Alhamisi, 9 Julai 2026

YAZINGATIENI NA KUYAJALI MAKUNDI YENYE MAHITAJI MAALUM: JAJI MKUU

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama - Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Mawakili wapya wa Kujitegemea kutenda haki huku wakiyazingatia, kuyaheshimu, kuyajali na kuyapa kipaumbele makundi yenye mahitaji maalum wakiwemo Wajane,  Watoto, Wajawazito, Wazee na Watu wenye ulemavu.

Mhe. Masaju ameyasema hayo leo tarehe 09 Julai, 2026 alipokuwa akitoa hotuba yake katika Hafla ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza na Mawakili hao Jaji Mkuu amewasisitiza kuendelea kutekeleza majukumu yao huku wakimtanguliza Mungu kama ambavyo wote wamekiri uwepo wa Mungu kupitia viapo vyao.

Ameeleza kuwa, Mawakili wana mchango mkubwa katika kuisaidia Mahakama kufanya maamuzi yanayozingatia haki kutokana na uhalisia wa matukio bila upendeleo huku wakitenda haki bila kufungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi na kutekeleza jukumu la kusimamia upatikanaji haki kwa ufanisi, jambo litakaloiwezesha Mahakama kuifikia azma ya kutoa haki mapema ipasavyo.

“Moja nikiwakumbusha sisi wenzetu huku mahakamani umuhimu wa kutenda haki bila kufungwa na masharti ya kiufundi kupita kiasi. Sasa sisi mahakamani, Mahakimu na Majaji hatukai peke yetu. Tunasaidiwa na ninyi Mawakili mlioko kwenye utumishi wa umma na Mawakili mnaojitegemea. Ninazungumza na ninyi kuwataka mtusaidie,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, Serikali imetunga sheria inayowawezesha Mawakili kutoa msaada wa kisheria kwa Watanzania wasio na Mawakili na wale wasio na uwezo wa kumudu gharama za Mawakili hivyo ni jukumu la Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) kutekeleza jukumu hilo, huku akiwasihi kutekeleza jukumu hilo kwa ufanisi ipasavyo na si kwa unyonge kwa kuwa dhamira yao ni njema kuwasaidia watu masikini…...” Na mnavyotekeleza hilo jukumu litekelezeni kwa ufanisi ipasavyo na wala sio kwa unyonge. Kwa sababu dhamira yenu ni njema mmejiwekea hiyo ninyi wenyewe.”

Akizungumzia kuhusu uhuru wa Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), kama ilivyoanzishwa na Ibara ya 59B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, hiyo ndio ofisi iliyopewa mamlaka ya kufungua, kuendesha na kusimamia mashauri yote, na kwamba inapokuwa ikitekeleza jukumu hilo ikiongozwa na Mkurugenzi wa Mashtaka, Katiba imeelekeza katika Ibara ya 59B(4) kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka atakuwa huru, hataingiliwa na mtu yeyote au na mamlaka yeyote isipokuwa itazingatia mambo matatu, moja nia ya kutenda haki, kuzuia matumizi mabaya ya taratibu za utoaji haki na maslahi ya umma. Akisisitiza kwa kusema “ishini mambo hayo yote kwa namna ambayo tunataka watu wapate haki.”

Ameongeza kuwa, zipo kanuni zilizotungwa na Mahakama mahsusi kwa ajili ya makundi ya watu maalum katika jamii ambazo zilitangazwa katika gazeti la Serikali namba 110 mwaka 2019 kanuni zinazowahusu watu wa makundi maalum ambao ni Wajane, Watoto, Wajawazito,Wazee na Watu wenye ulemavu ambao wanatambulika kutokana na tamaduni za kijamii, kiuchumi zilizopo katika jamii ambazo sio rafiki na wanabaguliwa au wamekuwa waathirika wa muda mrefu wa ukiukwaji wa haki.

Kadhalika, amewataka kutenda kwa umakini na kuendelea kuwajibika vema na kwamba ikiwa hawatafanya hivyo basi watawajibishwa na Mahakama endapo Mungu atachelewa kuwaadhibu hapa duniani.

Mimi nataka kila mmoja wetu anaposhughulika na mashauri haya awe makini. Sisi hatutamfuata mmoja mmoja huko na kuanza kumchapa viboko lakini tukimjua kwamba anacheza na haki za watu hawa, kama Mwenyezi Mungu atachelewa kumuwajibisha, sisi hapa tutamuwajibisha,” amesema Mhe. Masaju.

Amefafanua kuwa, kanuni zinaeleza wazi kuwa, mashauri yoyote ya Haki Jinai au Haki Madai yanayohusu watu kutoka katika makundi maalum yanapaswa kuhitimishwa ndani ya miezi sita kuanzia tarehe ya kuanza kwa usikilizaji wake isipokuwa kama Mahakama inaweza katika hali ya kipekee kuongeza muda huo kwa kipindi kisichozidi miezi mitatu.

“Jaji au Hakimu anayesikiliza kesi inayohusu mtu kutoka katika kundi maalum atatakiwa kuzipa kipaumbele kesi hizo kuliko kesi nyingine zote katika hatua zote ikiwemo usajili, usikilizaji na utoaji wa maamuzi na ninyi mtawakumbusha wanaozembea kwamba kuna maelekezo ya Mheshimiwa Jaji Mkuu, mzipe kipaumbele kesi hizi,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Ameeleza kuwa, ni wajibu wa Mahakama kuteua Afisa Dawati ili kusimamia kesi za makundi maalum huku akirejelea kitabu cha Zaburi 41: 1-3, inayosisitiza kumkumbuka mnyonge…. Heri amkumbukaye mnyonge; Bwana atamwokoa siku ya taabu, Bwana atamlinda na kumhifadhi hai, naye atafanikiwa katika nchi, wala usimtie katika hali wamtakiayo adui zake…… akaongeza kuwa “msipowahudumia kwa haki wanyonge mnakaribisha laana katika familia zenu kuanzia kizazi cha kwanza hadi cha nne, hatuwezi kufanikiwa katika nchi kama tutakuwa tunawadharau wanyonge.”

Amezitaja kazi za Afisa Dawati kuwa ni pamoja na kutambua kesi na wahusika na kuwasilisha taarifa hizo kwa Jaji au Hakimu aliyepangiwa kesi hiyo, kuwatambua watu wenye uhitaji maalum, kuanzisha na kutunza kanzidata ya kesi zinazohusu makundi maalumu, kutoa elimu na kuwaongoza wafanyakazi wengine kuhusu masuala ya makundi maalumu na kutekeleza majukumu mengine yote kama yatakavyoelekezwa na Jaji au Hakimu Mfawidhi, huku mahakamani hilo litekelezeni kwa ufanisi ipasavyo.

Aidha, amewataka Mawakili kushirikiana na Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama katika utekelezaji wa majukumu yao na yenu huku wakizingatia uadilifu, faraja kwa wanyonge, staha, uaminifu, uwezo wa kumudu majikumu na ushirikiano.

Katika hatua nyingine, ameitaka TLS kulinda na kusimamia sheria na utekelezaji wa kanuni zinazogusa makundi maalum huku wakiwa sauti kwa wasio na sauti, wakitoa mchango wao wa usaidizi wa sheria kwa makundi hayo wakitekeleza majukumu yao kwa uadilifu, akili weledi na busara.

Amewataka Mawakili hao kutimiza wajibu wao wa kuwa mstari wa mbele kuwakumbusha Majaji na Mahakimu katika mashauri ya Haki Jinai na Haki Madai kwa heshima na si kulaumu, pia wajiulize wanatekeleza wajibu gani kama inavyoelekezwa katika kifungu cha 75 cha Sheria ya Mawakili (Sura ya 341 Marejeo ya 2023), hivyo ni vema kwa pamoja kutekeleza ipasavyo sheria na kanuni zilizowekwa.

Pia, amewaasa Mawakili hao kuendelea kuwaenzi wazazi, wenza wao, ndugu, jamaa na marafiki ambao walikuwa pamoja nao kwa kipindi chote hadi walipofika walipo…… amesema, “muwaenzi wazazi wenu na ninyi mliooa na mlioolewa muwaheshimu wenzi wenu kwa kuheshimu mchango wao kwani ni kuenzi utu na heshima kama inavyoelezwa katika amri ya 4 inayosema waheshimu baba yako na mama yako, upate miaka mingi na heri duniani…… nendeni mkatekeleze majukumu yenu kwa haki, usawa na uadilifu Mahakama itaendelea kufuatilia utendaji wenu.”

Ameuhakikishia Umma wa Watanzania kwamba, Mahakama itaendelea jukumu lake la msingi la kutoa haki mapema ipasavyo kwa mujibu wa sheria.

Hii ni sherehe ya 74 ya kuwapokea Mawakili, tangu kuanzishwa kwake mwaka 1986 kupokelewa na kukubaliwa waombaji hao 655 kunafanya idadi ya Mawakili walioandikishwa kufikia 14,875.


Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba yake wakati wa Hafla ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika leo tarehe 09 Julai, 2026 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Baadhi ya Mawakili wapya kati ya 655 waliokubaliwa na Kuwapokewa na Jaji Mkuu leo tarehe 09 Julai, 2026 katika Viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama na Mawakili wapya wakifuatilia yanayojiri katika hafla
ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika leo tarehe 09 Julai, 2026 katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Picha mbalimbali za Mawakili wapya 655 waliokubaliwa na kupokewa leo tarehe 09 Julai, 2026 na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania waliohudhuria Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katiba (aliyesimama kushoto) na Katibu wa Bunge la Tanzania, Bw. Baraka Leonard katika Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) wakiwa katika picha ya pamoja na Wataalam wa Sheria waliohudhuria katika Sherehe ya 74 ya Kuwakubali na Kuwapokea Mawakili wapya 655 iliyofanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa kwanza kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya na wa tatu kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja Mawakili wapya (walioketi nyuma). Wa nne kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Mhe. Jacobs Mwambegele, wa tatu kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Zephrine Galeba, wa tatu kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Abraham Mwampashi, wa pili kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Leila Edith Mgonya, wa nne kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kushoto ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Zainab Katimba na wa kwanza kulia ni Katibu wa Bunge la Tanzania, Bw. Baraka Leonard.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama)



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni