Na EVA LESHANGE & AMIRI BAKARI, Mahakama Singida
Jaji
Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Singida, Mhe. Ayoub Mwenda tarehe
29 Agosti, 2026 aliwaongoza watumishi katika zoezi la usafi ikiwa ni jitihada
za kuhakikisha mazingira yanakuwa safi licha ya kuwa na watoa huduma ya usafi
sambamba na kujenga utamaduni wa kutunza mazingira na kujenga mahusiano mazuri
baina ya watumishi na kuimarisha umoja.
Akizungumza
na Watumishi wa Mahakama Kuu Singida aliwaeleza kuwa, zoezi hilo ni endelevu na
litakuwa likifanyika kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi likihusisha hadi Mahakama
za ngazi za chini.
“Watumishi
wenzangu kufanya usafi ni mojawapo ya mazoezi ya viungo lakini pia ni utaratibu
mzuri kwani unaimarisha umoja na mshikamano mahala pa kazi na pia kila mmoja
wetu atakuwa balozi katika masuala ya utunzwaji wa mazingira kama tulivyoona
usafi sio jambo rahisi na zoezi litakuwa endelevu na litahusisha Mahakama ngazi
za chini,” alisema Mhe. Mwenda.
Mahakama
zilizofanya usafi kwa siku hiyo ni pamoja na Mahakama ya Wilaya Singida, Mahakama
ya Wilaya Manyoni, Mahakama ya Mwanzo Itigi, Mahakama ya Mwanzo Mgandu, Mahakama
ya Mwanzo Ikungi, Mahakama ya Mwanzo Ipembe na Mahakama ya Mwanzo Utemini.
Aidha, watumishi wamefurahishwa na zoezi hilo ambalo limeleta tija kwa kuonesha jukumu la usafi ni la wote hivyo, wameahidi kuwa mabalozi wazuri katika utunzaji wa Mazingira.
Mhe. Aggrey Muhigi wa Mahakama
ya Mwanzo Mgandu akifanya usafi.
Watumishi wa Mahakama ya Wilaya Manyoni kwa wakiendelea kufanya usafi kwa pamoja.
Watumishi wa Mahakama ya Mwanzo Utemini Singida wakiendelea na zoezi la kufanya usafi kwa pamoja.
(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)





Hakuna maoni:
Chapisha Maoni