Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Idara
ya Mipango na Uratibu ya Mahakama ya Tanzania inaendesha Mafunzo kuhusu
matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Uratibu wa Vihatarishi kwa watendaji wa
Mahakama Kuu pamoja na Maafisa Vihatarishi kutoka Kanda ya Nyanda za Juu Kusini
ikiwemo Songwe, Iringa, Njombe, Songea, Sumbawanga na Mbeya.
Mafunzo
hayo yaliyoanza tarehe 17 Agosti, 2026 katika Masjala Ndogo ya Mbeya, yanalengo
la kuwajengea uwezo watendaji na Maafisa bajeti wa Mahakama ya Tanzania katika
kubaini, kutathmini na kukabiliana na vihatarishi vinavyoweza kuathiri
utekelezaji wa majukumu na malengo ya Mahakama katika suala zima la utoaji wa
haki kwa wananchi.
Akifungua
mafunzo hayo ya mfumo mpya unaotambulika kama GERMIS (Government Enterprise
Risk Management Information System), Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti,
Uendelezaji na Ubunifu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania,
Bw. Kisingi Salehe Mhando, amesema kuwa, mafunzo yanalenga kuimarisha uelewa na
uwezo wa washiriki katika matumizi ya mfumo mpya wa kielektroniki wa kubaini na
kuratibu vihatarishi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Mahakama katika
kuhakikisha malengo yake yanafikiwa kwa ufanisi.
Bw. Mhando
amesema kwamba, mfumo huo utasaidia Mahakama kubaini vihatarishi kwa wakati,
kuvifanyia tathmini na kuweka mikakati stahiki ya kukabiliana navyo kabla
havijaathiri utekelezaji wa mipango na shughuli za Mahakama.
Aliongeza
kuwa mfumo mpya unaleta maboresho katika namna ya kuratibu vihatarishi
ikilinganishwa na mfumo wa awali, hususan katika kurahisisha mchakato wa
kutambua, kurekodi, kufuatilia na kuchukua hatua dhidi ya vihatarishi
vinavyoweza kujitokeza katika utekelezaji wa shughuli mbalimbali.
Katika
siku ya kwanza ya mafunzo, washiriki wamejifunza kuhusu asili ya vihatarishi,
matokeo hasi na chanya ya vihatarishi, pamoja na tofauti kati ya kihatarishi
(risk) na tatizo (problem). Aidha, wamepata uelewa kuhusu aina na mgawanyo wa
vihatarishi pamoja na misingi ya namna ya kukabiliana navyo kupitia dhana ya
Usimamizi wa Vihatarishi (Risk Management).
Akifafanua
zaidi kuhusu tofauti kati ya kihatarishi na tatizo, Bw. Mhando amesisitiza
umuhimu wa kuchukua hatua mapema ili kuzuia kihatarishi kisifikie hatua ya kuwa
tatizo linalohitaji rasilimali kubwa zaidi katika kulitatua.
“Rasilimali
zinazotumika kutatua kihatarishi ni chache na gharama ndogo ukilinganisha na
rasilimali na gharama zinazotumika kutatua tatizo. Hivyo, tuweke nguvu kubwa
katika kuthibiti vihatarishi kabla haijafikia hatua ya kuwa tatizo,” alisema
Bw. Mhando
Kwa
upande wake, Mtakwimu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu ya Mahakama ya
Tanzania Bw. Mussa Wigute, ameongeza kwa kusema kuwa, usimamizi wa vihatarishi
haukusudii kuondoa vihatarishi vyote, bali ni kuweka mikakati inayowezesha
taasisi kuendelea kufikia malengo yake licha ya uwepo wa vihatarishi.
Mafunzo
hayo yanaendeshwa na timu ya wakufunzi kutoka Idara ya Mipango na Uratibu ya
Mahakama ya Tanzania, inayoongozwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Utafiti,
Uendelezaji na Ubunifu Bw. Kisingi Salehe Mhando, akisaidiwa na Mtakwimu, Bw.
Mussa Wigute, pamoja na Mchumi Bi. Reine Kissae.
Mafunzo
hayo yatawasaidia washiriki kupata ujuzi na maarifa ili kwenda kuwa mabalozi
kwa watumishi wengine wanaoshughulikia vihatarishi kuhusu matumizi ya mfumo huo
mpya wa kielektroniki na namna utakavyotumika katika kuimarisha usimamizi wa
vihatarishi, utekelezaji wa mipango na matumizi bora ya rasilimali za Mahakama.
Mtendaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Iringa, Bi. Melea Mkongwa (wa kwanza kushoto),
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songea Bw. Allan Mwela (Katikati), na
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Njombe, Bw. Richard Mbambe (wa kwanza
kulia) wakiwa katika mafunzo hayo.
Afisa Utumishi kutoka Masjala Ndogo ya Mbeya Bi. Sarah Rossi akichangia jambo kama sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.
Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo.
Mtendaji
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (kulia) na Mtendaji wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Songwe, Bw. Sostenes Mayoka (kushoto)
wakifuatilia kwa karibu mafunzo hayo.
Sehemu ya watendaji wa Mahakama ambao ni washiriki katika mafunzo hayo.
Mchumi kutoka
Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bi. Reine Kissae.
(aliyesimama) akitoa elimu juu ya mfumo mpya wa GERMIS unavyofanya kazi.
Mtakwimu
kutoka Idara ya Mipango na Uratibu Mahakama ya Tanzania, Bw. Mussa Wigute
akitoa ufafanuzi juu ya kukabiliana na vihatarishi katika mafunzo hayo.
Mkurugenzi
Msaidizi wa Utafiti, Uendelezaji na Ubunifu kutoka Idara ya Mipango na Uratibu
Mahakama ya Tanzania, Bw. Kisingi Salehe Mhando akiendesha mafunzo hayo kwa
washiriki (hawapo pichani)
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni