Na MWANDISHI WETU-Mahakama ya Kazi, Dar es Salaam
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, jana tarehe 18
Agosti, 2026 alitembelea Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA).
Lengo la ziara hiyo ni kujionea
utendaji, kufahamu kwa undani namna inavyotekeleza majukumu yake na kuimarisha
ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na Tume katika kuhakikisha migogoro ya
kikazi inatatuliwa kwa ufanisi na kwa wakati.
Ziara hiyo imekuwa ya kwanza kwa Mhe.
Dkt. Kilekamajenga katika Tume hiyo
tangu alipoteuliwa kuwa Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, ikiwa ni
sehemu ya jitihada za kuendelea kujenga uelewa na ushirikiano wa kiutendaji
kati ya Taasisi zinazohusika katika mnyororo wa utoaji wa haki kazi nchini.
Jaji Mfawidhi alipokelewa na uongozi
wa Tume na kupata fursa ya kutembelea baadhi ya ofisi, ambapo alijionea
mazingira ya kazi na namna watumishi wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku.
Uongozi wa Tume ulimweleza Jaji Mfawidhi
na wajumbe aliokuwa ameambatana nao kuhusu majukumu mbalimbali ya CMA, muundo
wa utendaji kazi pamoja na nafasi ya Tume katika utatuzi wa migogoro ya kikazi
nchini.
Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ni Taasisi
huru ya utatuzi wa migogoro ya kikazi iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya
Taasisi za Kazi. Miongoni mwa majukumu yake ni kufanya usuluhishi wa migogoro
ya kikazi inayowasilishwa mbele yake na, kwa mujibu wa sheria, kuamua migogoro
kupitia mchakato wa uamuzi.
Akizungumza katika kikao cha pamoja,
Mkurugenzi Mkuu wa CMA, Mhe. Usekelege Mpulla, alimweleza Jaji Mfawidhi kuhusu
matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa Usimamizi wa Mashauri ya Usuluhishi na
Uamuzi unaojulikana kama e-Utatuzi.
Mfumo huo ulianza kutumika rasmi
Januari 21, 2026, ukiwa na lengo la kuboresha usimamizi na uendeshaji wa
mashauri ya migogoro ya kikazi kwa kutumia teknolojia ya kidijitali.
Mfumo huo unamwezesha mdau kusajili
na kufuatilia shauri lake kwa njia ya mtandao, bila kulazimika kufika ofisi za
Tume kwa kila hatua.
Mpaka sasa, zaidi ya mashauri 1,678
yamewasilishwa kwa njia ya mfumo ambapo
mashauri 622 yameisha kwa njia ya usuluhishi na mashauri 277 yameisha kwa njia
ya uamuzi.
Hata hivyo, Kiongozi huyo alieleza
kwamba jitihada za kufanya mfumo huo usomane na mfumo wa usimamizi wa mashauri
unaotumiwa na Mahakama ya Tanzania.
Akielezea umuhimu wa mfumo huo,
Mkurugenzi wa CMA alisema matumizi ya e-Utatuzi yanalenga kuongeza ufanisi
katika utendaji wa Tume, kurahisisha upatikanaji wa huduma na kupunguza gharama
ambazo wadaawa wanaweza kuzitumia katika kufuatilia mashauri yao.
Mfumo huo umesaidia kupunguza
utegemezi wa majalada ya nakala ngumu, kuimarisha usimamizi wa nyaraka za
mashauri na kuongeza uwazi na uwajibikaji katika hatua mbalimbali za mchakato
wa utatuzi wa migogoro.
Aidha, matumizi ya mfumo huo
yanaongeza uwezekano wa huduma za utatuzi wa migogoro kufikiwa kwa urahisi
zaidi na wananchi walioko maeneo mbalimbali nchini.
Mhusika anaweza kusajili na
kufuatilia mwenendo wa shauri lake akiwa mahali alipo, kwa kutumia kifaa chenye
mtandao, jambo linalosaidia kupunguza ulazima wa kusafiri mara kwa mara kwenda
katika ofisi za Tume.
Kwa upande wake, Mhe. Dkt. Kilekamajenga
aliipongeza Tume kwa namna inavyotekeleza majukumu yake katika kusaidia kutatua
migogoro ya kikazi na kwa hatua zinazochukuliwa katika kuboresha huduma kwa
wananchi.
Jaji Mfawidhi alieleza kuwa ziara
hiyo imempa fursa ya kupata uelewa mpana zaidi kuhusu utendaji wa CMA,
changamoto zinazokabili Tume pamoja na hatua mbalimbali zinazochukuliwa katika
kuboresha huduma za usuluhishi na uamuzi.
Vilevile, alisisitiza umuhimu wa
kuendelea kuimarisha ushirikiano kati ya Mahakama ya Kazi na CMA, akieleza kuwa
Taasisi hizo zina nafasi muhimu katika mfumo wa utoaji wa haki za kazi nchini.
Jaji Mfawidhi aliwataka viongozi na
watumishi wa Taasisi hizo kuendelea kushirikiana katika kubaini maeneo
yanayohitaji maboresho, kubadilishana uzoefu na kutafuta njia bora za kuongeza
ufanisi katika utatuzi wa migogoro ya kikazi.
Aidha, aliwasihi viongozi wa CMA
kuendelea kufanya jitihada ili kuhakikisha mifumo hiyo inasomana na kurahisisha
uendeshaji wa mashauri katika utoaji haki kazi.
Ziara hiyo imeonesha umuhimu wa
mawasiliano na ushirikiano wa mara kwa mara kati ya Taasisi zinazohusika katika
utoaji wa haki za kazi. Kwa kuwa CMA na Mahakama ya Kazi zina majukumu
yanayogusana katika mnyororo wa utatuzi wa migogoro ya kikazi, ushirikiano wao
unaweza kusaidia kubaini changamoto za kiutendaji na kutafuta suluhisho kwa pamoja.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni