Ijumaa, 7 Agosti 2026

MAZOEZI YA KUJENGA AFYA YA MWILI NA AKILI YASHIKA KASI MBEYA

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Uongozi na Watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya wameendeleza dhamira yao ya dhati ya kujenga afya bora ya mwili na akili kupitia programu ya mazoezi ya pamoja inayofanyika kila Jumanne na Ijumaa ya kila wiki katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala hiyo.

Mazoezi hayo yanawakutanisha viongozi, wadau na watumishi wa kada mbalimbali katika mazingira yanayosaidia kukuza mshikamano, ushirikiano na ustawi wa afya, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utamaduni wa kujali afya mahali pa kazi.

Ushiriki wa Viongozi na Watumishi hao umeendelea kuwa chachu ya kuwahamasisha watumishi wengine kujitokeza kwa wingi katika zoezi hilo, jambo linalosisitiza kwamba, uwepo wa afya njema ni msingi muhimu wa kuongeza ufanisi, tija na ubora wa utoaji huduma za haki kwa wananchi.

Mbali na kuimarisha afya ya mwili, mazoezi hayo yamekuwa yakisaidia kupunguza msongo wa mawazo, kuongeza nguvu ya kiutendaji na kuimarisha mahusiano ya kikazi miongoni mwa watumishi wa Mahakama.

Nayo, timu ya mpira wa miguu ya Mahakama “Mbeya Mahakama sports” inayoundwa na wachezaji kutoka Mahakama zilizopo Mbeya Mjini imeendelea kufanya mazoezi yake katika viwanja mbalimbali huku ikiwa na mwendelezo mzuri wa kupata matokeo uwanjani.

Timu hiyo hivi karibuni imecheza mechi za kirafiki na baadhi ya timu za mpira wa miguu za taasisi na timu za wanachi huku wakiibuka na ushindi kwa mechi tatu mfululizo na kupata sare kwa mechi moja pekee iliyochezwa hivi karibuni na timu ya mpira wa miguu ya watumishi wa Hospitali ya Mkoa wa Mbeya.

Mwamko huo wa kufanya mazoezi kwa watumishi unaendelea kujenga taswira inayotambua kuwa mtumishi mwenye afya bora ni nguzo muhimu katika utoaji wa haki kwa wakati na kwa ubora unaostahili.

Aidha, kupitia utaratibu huo wa mazoezi ya kila wiki, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya inaendelea kuonesha mfano kwamba uwekezaji katika afya ya watumishi ni uwekezaji katika huduma bora kwa wananchi. Vilevile ushiriki wa pamoja kati ya watumishi wa Mahakama na wananchi katika michezo mbalimbali ni chachu ya kuisaidia Mahakama kuongeza imani ya Mahakama kwa wananchi.

Sehemu ya viongozi, wadau na watumishi Mahakama wa Kada mbalimbali wakiwa kwenye mazoezi ya pamoja yaliyowakutanisha kwa ajili ya kujenga afya ya mwili na akili ili kurejesha utimamu wa mwili katika mahala pa kazi, mazoezi hayo yanafanyika katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya. 

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Sehemu ya matukio katika mazoezi mbalimbali yanayoendelea Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya apo.

Timu ya mpira wa miguu ya Mahakama Kuu Mbeya ikiendelea na mazoezi yake katika uwanja cha shule ya msingi Nzovwe Mbeya kujiandaa na mechi zinazoendelea za kirafiki. 

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (kushoto) akiwa katika mazoezi pamoja na sehemu ya watumishi alioshiriki na mazoezi hayo.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (Kushoto) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (kulia) wakiendelea kufanya mazoezi katika viunga vya Mahakama Kuu jijini Mbeya.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (wa kwanza kulia) akizungumza machache wakati wa kufunga mazoezi. (wa kwanza kushoto) ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (wanne kulia)

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiongozwa na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (watano kutoka kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya watumishi wa kada mbalimbali baada ya mazoezi ya pamoja katika viunga vya Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni