Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Mtendaji Mkuu wa
Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda amesema
kwamba Mahakama ni mdau muhimu katika kusimamia masuala ya usalama na afya
mahala pa kazi kwa kuwa Ofisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Mhimili huo katika
kuhamasisha uwepo na uzingatiaji wa sheria, taratibu na kanuni mahala pa kazi.
Bi. Mwenda alieleza
hayo jana tarehe 02 Julai, 2026 akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa
wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi
kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano
wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
“Mafunzo haya si
tu kwamba ni kwa wafanyakazi kwa kuwa ninyi ni wafanyakazi wa ndani ya Mahakama,
lakini vilevile tunatambua kazi yenu kubwa ya kufanya maamuzi. Kwa hiyo
kuifahamu Sheria ya Usalama na Afya, majukumu yake... Tunafahamu mnafahamu ipo,
lakini inavyotekeleza majukumu yake na mafunzo yatakayotolewa hapa basi hata
katika kutoa maamuzi mna inakuwa wepesi, lakini tunategemea sana Mhimili huu wa
Mahakama na Wahe. Majaji ninyi muweze kuwa msaada mkubwa sana kwetu katika
kuhakikisha kwamba maeneo ya kazi yanazingatia sheria,” amesema Mtendaji Mkuu
huyo.
Amesema kuwa,
suala hilo pia inakutokana na kwamba Sheria ya Usalama na Afya imekuwa ni haki
na kanuni ya msingi mahali pa kazi. Kwa hiyo kutozingatia Sheria ya Usalama na
Afya maanake ni kutozingatia haki za binadamu.
Aidha, Mtendaji Mkuu huyo
wa OSHA, amebainisha kuwa, uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya
mahala pa kazi ni sehemu ya haki za msingi za binadamu, kama ilivyopitishwa na
Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2022 kupitia Mikataba Namba 155 na 187.
Ameongeza kwa kusema kuwa, Majaji wana uwezo wa kusaidia kutoa mwongozo wa namna gani ambavyo pia Nchi inaendelea kuwa salama katika uzingatiaji wa haki za binadamu mahali pa kazi.
Kadhalika Bi. Mwenda amemshukuru
Jaji Mkuu kwa kuruhusu mafunzo hayo kufanyikia katika Jengo la Makao Makuu ya
Mahakama ya Tanzania Dodoma. Amewapongeza pia Majaji wapya wa Mahakama ya
Rufani walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Dkt.Samia kwa kuaminiwa na kupewa dhamana hiyo kubwa.
"Sheria ya Usalama
na Afya ya mwaka 2003 inatutaka kulinda nguvu kazi ya Taifa ili kuhakikisha
uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kwa watumishi unaleta tija. Tunataka Majaji
wetu wafanye kazi kwa miaka yote waliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu wakiwa na afya
njema na salama," alisema Kiongozi huyo wa OSHA.
Ameongeza kwamba, kupitia
mafunzo hayo, Majaji hao watapata uelewa wa kina wa jinsi OSHA inavyofanya
kazi, hatua zinazofuatwa kuthibitisha magonjwa yanayotokana na kazi (work-related
diseases), jambo litakalorahisisha utoaji wa maamuzi na utendaji wa haki pale
ambapo mashauri ya namna hiyo yanapofikishwa Mahakamani.
Katika mafunzo hayo ya
siku mbili, Wataalam wa OSHA na Madaktari Bingwa watatoa elimu kuhusu
vihatarishi vya kemikali, biolojia, na vihatarishi vya ki-ergonomia vinavyotokana
na uhusiano wa mfanyakazi na mazingira yake.
Mbali na mafunzo hayo,
OSHA imeweka kambi maalum ya Madaktari Bingwa wa Mifupa, Mgongo na Macho kwa
ajili ya kuwafanyia uchunguzi wa afya na kutoa ushauri wa kitiba kwa Viongozi
na watumishi wa Mahakama, pamoja na kutoa mafunzo ya vitendo ya Uokoaji na
Huduma ya Kwanza.
OSHA imesisitiza utayari
wake wa kuendelea kushirikiana na Mhimili wa Mahakama, ikiwa ni pamoja na
kufanya ukaguzi wa mazingira ya kazi katika majengo mbalimbali ya Mahakama
nchini ili kuhakikisha yanakuwa salama wakati wote.
Wakala wa Usalama na Afya
Mahala pa Kazi (OSHA) ni Taasisi ya Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu
(Kazi, Ajira na Mahusiano) yenye jukumu la kusimamia Sheria Namba 5 ya Mwaka
2003 (Sura namba 297) ili kuzuia ajali, magonjwa na vifo vinavyotokana na
mazingira ya kazi nchini Tanzania.
Mafunzo hayo yalifunguliwa na Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani, Kaimu Jaji Kiongozi, pamoja na Viongozi na Watendaji wakuu wa Mahakama na OSHA.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa OSHA walioshiriki ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.
(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)






Hakuna maoni:
Chapisha Maoni