Jumatatu, 27 Julai 2026

TIMU ZA MAHAKAMA SPORTS KIGOMA, HALMASHAURI YA WILAYA UVINZA ZASAKATA KABUMBU

Na AIDAN ROBERT, Mahakama-Kigoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile, amewaongoza wajumbe wa kikao cha Kamati ya Uongozi ya Mahakama kushuhudia mchezo wa mpira wa miguu wa kirafiki kati ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza.

Mchezo huo uliofanyika hivi karibuni katika Uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu, ulikuwa na lengo la kuimarisha na kudumisha ushirikiano pamoja na mahusiano mema kati ya Mahakama na wadau wake katika Wilaya ya Uvinza mkoani Kigoma.

Katika mchezo huo, kikosi cha Mahakama Sports Kigoma kiliongozwa na Kapteni wake, Bw. Omary Magege.

Akizungumza kabla ya kuanza kwa pambano hilo, Kocha wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma, Bw. Ramadhan Kufakunoga aliwahimiza Wachezaji wake kucheza kwa kujituma na nidhamu ya hali ya juu.

"Wachezaji wenzangu chezeni mpira kwa kujituma maana bidii yenu ndiyo itakayofikia malengo ya kuwa washindi wa mechi hii. Hata hivyo, matokeo yanapatikana baada ya dakika 90, hivyo chezeni bila kusababisha majeruhi kwa timu pinzani kwa kuwa hii ni mechi ya kirafiki," alisema Bw. Kufakunoga.

Kocha huyo aliongeza kuwa, mchezo huo ni sehemu ya kupima uwezo wa timu yake ili kubaini na kurekebisha mapungufu kabla ya kushiriki michuano mingine inayoratibiwa na Viongozi wa Mahakama Sports Kigoma.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi, Mhe. Rwizile alisisitiza umuhimu wa mchezo huo katika kujenga afya na kuimarisha mahusiano ya kiutendaji.

Alisema, "Mechi hii ni ya kuimarisha mahusiano, hivyo chezeni kwa furaha, hii ni sehemu ya kujenga afya zenu na tunategemea burudani nzuri kupitia ushindani wa mechi hii."

Baada ya dakika 90 za mchezo huo, Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 2-0 dhidi ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma.

Licha ya kufungwa, benchi la ufundi la Mahakama Sports lilieleza kuwa matokeo hayo yamekuwa kipimo kizuri cha kubaini maeneo yanayohitaji uboreshaji ili kujenga timu imara zaidi kwa ajili ya mechi zijazo.

Waliohudhuria walipongeza kiwango cha nidhamu, utulivu na weledi kilichooneshwa na timu zote mbili katika kufanikisha malengo ya mchezo huo.

Mchezo huo ulihudhuriwa pia na Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Uvinza, Wajumbe wa Kikao cha Uongozi pamoja na wananchi waliojitokeza kushuhudia.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile akitoa mkono wa salamu kwa vikosi vya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza kabla ya mechi kuanza hivi karibuni.


Kapteni wa Timu ya Mahakama Sports, Bw. Omary Magege akionesha uwezo wa kusakata kabumbu katika mechi ya kirafiki kati ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza iliyofanyika hivi karibuni.

Mchuano mkali ukiendelea baina ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza,  katika uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma (wa kwanza kulia), Mhe. John  Francis Nkwabi pamoja na wajumbe wa Kikao cha Uongozi wa Mahakama Kigoma wakifuatilia mechi iliyokuwa ikiendelea baina ya Timu ya Mahakama Sports Kigoma na  Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza iliyochezwa, katika uwanja wa Shule ya Msingi Rugufu mara baada ya kikao chao kumalizika.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (wa 10 kulia aliyevaa shati jeupe) akiwa katika picha ya pamoja ya Wachezaji wa Timu ya Mahakama Sports Kigoma (kulia)na Timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe. Augustine Karichuba Rwizile (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo ya Kigoma, Mhe.John  Francis Nkwabi (wa kwanza kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mkoa Kigoma, Mhe. Aristida Valerian Tarimo na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya za Kigoma Uvinza, Buhigwe na Kibondo.

 

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)


 



 



 

 



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni