Na CHRISTOPHER MSAGATI- Mahakama, Manyara
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
ametembelewa na Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya
Tanzania (TUGHE) Bw. Henry Mkunda ofisini kwake jana tarehe 05 Agosti, 2026
mjini Babati.
Akimkaribisha
Katibu Mkuu huyo wa TUGHE, Jaji Mfawidhi Mhe. Dkt. Mambi alimueleza Bw. Mkunda
kuwa, ujio wake ni muhimu sana katika kujadili maslahi mapana ya ushirikiano
miongoni mwa watumishi wa Umma wanaounda Shirikisho hilo la wafanyakazi kutoka
Taasisi mbalimbali.
“Katibu
Mkuu ninakukaribisha sana Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara na tumefurahi
umefika kwa kuwa ujio wako ni chachu ya kuongeza ushirikiano ambao unapaswa
kuwepo miongoni mwetu sisi watumishi wa Umma. Ninaomba pia muendelee kutoa
elimu kwa watumishi kuhusu umuhimu wa kujiunga kwenye vyama vya wafanyakazi,”
alisema Mhe. Dkt. Mambi.
Kwa
upande wake, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha
Kamuzora akitoa salamu alimshukuru Katibu huyo wa TUGHE kwa kufika mahakamani
hapo na kumueleza kuwa, watumishi wa Mahakama wanapaswa kujua majukumu
yanayofanywa na Vyama vya Wafanyakazi hivyo waendelee kufundishwa na
kueleweshwa.
“Pamoja
na jukumu kubwa tulilopewa la kusikiliza na kuamua mashauri, watumishi wetu
wanastahili kupata nafasi ya kueleweshwa majukumu ya Vyama hivi vya wafanyakazi
kwa sababu vyama hivi vinawasaidia sana kujua haki na wajibu wao wanapokuwa
kazini kama watumishi wa umma,” ameongeza Mhe. Kamuzora.
Naye,
Bw. Mkunda, aliushukuru Uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa
ukaribisho aliopewa na kuahidi kuongeza ushirikiano miongoni mwa watumishi wa
Mahakama katika kutekeleza majukumu yake ya kitaasisi kwani Chama kinategemea
wanachama kwa kiasi kukubwa ili kuendesha programu zake.
“Mhe.
Jaji Mfawidhi ninakushukuru sana kwa kunikaribisha ofisini kwako, nami
ninaahidi kuendelea kutoa ushirikiano katika ofisi yako ili kazi zetu
tunazozifanya ziende kwa ufasaha lakini pia ili tuwawezeshe watumishi wote
waweze kujua haki na wajibu wao wa kila siku wanapokuwa katika mazingira ya
kazi,” alisema Bw. Mkunda.
Aidha,
Bw. Mkunda aliipongeza Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara kwa kuweza kumpata
na kuchaguliwa Bw. Shadrack Aron ambaye ni mtumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo
ya Manyara ambaye alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Manyara katika
uchaguzi uliofanyika hivi karibuni.
Katika
ziara hiyo, Mwenyekiti huyo Bw. Mkunda aliambatana na Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa
wa Manyara Bw. Shadrack Aron pamoja na Katibu wa TUGHE Mkoa wa Manyara Bw.
Maulidi Kasimba.
Viongozi
wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara wakiwa kwenye mazungumzo yaliyokuwa yanaendelea
katika ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe.
Dkt. Adam Mambi (kiti cha mbele) wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa
Bw. Henry Mkunda (aliyevalia kofia).
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
akifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea ofisini kwake mara baada ya
kutembelewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda.
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wageni waliomtembelea ofisini kwake
wakati wa ziara ya Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda.
Mwenyekiti wa TUGHE Mkoa wa Manyara Bw. Shadrack Aron akifuatilia mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea mara baada ya kutembelewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda.
Katibu
Mkuu wa TUGHE Taifa Bw. Henry Mkunda akimsikiliza na kufuatilia ujumbe mahususi
wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi
(hayupo pichani) wakati alipomtembelea ofisini kwake.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni