzo hayo, jumla ya wanafunzi 149 kutoka Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori
Pasiansi kutoka Mwanza wakiwa wameambatana na walimu wao watatu (3) wamefika
kwa lengo la kujifunza taratibu za kisheria na masuala mbalimbali yanayotokea
mahakamani kwa njia ya Mahakama mtandao ili njia hizo iweze kuwasaidia katika
masomo wanayojifunza chuoni.
Akizungumza
wakati wa kufungua mafunzo hayo, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo
ya Manyara, Mhe. Charles Mnzava, aliwasihi wanafunzi hao kuzingatia yale yote
ambayo watafundishwa na wataalamu wa masuala ya kisheria ili yaweze kuwasaidia
katika masomo yao chuoni na hata katika maisha baada ya chuo pale ambapo
watakuwa wameajiriwa au kujiajiri katika maeneo mbalimbali.
“Chuoni
mnasoma zaidi kwa nadharia, nawapongeza kwa kuja leo na kushuhudia namna mashauri
haya yanayohusu wanyamapori na nyara za Serikali yanavyoendeshwa Mahakamani.
Mafunzo haya yataongeza tija na uelewa wenu zaidi katika hayo mnayojifunza
chuoni na hata baadae mtakapokuwa katika ajira zenu.” alisema Mhe. Mnzava.
“Pamoja
na hayo tunawapongeza kwa kuchagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa
ajili ya kupata mafunzo haya. Kwetu Mahakama ni furaha kubwa sana kuweza
kuunganisha Taasisi mbili kama mlivyokuja jana na leo kwa ajili ya mafunzo haya
ya kimahakama na hususan namna ya uendeshaji na usikilizaji wa mashauri
yanayohusu wanyamapori,” ameongeza Mhe. Mnzava
Katika
hatua nyingine, Mhe Mnzava alitumia nafasi hiyo kuwafundisha wanafunzi hao juu
ya Muundo wa Mahakama ya Tanzania ulivyo. “Mahakama zetu hapa nchini, kuanzia
Mahakama ya Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama
Kuu Pamoja na Mahakama ya Rufaa zina taratibu zake za usikilizwaji wa mashauri
kulingana na uzito wa mashauri husika hivyo ni vema mkafahamu kuwa hata haya
mashauri ya Wanyamapori mathalani hayawezi kusikilizwa katika ngazi za Mahakama
za Mwanzo”.
Aidha,
wanafunzi wa Taasisi hizo waliweza kuhoji na kujibiwa maswali mbalimbali kwa
wawezeshaji wa Mafunzo hayo ambao walikuwa ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama
ya Wilaya ya Babati Mhe. Victor Joseph Kimaro pamoja na Mahakimu Wakazi wa Mahakama
ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao na Mhe. Jumaa Mwambago.
Akishukuru
baada ya mafunzo hayo Mwakilishi wa Walimu waliombatana na wanafunzi hao kutoka
Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi Mwalimu Hamisi Philimon Matinde, alishukuru
uongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuwapokea vema na kuwapa
Elimu waliyokuwa wakiihitaj.
“Tunashukuru
sana Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa kutupokea na kwa
ushirikiano mliotupa, tuaamini kuwa elimu hii itatusaidia sana na tutaendelea
kuja hapa kwa ajili ya mafunzo mengine,” alisema Mwalimu Matinde.
Utaratibu
wa kutoa Elimu, unaendelea kufanyika kwa kuwawezesha wanafunzi na wanataaluma
mbalimbali kutoka Taasisi za Elimu kujifunza masuala mbalimbali kama
walivyofanya Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma
ya Wanyamapori Pasiansi Mwanza.
Wanafunzi
wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka wakiwa katika picha ya Pamoja na walimu
wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya jengo la
Mahakama Kuu Manyara.
Mahakimu
Wakazi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe. Martin Massao (aliyesimama kushoto)
na Mhe. Jumaa Mwambago wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yanatolewa kwa Wanafunzi
wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya
Wanyamapori Pasiansi.
Wanafunzi
wa Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi wakiwa katika picha ya Pamoja na
walimu wao na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara mbele ya
jengo la Mahakama Kuu Manyara.
Wanafunzi
wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya
Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa
katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.
Wanafunzi
wa Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya
Wanyamapori Pasiansi, Mwanza wakifuatilia mada ambazo zilikuwa zinatolewa
katika Ukumbi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati.
Naibu
Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava (wa
kwanza kushoto) na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Babati Mhe.
Victo Kimario wakiendelea kutoa Elimu kwa wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa
Wanyamapori, Mweka Pamoja na Taasisi ya Taaluma ya Wanyamapori Pasiansi, Mwanza (hawapo pichani) walipofika Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kupata mafunzo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni