Jumatano, 22 Julai 2026

"USULUHISHI NI NGUZO MUHIMU YA UTOAJI HAKI TANZANIA"

Na HABIBA MBARUKU – Mahakama Dar es Salaam

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amesema kuwa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya usuluhishi na upatanishi, unapaswa kutambuliwa kama sehemu muhimu ya mfumo wa utoaji haki nchini.

Mhe. Siyani ameyasema hayo leo tarehe 22 Julai, 2026, katika hotuba  aliyoisoma kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) ya mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Ameeleza kuwa, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa wahusika wa migogoro kama ilivyofafanuliwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo usuluhishi na upatanishi unapaswa kutazamwa kama mwendelezo wa jukumu la Mahakama katika utoaji wa haki ndani ya mfumo wa utawala wa sheria.

"Utoaji wa haki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umepewa Mahakama. Hata hivyo, mamlaka hiyo haiwazuii wahusika wa mgogoro kutafuta haki kwa njia nyingine walizokubaliana, kama inavyoainishwa katika Ibara ya 107A(2)(d) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambayo inaielekeza Mahakama kukuza na kuimarisha utatuzi wa migogoro miongoni mwa watu wanaohusika katika migogoro hiyo,” amesisitiza Mhe. Siyani.

Amesema mifumo ya jadi ya utatuzi wa migogoro iliyokuwepo kabla ya ukoloni, iliyojengwa katika misingi ya maridhiano na maelewano, bado ina mchango mkubwa katika maendeleo ya mifumo ya kisasa ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya Usuluhishi, huku akisisitiza umuhimu wa kuhakikisha mifumo hiyo inaendana na mazingira ya Tanzania na inayokidhi viwango vya kimataifa.

"Uhalali wa mfumo wowote wa utatuzi wa migogoro hautegemei tu uhalali wake wa kisheria, bali pia kukubalika kwake na jamii pamoja na kuendana kwake na mila na utamaduni wa wananchi. Kwa hiyo, mustakabali wa mifumo ya Usuluhishi/upatanishi nchini Tanzania unapaswa kuwa shirikishi, ukichota mema kutoka katika mila na desturi mbalimbali huku ukizingatia misingi ya haki, kutopendelea upande wowote na utawala wa sheria,” amesema Jaji Kiongozi.

Aidha, ameeleza kuwa, usuluhishi na upatanishi havipaswi kuonekana kama njia zinazotumika pale Mahakama zinapokuwa na mlundikano wa mashauri, bali ni miongoni mwa njia kamili za utoaji haki zilizoidhinishwa na Katiba na Sheria za nchi, zenye uwezo wa kusaidia upatikanaji wa haki mapema ipasavyo.

Amebainisha kuwa, katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kushuhudia ongezeko la uwekezaji katika miundombinu, Sekta ya Nishati, rasilimali asilia na biashara za kimataifa, mifumo ya Usuluhishi na Upatanishi ina nafasi muhimu katika kushughulikia migogoro yenye thamani kubwa na masuala ya kitaalamu kwa ufanisi, kuongeza uhakika wa mazingira ya biashara na kuimarisha imani ya wawekezaji.

Mhe. Siyani ameeleza kuwa, pamoja na uhuru wa mchakato wa usuluhishi, Mahakama inaendelea kuwa na jukumu la kuhakikisha taratibu za usuluhishi zinafuatwa, tuzo za usuluhishi zinatekelezwa, maslahi ya umma yanalindwa na mfumo wa sheria unabaki kuwa thabiti kwa kuwa Mahakama na usuluhishi ni mifumo inayokamilishana katika kufanikisha utoaji haki.

Aidha, amewataka Wadau wa Sekta ya Sheria kuendelea kuimarisha uwezo wa kitaaluma, kutumia teknolojia katika uendeshaji wa mashauri ya usuluhishi, kuendeleza utaalamu katika sekta mbalimbali na kuoanisha mifumo ya ADR na viwango vya kimataifa ili kuiwezesha Tanzania kujijengea nafasi kama kitovu cha usuluhishi kimataifa.

Pamoja na hayo, Jaji Kiongozi amewahimiza washiriki kutumia mkutano huo kujifunza, kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza matumizi ya Utatuzi wa Migogoro kwa Njia Mbadala nchini.

Katika hatua nyingine Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, ametaja hatua mbalimbali zinazofanywa na Ofisi hiyo huku akisisitiza kuwa haki inapaswa kupatikana mapema ipasavyo.

Pamoja na hayo, amewataka kuzingatia R4 za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ambazo ni Maridhiano, Ustahimilivu, Mageuzi na Kujenga Upya.

Kwa upande wake Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) Wakili Aderickson Njunwa, ameeleza kuwa, Taasisi hiyo iliyoanzishwa mwaka 1997, imebeba dhima kubwa ya kuisaidia jamii kutatua migogoro kwa njia ya upatanishi, kadhalika kukuza uwekezaji na kuimarisha uchumi endelevu.

Wakili Njunwa amefafanua kuwa miongoni mwa majukumu mengine ya (TIArb) ni kuhakikisha kuwa jamii ya Tanzania inapata elimu kuhusu maana ya usuluhishi na umuhimu wake kwa maendeleo endelevu pamoja na kuendeleza uwajibikaji kwa kujengeana uwezo na majukumu ya kitaasisi.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akifungua Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju uliofanyika leo tarehe 22 Julai, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Delta jijini Dar es Salaam.

Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026.

Sehemu ya washiriki waliohudhuria katika ufunguzi wa mkutano huo wakifuatilia kinachojiri.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja. Wa pili kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. Hamza Johari, wa pili kushoto ni Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa, wa kwanza kushoto ni Makamu wa Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Usaje Mwambene na wa kwanza kulia ni Meneja wa Uwekezaji wa Taasisi hiyo, Bw. Daudi Riganda.

Rais wa Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb), Wakili Aderickson Njunwa akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni Rasmi, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Nane wa Mwaka wa Taasisi ya Wasuluhishi wa Tanzania (TIArb) na Wiki ya Usuluhishi ya Dar es Salaam (DAR Arbitration Week) mwaka 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya  Delta jijini Dar es Salaam.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.







Meza kuu ikiongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) wakiwa katika picha za pamoja na Wadau mbalimbali walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano huo.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni