Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Kamati
ya Utatu inayojumuisha Jeshi la Polisi Tanzania (PT), Ofisi ya Taifa ya
Mashtaka (NPS), Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mamlaka
ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA), imefanya ziara Mahakama
Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kubaini
maeneo yanayohitaji maboresho katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi za haki
jinai.
Kamati
hiyo iliongozwa na Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS)
Bw. Basilius Namkambe ilikutana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo
ya Mbeya ofisini kwake jana tarehe 11 Agust 2026, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji
wa majukumu yake ya kufanya ukaguzi wa utendaji kazi wa vyombo hivyo na
kukutana na wadau wanaoshirikiana navyo katika kutekeleza majukumu ya haki
jinai.
Ziara
hiyo imelenga kupata maoni, kubaini changamoto na kupokea mapendekezo kutoka
kwa wadau wa mfumo wa haki jinai, hatua inayolenga kuongeza ufanisi na
kuboresha namna vyombo hivyo vinavyotekeleza majukumu yao kwa pamoja.
Akizungumza
wakati wa kukutana na Kamati hiyo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo
ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya amesisitiza kuwa ushirikiano wa karibu miongoni mwa
vyombo vya haki jinai ni msingi muhimu katika kulinda haki, usalama na ustawi
wa jamii.
“Vyombo
vyote vya haki jinai vikishirikiana kwa pamoja itasaidia kurahisisha kulinda
usalama na haki kwa jamii. Nashukuru sana kwa ujio wenu na tunaahidi kama
Mahakama tutatoa ushirikiano wa kutosha kila itakapohitajika kufanya hivyo,”
alisema Mhe. Mtulya.
Kwa
upande wake, Naibu Msajili wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya, Mhe. Zawadi
Laizer, amesema kuwa, Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya imeendelea kupata
ushirikiano mzuri kutoka kwa wadau hao katika uendeshaji wa mashauri na
utekelezaji wa majukumu mbalimbali ya kimahakama yanayohitaji ushirikiano wa
vyombo vya haki jinai.
Mhe.
Laizer aliongeza kuwa, ushirikiano huo ni muhimu katika kuhakikisha mnyororo wa
utoaji haki jinai unafanya kazi kwa ufanisi, huku kila chombo kikitekeleza
wajibu wake kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa.
Ziara
ya Kamati ya Utatu Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya ni miongoni mwa hatua
zinazolenga kuimarisha uratibu na mahusiano ya kikazi baina ya Mahakama na
wadau wake, hususan katika masuala yanayohusu utekelezaji wa haki jinai.
Aidha,
ziara hiyo inaendana na utekelezaji wa Nguzo ya Tatu ya Mahakama ya Tanzania,
inayolenga kujenga na kuboresha mahusiano mazuri na wadau pamoja na kuimarisha
imani ya wananchi kwa Mahakama.
Kwa
mantiki hiyo, Mahakama ya Tanzania imeendelea kutambua kuwa ufanisi katika
utoaji wa haki unahitaji ushirikiano wa karibu na endelevu kati ya Mahakama na
wadau wote wa mfumo wa haki, kwa lengo la kuhakikisha haki inatendeka kwa
wakati, kwa usawa mapema ipasavyo na kwa kuzingatia sheria.
Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati
waliosimama mbele) akiwa kwenye picha ya pamoja na Moafisa wa Taasisi
zinazounda Utatu waliomtembelea ofisini kwake, pamoja na sehemu ya Viongozi wa
Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya mara baada ya mazungumzo yanayohusu Taasisi
hizo. Wengine ni (kushoto) Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe.
Zawadi Laizer, (wa pili kushoto) ni Mkurugenzi wa Elimu kwa Umma kutoka Taasisi
ya Kupambana na Kuzuia Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Bw. Joseph Kasongwa
Mwaiswelo, (wa kwanza kulia) ni Naibu Mkuu wa
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mbeya, Bw. Jasper
Luoga na (wa pili kulia) ni Mkurugenzi Msaidizi kutoka Ofisi ya Taifa ya
Mashtaka (NPS) Bw. Basilius Namkambe.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni