Ijumaa, 21 Agosti 2026

VIONGOZI WA MAHAKAMA CHINA WATEMBELEA MAHAKAMA KUU DIVISHENI YA KAZI, KISUTU

Na LIGHTNESS KABAJU-Mahakama ya Kazi na WINFRED NZILANO-Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.

Baadhi ya viongozi kutoka Mahakama nchini China jana tarehe 20 Agosti, 2026, waitembelea Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi na katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kujifunza na kubadilishana uzoefu kuhusu uendeshaji wa mashauri ya kazi.

Viongozi hao ni Shan Guojun, ambaye ni mjumbe wa kudumu wa kamati ya uamuzi wa mashauri Mahakama Kuu ya Watu Beijing na Wang Fei, ambaye ni Jaji wa Divisheni ya Kwanza ya Mashauri ya Madai ya Mahakama ya Watu Beijing.

Wengine ni Wu Bowen, ambaye ni Naibu Mkuu wa Divisheni ya Sita ya Madai Mahakama ya Watu Beijing pamoja na Li Guodong, ambaye ni Naibu Jaji Mkuu wa Divisheni ya Kwanza ya Madai ya Changping Beijing.

Wakiwa katika Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, wageni hao walipata maelezo kutoka kwa Naibu Msajili Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi, Mhe. Enock Matembele, ambaye aliwaelezea kwa kina namna uendeshaji na usimamizi wa mashauri ya kazi unavyofanyika, ikiwemo hatua mbalimbali zinazohusika katika mchakato wa utoaji haki.

Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga, aliwashukuru viongozi hao kwa kutenga muda wa kuitembelea Mahakama na kushiriki katika ziara hiyo ya kubadilishana uzoefu.

Aidha, aliwakaribisha tena kutembelea Mahakama hiyo wakati mwingine, akieleza kuwa ushirikiano na kubadilishana uzoefu miongoni mwa Taasisi za Mahakama kutoka nchi mbalimbali ni muhimu katika kuimarisha utoaji wa haki na ufanisi wa huduma za Mahakama.

Viongozi hao wa Mahakama China pia walitembelea Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusiana na mamalaka ya Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya na namna mashauri ya kazi yanayohusiana na jinai na madai.

Ziara hiyo imekuwa sehemu muhimu ya kubadilishana uzoefu na maarifa kati ya mifumo ya utoaji haki ya Tanzania na China, hususan katika eneo la utatuzi wa migogoro ya kazi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akisalimiana na Mhe. Shan Guojun baada ya kuwasili kwenye Mahakama hiyo kwa ziara ya mafunzo na kubadilishana uzoefu kuhusu usikilizaji wa mashauri ya kazi.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Divisheni ya Kazi, Mhe. Enock Matembele, akiwaeleza wageni hao namna Mahakama hiyo inavyoendesha mashauri.

Uongozi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi na Viongozi wengine wa wakiwa katika kikao cha pamoja.

Picha ya pamoja ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga (mbele kushoto) na Viongozi wengine kutoka Mahakama nchini China.

Picha ya pamoja ya Viongozi wa Mahakama nchini China na Mahakama ya Tanzania.

Viongozi wa Mahakama China wakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Viongozi wa Mahakama China wakipitishwa kwenye mada mbalimbali.

Viongozi wa Mahakama China na Vingozi Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja baada ya ziara hiyo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni