Jumatano, 19 Agosti 2026

WATUMISHI MASJALA NDOGO TABORA WAFANYA ZIARA YA KIKAZI MANYARA

Na CHRISTOPHER MSAGATI - Mahakama, Manyara

Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Manyara iliwaalika watumishi kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo na kubadilishana uzoefu wa majukumu. Ziara hiyo imefanyika kwa siku mbili kuanzia tarehe 17 na 18 Agosti, 2026 ili kuwapa watumishi hao fursa ya kujifunza mambo mbalimbali ya kimahakama.

Aidha, watumishi hao waliofika kutoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga na Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda

Akizungumza wakati wa ziara hiyo ya kikazi, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi aliwapongeza watumishi hao wa Tabora kwa kuichagua Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara kwa ajili ya mafunzo hayo na kuwaeleza kuwa Manyara ni mahali sahihi pa kujifunza.

“Tunawakaribisha Manyara, hapa ni mahala sahihi kwenu pa kujifunza. Tumekuwa tukiwawezesha hata wanafunzi wa vyuo mbalimbali kupata mafunzo yao kwa ajili ya kutimiza vigezo na matakwa yao ya kielimu hivyo nanyi tunawakaribisha ili mjifunze na sisi pia tujifunze kutoka kwenu,” alisema Mhe. Dkt. Mambi.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga aliushukuru uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara kwa mapokezi mazuri ikiwa ni pamoja na kuwapa nafasi ya kujifunza masuala mbalimbali yanayohusu majukumu ya kila siku ya mahakamani.

“Tumesikia mambo mazuri ambayo Wanamanyara mnayafanya hivyo nasi tukaona ni vema tufike tujifunze kutoka kwenu pamoja na kushiriki uzoefu wa Masjala zetu ili tuboreshe utendaji kazi wetu wa kila siku”, alisema Mhe. Ngimilanga.

Pamoja na kushiriki namna wanavyotekeleza majukumu yao ya kila siku, viongozi hao wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweza kujifunza namna ya uandaaji bora wa taarifa mbali mbali za kimashauri pamoja na zile za Kiutawala ambazo huwa zinapaswa kuwasilishwa katika vikao mbalimbali. Katika hatua hiyo, viongozi hao waliweza kushiriki Kikao cha pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara ambacho hufanyika kila wiki kwa ajili ya kupeana taarifa na maelekezo mbalimbali ya kikazi.

Akitoa shukrani kwa uongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda aliwapongeza watumishi wa Manyara pamoja na viongozi wao kwa kufanya kazi kwa bidii na kwa weledi hali ambayo inawezesha mashauri yao kwenda kwa haraka jambo ambalo linapunguza mlundikano wa mashauri.

“Kwa kweli tumeona jitihada zenu Wanamanyara katika usikilizwaji wa mashauri ya kila siku lakini pia katika usimamizi wa rasilimali zenu, tunaahidi kutumia elimu hii tuliyoipata katika kuboresha utendaji kazi wetu tutakaporejea Tabora.

Pamoja na kupata elimu na kubadilishana uzoefu juu ya utendaji kazi, Viongozi wa Mahakama hizo waliweka mikakati ya kuwa Masjala rafiki hata katika masuala ya kijamii na viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora waliweka ahadi ya kuwakaribisha watumishi wa Manyara kwenda Tabora kwa ajili ya kujifunza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyekaa mbele), pamoja na Viongozi wengine wa Mahakama Kuu wakiwa katika mazungumzo ndani ya Ofisi ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara pamoja na wageni waliotoka Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora kwa ajili ya mafunzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (aliyesimama wa nne kutoka upande wa kulia) akiwa katika picha ya pamoja na viongozi na watumishi wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara pamoja na wageni wao waliotoka Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Tabora.

Afisa Tawala wa Mahakama Kuu Manyara, Bw. Christopher Msagati akiwasilisha mada katika mafunzo waliyokuwa wanapatiwa viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Bw. Emmanuel Munda (kushoto), pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga wakifuatilia mafunzo yaliyokuwa yakitolewa katika ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara.

Mtendaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe Bw. Emmanuel Munda (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora. Aidha, katika Runinga wanaoonekana ni washiriki wa kutoka Mahakama za Wilaya na za Mwanzo zilizopo katika Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara wakishiriki kwa njia ya video.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora Mhe. Rhoda Ngimilanga (aliyesimama) akichangia mada wakati wa kikao cha kutoa taarifa kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Dkt. Adam Mambi (kulia) akifuatilia taarifa mbalimbali zilizokuwa zinatolewa katika Kikao kilichoambatana na mafunzo kwa viongozi wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Tabora katika Ukumbi wa wazi wa Mahakama Kuu Manyara. Wengine ni Jaji wa Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Manyara Mhe. Devotha Kamuzora na (kushoto) ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Masjala ndogo ya Manyara Mhe. Charles Mnzava.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Kansha)





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni