Alhamisi, 16 Julai 2026

WATUMISHI MBEYA WAMUAGA MSTAAFU BW. CHARLES MAPUNDA CHITEKETELA KWA HESHIMA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama Mbeya

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya jana tarehe 15 Julai, 2026 walishiriki katika hafla ya kumuaga aliyekuwa mtumishi Mahakama mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela, ambaye alikuwa akihudumu kama Msaidizi wa Kumbukumbu na Msimamizi wa Kitengo cha mashauri ya Madai, anayestaafu utumishi wa umma baada ya kuitumikia Mahakama kwa weledi, uadilifu na kujituma kwa muda wa miongo kadhaa.

Hafla hiyo ilifanyika katika ukumbi wa Mahakama Kuu Mbeya na kuhudhuriwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, viongozi mbalimbali wa vitengo pamoja na watumishi wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Wilaya Mbeya.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Mpepo alimpongeza Bw. Mapunda kwa utumishi wake uliotukuka na mchango mkubwa alioutoa katika kuimarisha utendaji wa Mahakama. Alieleza kuwa mstaafu huyo amekuwa mfano wa uwajibikaji, uaminifu na uzalendo katika kutekeleza majukumu yake.

“Tunakupongeza sana Bw. Mapunda, umekuwa mtumishi uliyeitumikia Mahakama kwa utumishi uliotukuka. Tunazijua na kuzithamini kazi ulizozifanya na kwa juhudi zako uliendelea kujiendeleza hadi kufika hapo ulipo, kwa hakika uliipenda na kuiheshimu kazi yako Mungu akubariki katika maisha yako mapya,” alisema Mhe. Mpepo.

Kwa upande wake, mstaafu huyo Bw. Chiteketela alitoa shukrani kwa viongozi na watumishi wote aliobahatika kufanya nao kazi kwa kipindi chote cha utumishi wake. Alisema ushirikiano, upendo na mshikamano alioupata kutoka kwa wenzake umechangia mafanikio yake katika kazi.

“Napenda kuwashukuru watumishi wenzangu ambao tumefanya kazi pamoja kwa ushirikiano mkubwa bila kuchoka na bila kubaguana. Nawashukuru pia viongozi wangu kwa kunilea na kuniongoza vyema hadi kufikia hatua hii, Mungu awabariki sana.”

Aidha, Bw. Chiteketela aliwaasa watumishi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, bidii na uaminifu, akisisitiza kuwa mafanikio katika utumishi yanatokana na kuipenda kazi na kutimiza wajibu kwa moyo wa kujituma.

“Ukifanya kazi kwa weledi na kujituma haikupi shida kuifanikisha kazi yako. Nawausia kuipenda kazi yenu na kujituma katika majukumu yote mnayopangiwa na viongozi, kwani huo ndiyo msingi wa mafanikio,” alisisitiza Bw. Chiteketela

Bw. Mapunda aliwahimiza watumishi kudumisha umoja na ushirikiano mahali pa kazi ili kuendelea kujenga mazingira bora ya utendaji na kuimarisha mahusiano ya kikazi.

“Nawasihi muwe na umoja na ushirikiano baina yenu, kwa kuwa kufanya hivyo kutaboresha utendaji kazi na kujenga undugu imara baina yenu.”

Hafla hiyo imeendelea kudhihirisha utamaduni wa Mahakama wa kuthamini na kuenzi mchango wa watumishi wake waliotumikia taasisi kwa uaminifu, uadilifu na kujituma.

Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) akizungumza machache na kutoa neno la shukurani katika hafla hiyo.


Bw. Charles Mapunda Chiteketela (watatu kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na Mahakimu Mbalimbali wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba (watatu kushoto)

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa kitengo cha madai ambacho Bw. Charles Mapunda Chiteketela alikuwa msimamizi wa kitengo hicho

Bw. Charles Mapunda Chiteketela (wapili kulia) akiwa kwenye picha ya Pamoja na maafisa Utumishi/Tawala (wa kwanza kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Watoto Mbeya Bw. Ibrahim Mgallah, (wa pili kushoto) ni Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya Mbeya Bi. Odilia Mapunda, (wa kwanza kulia) ni  Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bi. Sarah Lossi a aliyesimamama nyuma ni Afisa Utumishi Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Mbeya Bw. Alintula Ngalile.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akikabidhi sehemu ya zawadi zilizoandaliwa kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo (kushoto) akimlisha keki kuonesha ishara ya pongezi kwa Mtumishi Mstaafu Bw. Charles Mapunda Chiteketela (kulia) wakati wa hafla hiyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni