Na SOJO MWAKOBA – Mahakama, Mtwara
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Katarina Mteule, ambaye pia ni Mlezi wa
Chama cha Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Tawi la Mtwara, hivi karibuni aliwaongoza
wanachama wao katika ziara ya siku mbili ya utalii iliyofanyika katika Visiwa
vya Kilwa Masoko.
Katika ziara hiyo ya siku
mbili ambayo Mhe. Mteule aliongozana na Mwenyekiti wa TMJA Tawi la Mtwara, Mhe.
Aisha Ndossy, wanachama walitembelea magofu ya mali kale yaliyopo Kilwa
Kisiwani, ikiwemo Msikiti Mkuu wa Malindi na makaburi ya kale (Malindi
Gravestones), kabla ya kufanya utalii wa majini na kuvuka hadi Kisiwa cha Songo
Mnara ambako walitembelea magofu ya Ikulu ya Kale ya Masultani (Sultan’s Palace
Ruins).
Lengo la ziara hiyo
lilikuwa ni utalii, elimu pamoja na kuchangamsha na kuburudisha akili na mwili
baada ya majukumu ya kazi. Wanachama walitembelea na kujionea mabaki ya mali
kale zilizopo visiwani humo, kujua historia ya urithi huo, huku pia wakipata
elimu ya uendeshaji wa mashauri yanayohusu uhifadhi wa wanyamapori kutoka kwa
mwanasheria wa Mamlaka ya Usimamizi wa
Wanyamapori (TAWA).
Akizungumza wakati wa
ziara hiyo, Jaji Mfawidhi aliwapongeza wanachama kwa ushirikiano wao na moyo wa
kupenda kujumuika pamoja katika matukio muhimu kama hayo, huku akisisitiza
umuhimu wa kushirikiana na kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza ipasavyo kauli
mbiu ya Mahakama ya “Uadilifu, Weledi na Uwajibikaji.”
“Niwapongeze wanachama
kwa umoja na ushirikiano wenu wa kupenda kujumuika katika shughuli kama hizi.
Tuendelee kushirikiana na kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza ipasavyo kauli
mbiu ya Mahakama yetu,” alisema Mhe. Mteule.
Miongoni mwa
waliohudhuria ziara hiyo ni Mahakimu, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Mtwara,
Mhe. Seraphine Nsana, wakiwa ni sehemu ya wanachama wa TMJA Tawi la Mtwara,
pamoja na Mtendaji wa Mahakama Mtwara, Bw. Yusuph Msawanga.
Ziara hiyo imeongeza mshikamano miongoni mwa wanachama huku ikiwapa fursa ya kujifunza historia na urithi wa mali kale za Kilwa, historia ya urithi huo, pamoja na umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na wanyamapori.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Mtwara, Mhe. Katarina Mteule (wapili kulia)
akiwasili Kilwa Kisiwani kutembelea magofu ya Malindi.
Mwanasheria kutoka TAW A(kulia)
akiwakaribisha wanachama wa TMJA Mtwara kabla ya kuanza kutembelea magofu ya
Kilwa Kisiwani.
Wanachama wa TMJA Mtwara
wakipata elimu ya historia ya urithi wa Dunia ulioachwa hapo Kilwa Kisiwani.
Mahakimu wakitembelea moja
ya majumba la kale yaliyopo Kilwa Kisiwani.
Wanachama wa TMJA Mtwara
wakiwa kwenye picha ya pamoja kama kumbukumbu ya ziara yao ya utalii visiwani
Kilwa.
Wanachama wa TMJA Mtwara wakiwa kwenye boti
katika utalii wa majini baada ya kutembelea magofu ya Kilwa Kisiwani.
Mahakimu wakisoma mchoro
wa ramani mara baada ya kufika Kisiwa cha Songo Mnara ikiwa ni siku ya pili ya
ziara yao.
Picha ya pamoja ya
wanachama wa TMJA Tawi la Mtwara mbele ya Magofu yanayopatikana Songo Mnara
(Kilwa).
Wanachama wa TMJA Mtwara wakifurahia
mandhari tulivu na upepo wakiwa kwenye kibanda cha kitamaduni.
Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.










Hakuna maoni:
Chapisha Maoni