Alhamisi, 13 Agosti 2026

JAJI KIONGOZI AKUTANA NA WAJUMBE BARAZA LA TAASISI YA WASULUHISHI TANZANIA

  • Asema Mahakama ipo tayari kushirikiana ili kuimarisha matumizi ya usuluhishi

Na FAUSTINE KAPAMA na HABIBA MBARUKU-Mahakama, Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, leo tarehe 12 Agosti, 2026, amekutana na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania (TIArb) na kufanya nao mazungumzo yanayolenga kuimarisha ushirikiano na kukuza utatuzi wa migogoro kwa njia ya mbadala (ADR).

Viongozi hao wakiongozwa na Rais wa TIArb, Wakili Msomi Aderickson Njunwa, wamekutana na Jaji Kiongozi kwenye ofisi yake iliyopo Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Wajumbe wengine walioambatana na Rais wa TIArb, ni Wakili Nasra Songoro, Wakili Sultan Rajab, Wakili Marydenisia Katemana na Bi. Mariam Mruma, ambaye ni Katibu wa Baraza hilo.

Akizungumza na Wajumbe hao, Mhe. Dkt. Siyani alieleza kuwa Mahakama ya Tanzania ipo tayari kushirikiana na TIArb kuimarisha matumizi ya usuluhishi au upatanshi, kwani ndiyo mfumo ambao kwa sasa unapewa uzito mkubwa duniani katika utatuzi wa migogoro, iwe ya kibiashara kiuchumi na usalama.

“Mahakama itajitahidi kadri inavyowezekana kuwa karibu na nyinyi, tushirikisheni tukutane katikati pale ambapo mkono wetu na mkono wenu hauwezi kufika. Tumefungua milango, msione shida kugonga pale ambapo mkono wenu unafika, tutawafungulia,” amesema.

Jaji Kiongozi amewaambia Wajumbe hao kuwa Mahakama ya Tanzania ina wataalam wengi, ambao wana ujuzi wa masuala ya usuluhishi, wanaoweza kusaidia pale kunapotokea changamoto kwenye masuala hayo.

Aidha, Mhe. Dkt. Siyani amewaeleza kuwa TIArb inachokifanya ni kitu kikubwa ambacho jamii ya Watanzania bado haijapata elimu ya kutosha, hivyo wanayo kazi kubwa ya kuifanya Taasisi hiyo inafahamika zaidi kwa wananchi ili wanaopaswa kuitumia wasiwe wageni pekee.

“Nchi yetu inakua kiuchumi na uchumi unapokua kunakuwa na migogoro mingi ya kiuchumi. Ufanisi katika eneo la usuluhishi ni jambo ambalo lina faida kubwa kwani njia hii imeonekana kuokoa muda zaidi, tofauti na mchakato wa kimahakama,” amesema.

Jaji Kiongozi ametumia fursa hiyo kuwakumbusha Wajumbe hao kuwa Tanzania imeanza kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambayo eneo kubwa linahusu haki, hivyo kila Taasisi, ikiwemo TIArb ina mchango wa kutoa ili kuwa na jamii inayokusudia kufikia malengo ya Dira hiyo.

Mhe. Dkt. Siyani amebainisha kuwa Mahakama ya Tanzania inapoanda Mpango Mkakati wake, inajaribu kuamsha ndoto hiyo namna gani inaweza kutoa mchango wake katika utekelezaji wa dira hiyo.

“Ninyi kama TIArb hamtaweza kama sheria hazitakuwa haziwapi fursa ya kujielekeza huko, ni wakati muafaka sana wa kuishirikisha ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, mkiwa na mawazo yenu ya nini kitarahisisha kukuza usuluhishi katika nchi yetu. Hili ni jambo muhimu sana na huu ndiyo wakati sahihi zaidi kuliko utekelezaji wa Dira utakapokaposhika kasi,” amesema.

Awali, akizungumza baada ya kukutana na Jaji Kiongozi, Wakili Njunwa alieleza malengo ya kufanya ziara hiyo, ikiwemo kumshukuru kwa kuwafungulia Mkutanao wa nane wa Taasisi hiyo kwa niaba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George M. Masaju, uliofanyika jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Rais wa TIArb alimweleza Jaji Kiongozi kuwa lengo lingine ilikuwa kueleza namna Mkutano huo ulivyofanyika hadi kumalizika kwake, maazimio yaliyofikiwa na kusikiliza ushauri au malelekezo yake kwa Taasisi hiyo.

Aidha, Rais wa TIArb aliomba Mahakama kushirikiana na Taasisi hiyo katika mambo mbalimbali, ikiwemo kupata mwongozo wa namna bora ya utendaji kazi ambao utasaidia kufikia lengo kuu la kuisaidia Serikali katika kuboresha mifumo ya haki.

Rais huyo alifafanua kuwa majukumu ya TIArb, ni usimamizi wa mashauri ya usuluhishi na kujenga uwezo kwa kuandaa vipindi mbalimbali vya mafunzo, yanayolenga kukuza matumizi ya njia mbadala za utatuzi wa migogoro.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, akizungumza na Wajumbe wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania ofisini kwake jijini Dodoma (juu na chini).


Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, akizungumza wakati wa kikao hicho.

Rais wa Baraza la Taasisi ya Wasuluhishi Tanzania, Wakili Msomi Aderickson Njunwa (juu na picha chini katikati), akizungumza wakati wa kikao hicho. 


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa (juu) na Makatibu wa Viongozi (chini) wakichukua kumbukumbu wakati wa kikao hicho.


Kikao kinaendelea.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (wa nne kutoka kulia picha ya juu na wa sita kutoka kulia picha ya chini) akiwa katika picha ya pamoja na Wajumbe wa Baraza la Usuluhishi Tanzania na Viongozi wa Mahakama ya Tanzania baada ya kufanyika kwa kikao hicho.



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni