Jumatatu, 27 Julai 2026

MAHAKIMU SUMBAWANGA WAPIGWA MSASA MATUMIZI YA USHAHIDI WA KIELEKTRONIKI, MAADILI

Na. SHARIFU MOKIWA - Mahakama, Sumbawanga

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga imetoa Mafunzo maalum kwa Mahakimu yaliyolenga kuimarisha uwezo wao katika kushughulikia mashauri yanayohusisha ushahidi wa kielektroniki pamoja na kuwakumbusha kuendelea kuzingatia maadili ya kimahakama katika utekelezaji wa majukumu yao.

Mafunzo hayo yalifunguliwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda na kujumuisha Mahakimu Wakazi 27 kutoka Wilaya za Kalambo, Sumbawanga na Nkasi ili kuwajengea washiriki hao uelewa wa pamoja kuhusu uchukuaji wa ushahidi wa kielektroniki, kanuni zinazosimamia upokeaji na tathmini ya ushahidi huo mahakamani.

Aidha, Mafunzo hayo yalijikita katika kuondoa dosari na makosa ya kawaida yanayoweza kujitokeza wakati wa kushughulikia ushahidi wa kidijiti, pamoja na mbinu bora za kuhakikisha ushahidi huo unatumika kwa usahihi na kwa kuzingatia sheria wakati wote wa uendeshaji mashauri yanayohusu matumizi hayo.

Kupitia Mada mbalimbali, washiriki walijadili changamoto zinazotokana na maendeleo ya teknolojia katika utoaji wa haki na namna Mahakama zinavyoweza kuendana na mabadiliko hayo. Washiriki walisisitizwa umuhimu wa kuendelea kujenga uwezo wa Mahakimu katika masuala ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi katika utoaji wa maamuzi yenye haki na yanayozingatia ushahidi wa kisasa.

Mbali na mada za ushahidi wa kielektroniki, mafunzo hayo pia yaliendeshwa kwa njia ya mkutano mtandao kwenye mada iliyowasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Masjala Ndogo  ya Simiyu Mhe. Wilbert Martin Chuma ambaye alitoa mada kuhusu Utamaduni na Maadili ya Mahakama kwa Mahakimu hao (Judicial Ethics and Culture). Katika wasilisho hilo, alielezea umuhimu wa maadili ya kimahakama katika kujenga na kuimarisha imani ya wananchi/umma kwa Mhimili wa Mahakama.

Aidha, Mhe. Chuma alisisitiza kuwa, maadili ya kimahakama yanapaswa kuonekana si tu katika maamuzi yanayotolewa bali pia katika mwenendo, mawasiliano na utendaji kazi wa kila siku wa Hakimu.

Mhe. Chuma aliongeza kwa kusema kwamba, utamaduni mzuri wa kimahakama hujengwa kupitia weledi, uadilifu na uwajibikaji kwa kuzingatia misingi iyokuwa na upendeleo, kuheshimu sheria na kuendelea kujifunza na kujielimisha mambo mapya ya kisheria yanayojitokeza mara kwa mara ili kuendana na mabadiliko ya mazingira ya utoaji wa haki.

Washiriki walipata nafasi ya kuuliza maswali, kubadilishana uzoefu na kujadili mifano mbalimbali ya vitendo kuhusu matumizi ya ushahidi wa kielektroniki pamoja na masuala ya maadili katika utoaji wa haki. Majadiliano hayo yalichangia kuongeza uelewa na kutoa mbinu za kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika mazingira ya sasa ya kidijitali.

Mafunzo hayo yametumika kama jukwaa la kuimarisha uwezo wa Mahakimu katika matumizi sahihi ya ushahidi wa kielektroniki na kuwakumbusha umuhimu wa kuendelea kuzingatia maadili ya kimahakama kama msingi bora wa utoaji haki wenye ufanisi, uwazi na unaojenga imani kwa wananchi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela  Manyanda (katikati walioketi) akiwa kwenye picha ya pamoja na Washiriki wa mafunzo  ya Ushahidi wa Kielekroniki na Maadili ya kimahakama.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda akizungumza wakati wa kufungua mafunzo maalum kwa Mahakimu yaliyolenga kuimarisha uwezo wao katika kushughulikia mashauri yanayohusisha ushahidi wa kielektroniki.


Viongozi walioshiriki katika Mafunzo hayo, (kushoto) ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda, (katikati) ni Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga Bw. Machumu Essaba na kushoto ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Sumbawanga, Mhe. Pamela Mazengo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Sumbawanga Mhe. Frederick Kapela Manyanda (katikati aliyesimama) akijibu Maswali yaliyo ulizwa na washiriki wa Mafunzo hayo ya Ushahidi wa Kielektroniki.

Waheshimiwa Mahakimu wakiwa katika ukumbi wa Mahakama Kuu Sumbawanga, wakifatilia kwa umakini mafunzo hayo yaliyo kuwa yakitolewa.

Televisheni ikionesha Mkutano mtandao wakati wa mafunzo hayo yaliyokuwa yakiwasilishwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Simiyu Mhe. Wilbert Martin Chuma.




 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni