Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya
Mahakama
ya Rufani ya Tanzania hivi karibuni imefanya kikao cha tathmini ya utekelezaji
wa shughuli za usikilizaji wa mashauri ya rufaa za madai na jinai katika
Masjala Ndogo ya Mbeya, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuhitimisha rasmi
kikao cha Mahakama hiyo kilichoanza tarehe 3 Agosti, 2026 na kinachotarajiwa
kumalizika tarehe 28 Agosti, 2026.
Kikao
hicho kiliongozwa na Jaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania, Mhe. Dkt. Gerald A.
M. Ndika na kuhudhuriwa na Majaji wa Rufani walioambatana naye katika kikao
hicho ambao ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Dkt. Benhajj Shaban
Masoud na Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph Mlyambina na
Viongozi wengine wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya.
Akiwasilisha
taarifa ya utekelezaji wa kikao hicho, Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala
Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo alisema kuwa, kati ya mashauri 38 yaliyopangwa
kusikilizwa, mashauri 33 sawa na asilimia 87% yameshasikilizwa na kupatiwa
maamuzi.
Aidha,
alieleza kuwa, mashauri 05 ya rufaa za madai yameahirishwa kutokana na sababu
mbalimbali zikiwemo kuwapa warufani nafasi ya kuwafikishia wajibu rufaniwa hati
za mashauri, kumpa nafasi mrufani kumteua wakili mwingine na kutoa nafasi ya
kupatikana kwa mwakilishi wa kisheria wa mjibu rufani aliyefariki, hali
iliyolazimu wahusika kuongezewa muda wa kufanya mabadiliko hayo.
Katika
tathmini hiyo, ilibainika kuwa kumekuwa na changamoto kadhaa ikiwemo wadaawa
kutokuleta taarifa za kuondoa mashauri mapema jambo ambalo lingesaidia kupanga
mashauri mengine, kutokufuata taratibu za uendeshaji wa mwenendo kabidhi
(committal proceedings), washtakiwa wengi wanaotajana kuwakilishwa na wakili
mmoja, na kutokuzingatia kanuni inayotaka mdaawa akifariki ateuliwe msimamizi
wa mirathi ndani ya miezi 12 kwa mujibu wa kanuni ya 105(2) ya kanuni za
mahakama ya Rufani.
Aidha,
pamoja na changamoto hizo, kikao kilieleza kuridhishwa na mafanikio
yaliyopatikana, ikiwemo kusikilizwa kwa mashauri 33 kati ya 38 yaliyopangwa
pamoja na ushirikiano mzuri uliooneshwa na Warufani kwenye rufaa za madai,
Mawakili wa Serikali na wa kujitegemea waliohudhuria kwenye vikao hivyo kwa
wakati.
Mafanikio
hayo yameendelea kuimarisha juhudi za Mahakama ya Rufani ya Tanzania za
kuongeza ufanisi katika usikilizaji wa mashauri na kuhakikisha wananchi
wanapata haki kwa wakati mapema ipasavyo.
Viongozi
wengine walishiriki kikao hicho ni kutoka Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
ambao ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu
Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said Kalunde, Jaji wa
Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo.
Wengine
ni Naibu Msajili Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernard Mpepo, Naibu
Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer, Mahakimu mbalimbali
wakiongozwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya wilaya Mbeya Mhe. Teddy Mlimba,
Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Alintula Ngalile na
wadau wengine wa haki Madai na Jinai Mawakili na wadau wengine wa Haki Jinai na
madai kutoka Mbeya, Songwe na Tabora.
Mwenyekiti
wa Jopo la Majaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe.
Dkt. Gerald A. M. Ndika, (katikati)
akiongoza kikao cha kufanya tathmini ya uendeshaji
wa mashauri ya Madai na Jinai Masjala Ndogo Mbeya, kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Yose Joseph
Mlyambina na kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Benhajj Shaban
Masoud.
Sehemu
ya Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya waliohudhuria kikao cha
tathmini (kulia) ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya
Mhe. Fahamu Mtulya, Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Said
Kalunde (wa pili kulia), Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa
Pomo (wa pili kushoto) na Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe.
Zawadi Laizer (kushoto)
Naibu
Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Bernad Mpepo akiwasilisha
taarifa ya Naibu Msajili ya tathmini kuhusu uendeshaji wa mashauri ya rufaa
Masjala Ndogo Mbeya katika kikao hicho.
Sehemu
ya wadau walioshiriki katika kikao hicho
Sehemu
ya wadau walioshiriki katika kikao hicho.
Mwakilishi
kutoka Gereza Kuu Ruanda Mbeya akitoa neno la shukurani kwa Jopo la Majaji wa
Rufani katika kikao hicho.
(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni