Ijumaa, 3 Julai 2026

MAHAKAMA MDAU MUHIMU KATIKA KUSIMAMIA USALAMA NA AFYA KAZINI; MTENDAJI MKUU OSHA

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda amesema kwamba Mahakama ni mdau muhimu katika kusimamia masuala ya usalama na afya mahala pa kazi kwa kuwa Ofisi hiyo imekuwa ikishirikiana na Mhimili huo katika kuhamasisha uwepo na uzingatiaji wa sheria, taratibu na kanuni mahala pa kazi.

Bi. Mwenda alieleza hayo jana tarehe 02 Julai, 2026 akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa wakati wa ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Mafunzo haya si tu kwamba ni kwa wafanyakazi kwa kuwa ninyi ni wafanyakazi wa ndani ya Mahakama, lakini vilevile tunatambua kazi yenu kubwa ya kufanya maamuzi. Kwa hiyo kuifahamu Sheria ya Usalama na Afya, majukumu yake... Tunafahamu mnafahamu ipo, lakini inavyotekeleza majukumu yake na mafunzo yatakayotolewa hapa basi hata katika kutoa maamuzi mna inakuwa wepesi, lakini tunategemea sana Mhimili huu wa Mahakama na Wahe. Majaji ninyi muweze kuwa msaada mkubwa sana kwetu katika kuhakikisha kwamba maeneo ya kazi yanazingatia sheria,” amesema Mtendaji Mkuu huyo.

Amesema kuwa, suala hilo pia inakutokana na kwamba Sheria ya Usalama na Afya imekuwa ni haki na kanuni ya msingi mahali pa kazi. Kwa hiyo kutozingatia Sheria ya Usalama na Afya maanake ni kutozingatia haki za binadamu.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo wa OSHA, amebainisha kuwa, uzingatiaji wa masuala ya usalama na afya mahala pa kazi ni sehemu ya haki za msingi za binadamu, kama ilivyopitishwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) mwaka 2022 kupitia Mikataba Namba 155 na 187.

Ameongeza kwa kusema kuwa, Majaji wana uwezo wa kusaidia kutoa mwongozo wa namna gani ambavyo pia Nchi inaendelea kuwa salama katika uzingatiaji wa haki za binadamu mahali pa kazi.

Kadhalika Bi. Mwenda amemshukuru Jaji Mkuu kwa kuruhusu mafunzo hayo kufanyikia katika Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania Dodoma. Amewapongeza pia Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani walioteuliwa hivi karibuni na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt.Samia kwa kuaminiwa na kupewa dhamana hiyo kubwa.

"Sheria ya Usalama na Afya ya mwaka 2003 inatutaka kulinda nguvu kazi ya Taifa ili kuhakikisha uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali kwa watumishi unaleta tija. Tunataka Majaji wetu wafanye kazi kwa miaka yote waliyojaaliwa na Mwenyezi Mungu wakiwa na afya njema na salama," alisema Kiongozi huyo wa OSHA.

Ameongeza kwamba, kupitia mafunzo hayo, Majaji hao watapata uelewa wa kina wa jinsi OSHA inavyofanya kazi, hatua zinazofuatwa kuthibitisha magonjwa yanayotokana na kazi (work-related diseases), jambo litakalorahisisha utoaji wa maamuzi na utendaji wa haki pale ambapo mashauri ya namna hiyo yanapofikishwa Mahakamani.

Katika mafunzo hayo ya siku mbili, Wataalam wa OSHA na Madaktari Bingwa watatoa elimu kuhusu vihatarishi vya kemikali, biolojia, na vihatarishi vya ki-ergonomia vinavyotokana na uhusiano wa mfanyakazi na mazingira yake.

Mbali na mafunzo hayo, OSHA imeweka kambi maalum ya Madaktari Bingwa wa Mifupa, Mgongo na Macho kwa ajili ya kuwafanyia uchunguzi wa afya na kutoa ushauri wa kitiba kwa Viongozi na watumishi wa Mahakama, pamoja na kutoa mafunzo ya vitendo ya Uokoaji na Huduma ya Kwanza.

OSHA imesisitiza utayari wake wa kuendelea kushirikiana na Mhimili wa Mahakama, ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mazingira ya kazi katika majengo mbalimbali ya Mahakama nchini ili kuhakikisha yanakuwa salama wakati wote.

Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) ni Taasisi ya Serikali chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Mahusiano) yenye jukumu la kusimamia Sheria Namba 5 ya Mwaka 2003 (Sura namba 297) ili kuzuia ajali, magonjwa na vifo vinavyotokana na mazingira ya kazi nchini Tanzania.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Mgeni Rasmi, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju, na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani, Kaimu Jaji Kiongozi, pamoja na Viongozi na Watendaji wakuu wa Mahakama na OSHA. 


Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda akitoa neno wakati wa Ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Baadhi ya Viongozi na Watumishi mbalimbali wa Mahakama na OSHA wakiwa katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akimkabidhi zawadi ya Saa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akipokea zawadi ya (First Aid Tool Box) kutoka kwa Bi. Khadija Mwenda, Mtendaji Mkuu wa OSHA wakati wa Hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Watumishi wa OSHA walioshiriki ufunguzi wa Mafunzo ya siku mbili ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi kwa Majaji wapya wa Mahakama ya Rufani yanayofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina na kulia ni Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA), Bi. Khadija Mwenda.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni