Jumamosi, 22 Agosti 2026

TUGHE TAWI LA MAHAKAMA KUU DODOMA LAKUTANA

Na ARAPHA RUSHEKE -Mahakama Kuu Dodoma.

Tawi la Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) la Mahakama Kuu Dodoma limefanya mkutano wa wanachama uliojaa furaha, mshikamano na hamasa, ukiambatana na kujadili masuala mbalimbali ya ustawi wa wafanyakazi pamoja na kuwaaga wafanyakazi wastaafu na wanaokaribia kustaafu.

Mkutano huo ulifanyika katika ukumbi wa Mahakama uliopo Kituo Jumuishi cha uUoaji Haki (IJC) tarehe 21 Agosti,2026.

Mkutano huo uliongozwa na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, ambaye ni Jaji Mfawidhi, Mhe. Joachim Tiganga. Mhe. Tiganga aliwapongeza wanachama kushiriki katika mkutano huo na kusisitiza umuhimu wa umoja na mshikamano miongoni mwa wafanyakazi.

Jaji Tiganga alisema kuwa anaamini kikao hicho kitakuwa na manufaa kwa wanachama, akieleza kuwa TUGHE ni chama cha hiari kinacholenga kuwaleta pamoja wafanyakazi na kuwawezesha kushirikiana katika kujenga na kulinda maslahi yao.

Alitoa wito kwa wafanyakazi ambao bado hawajajiunga na TUGHE kujiunga kwa kadri watakavyoweza, akisisitiza kuwa nguvu ya wafanyakazi inatokana na kuwa na umoja na sauti moja.

Aidha, Jaji Mfawidhi alisisitiza ujumbe wa mshikamano unaosisitizwa kupitia wimbo wa TUGHE, akieleza kuwa wafanyakazi wanapaswa kuungana kwani kujitenga kunaweza kudhoofisha uwezo wao wa kusimamia masuala yao kwa pamoja.

Katika mkutano huo pia kulijadiliwa suala la afya ya akili, ambapo mada hiyo iliwasilishwa na Daktari kutoka Hospitali ya Mirembe, kwa lengo la kuongeza uelewa miongoni mwa wafanyakazi kuhusu umuhimu wa afya ya akili katika maisha na mazingira ya kazi.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa furaha na bashasha, ambapo wafanyakazi wastaafu pamoja na wanaokaribia kustaafu walikabidhiwa zawadi kama ishara ya kuthamini mchango wao katika utumishi wa Mahakama.

Shamrashamra ziliendelea kwa kukatwa kwa keki na kusherehekea pamoja, huku zawadi maalumu zikitolewa kwa Jaji Mfawidhi na Mtendaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Bw. Bedson Mariba, hali iliyoongeza furaha na kuufanya mkutano huo kuwa wa kipekee.

Mkutano huo umeendelea kuonesha umuhimu wa umoja, mshikamano na kujali ustawi wa wafanyakazi ndani ya Mahakama Kuu Dodoma.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, wakati akiwasilisha hotuba yake wakati wa kikao hicho.


 

Sehemu ya wajumbe wa Tawi la TUGHE Mahakama Kuu Dodoma wakiimba wimbo wa mshikamano mara baada ya ufunguzi wa kikao.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga akifurahishwa kwa bashasha na zawadi aliyopewa na wajumbe wakati wa kikao hicho.


 

Sehemu ya wajumbe wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma wakifurahia jambo wakati wa kikao hicho.


 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma na Mlezi wa TUGHE Tawi la Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto) pamoja na Mtendaji wa Mahakama Dodoma, Bw. Bedson Mariba wakifurahishwa kwa bashasha na zawadi waliyopewa na wajumbe wakati wa kikao hicho.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni