- Wampongeza kwa uongozi uliotukuka
- Wamzawadia tuzo, zawadi mbalimbali
- Yeye asema haki kazi haiwezi kujengwa na Mahakama peke yake
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Aliyekuwa Jaji Mfawidhi
wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambina,
ameagwa na Watumishi wa Mahakama hiyo pamoja na Wadau wa Haki Kazi baada ya kuapishwa
kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Hafla ya kumuaga Mhe.
Dkt. Mlyambina ilifanyika usiku wa kuamkia jana tarehe 18 Julai, 2026 katika
ukumbi wa mikutano wa Shirika la Hifadhi ya Jamii (PSSSF) Mwenge jijini Dar es
Salaam na kuhudhuriwa na wageni mbalimbali, akiwemo Majaji wa Mahakama Kuu.
Wengine ni Naibu Katibu
Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Mahusiano), Bi. Zuhura Yunus
Abdallah, Kamishna wa Kazi Bara na Wawakilishi kutoka Wadau mbalimbali wa Haki
Kazi, wakiwemo Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA),
Walikuwepo pia Mfuko wa
Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Mamlaka ya Usalama Kazini (OSHA), Mashirika ya Hifadhi ya Jamii ya PSSF na NSSF, Vyama vya Wafanyakazi, Chama cha Wanasheria Tanganyika
(TLS), Wawakilishi Binafsi na Watumishi wa Mahakama ya Kazi.
Hafla hiyo ilipambwa na
shamra shamra za utoaji Tuzo na Zawadi mbalimbali pamoja na muziki
uliotumbuizwa na bendi na vijana kutoka Mahakama ya Kazi uliobeba ujumbe murua wa
kumtakia heri Mhe. Dkt. Mlyambina kwenye majukumu yake mapya.
Salamu mbalimbali
ziliwasilishwa na washiriki kwenye hafla hiyo, akiwemo Jaji wa Mahakama Kuu
Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Modesta Opiyo pamoja na Naibu Katibu Mkuu kutoka
Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Ajira na Mahusiano.
Katika salamu zake, Mhe.
Dkt. Opiyo, pamoja na mambo mengne, alimwelezea Jaji Mlyambina kama Kiongozi
asiyependa makuu na asiye mbinabinafsi, bali ni mtu anayependa kuwamshirikisha
kila mtu kwenye majukumu mbalimbali ya kiutendaji, hivyo kuwa mfano bora katika
uongozi.
“Tunakushukuru sana kwa
uongozi uliotukuka, ni vigumu sana kukuelezea kutokana na makubwa uliyofanya,
sisi tuliokuwa Mahakama ya Kazi tumejifunza (mengi), umekuwa mama, siyo baba
katika uongozi...
“…Tumejifunza sana kwako
kwa uongozi shirikishi. Hatukujisikia unyonge kuwa pamoja nawe, ulitushirikisha
kwenye mambo mbalimbali. Hatutasahau kamati mbalimbali ulizozianzisha na
kutojilimbikizia majukumu,” alisema.
Jaji Opiyo alimwelezea
pia Mhe. Dkt. Mlyambina kama Kiongozi mfuatiliaji anayependa ndoto aliyonayo
itimie na kile anachokiamini na kupanga kitokee, hivyo ni mtu anayefanikisha
matokeo.
Aidha, Mhe. Dkt. Opiyo
alimwelezea Jaji Mlyambina kama Kiongozi aliyejaa upendo anayetamani kila
mtumishi apate kile kidogo kinachopatikana, kwani anaamini ufanizi kazini
huongezeka pale Mtumishi anapofurahi.
Kwa upande wake, Bi.
Zuhura alimpongeza Jaji Mlyambina kwa uimarisha uhusiano mzuri kati ya Mahakama,
Serikali, Waajiri na Wafanyakazi na kwa kusimamia haki na usawa kwa wafanyakazi
kwa Waajiri kwa weledi wa hali ya juu.
Aliemwelezea kuwa Ofisi
yake haikuwa tu kwa ajili ya kutoa maamuzi ya kisheria bali pia ilikuwa
chamichemi ya ushauri na hekima kwa Wadau wote wa sekta ya haki nchini.
Alieleza kuwa kuteuliwa
kwake na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Jaji wa Mahakama ya
Rufani halikuwa jambo la bahati mbaya, bali ni matokeo ya utendaji uliotukuka,
uadilifu na uwezo wake.
Naibu Katibu Mkuu
alitumia fursa hiyo kumkaribisha Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya
Kazi mpya, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, na kuahidi kuendeleza ushirikiano
uliokuwa wakati akitekeleza majukumu yake.
Akihitimisha hafla hiyo,
Mhe. Dkt. Mlyambina alieleza kuwa Ofisi ya Kamishna wa Kazi imeendelea kuwa
msimamizi muhimu wa utekelezaji wa sheria za kazi, upatanishi wa migogoro na
kukuza mazungumzo ya kijamii, hivyo kusaidia migogoro mingi kutatuliwa kabla
haijafika mahakamani.
Alisema kuwa WCF
imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuhakikisha wafanyakazi wanaopata madhara
wanapata fidia stahiki kwa mujibu wa sheria, jambo linaloimarisha haki na
ustawi wa wafanyakazi na kupunguza migogoro Mahakamani.
Mhe. Dkt. Mlyambina
alieleza pia kuwa OSHA imechangia kwa kiasi kikubwa kujenga utamaduni wa
usalama na afya mahali pa kazi, hivyo kupunguza ajali na magonjwa yatokanayo na
kazi na kuimarisha heshima kwa utu wa mfanyakazi.
Alisema kuwa CMA nayo amekuwa
mdau muhimu wa huduma za upatanishi na usuluhishi wa migogoro ya kikazi, na kwa
kufanya hivyo imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza migogoro inayofika
Mahakama na kuhimiza utatuzi wa migogoro kwa njia za amani.
Kwa mjibu wa Mhe. Dkt.
Mlyambina, PSSF na NSSF zimeendelea kutoa mchango mkubwa katika kuhakikisha
wafanyakazi wanapata hifadhi ya jamii, jambo ambalo si tu linawapa usalama wa
kiuchumi, bali pia linachangia ustawi wa jamii na uthabiti wa mahusiano ya
kazi.
Alielezea pia upande wa
vyama vya wafanyakazi TUCTA, TUGHE, TUICO na vingine ambavyo vimeendelea kuwa
sauti muhimu ya wafanyakazi kwa kutetea haki zao, kukuza mazungumzo ya pamoja
na kuhamasisha uhusiano wa kazi unaozingatia sheria, usawa na heshima.
“Kwa pamoja, kila mmoja
wenu amekuwa mshirika wa karibu wa Mahakama ya Kazi katika kuhakikisha kuwa
mfumo wa haki za kazi unafanya kazi kwa ufanisi,” alisema na kuongeza…
“Ingawa wakati mwingine
tumekutana katika nafasi tofauti kutokana na majukumu yetu ya kisheria,
tumekuwa tukiongozwa na lengo moja kuhakikisha haki inatendeka kwa mujibu wa
sheria, migogoro inatatuliwa kwa haki na kwa wakati, na mazingira ya kazi
nchini yanaendelea kuwa ya amani, tija na yenye kuheshimu utu wa binadamu.”
Jaji Mlyambina
alibainisha pia kuwa katika kipindi chake cha uongozi kama Jaji Mfawidhi, amejifunza
kuwa haki kazi haiwezi kujengwa na Mahakama peke yake, bali inahitaji waajiri
wanaoheshimu sheria na wafanyakazi wanaotekeleza wajibu wao kwa uaminifu.
Alieleza pia kuwa
inahitaji vyama vya wafanyakazi na waajiri vinavyotanguliza mazungumzo ya
kijamii, pamoja na taasisi za Serikali zinazotekeleza majukumu yao kwa weledi.
Mhe. Dkt. Mlyambina alisema
pia kuwa Mahakama imekuwa kiungo muhimu katika kuhakikisha kuwa tofauti
zinapotokea zinatatuliwa kwa haki, kwa mujibu wa sheria na bila upendeleo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni