Jumatano, 2 Septemba 2026

MAHAKAMA YA RUFANI YAFANIKIWA KUSIKILIZA ASILIMIA 82 YA MASHAURI ARUSHA

Na SETH KAZIMOTO – Mahakama Arusha

Kikao cha nne cha Mahakama ya Rufani kwa mwaka, 2026 kilichoketi Arusha kuanzia tarehe 03 hadi 28 Agosti, 2026 kimefanikiwa kusikiliza jumla ya mashauri 31 kati ya 38 yaliyopangwa, sawa na asilimia 82 ya mashauri yote.

 Jopo la Majaji wa kikao hicho kiliongozwa na Mhe. Lilian Mashaka huku Majaji wengine wakiwa Mhe. Gerson Mdemu, na Mhe. Imani Aboud.

Akiwasilisha taarifa ya Tathmini ya Kikao hicho cha Mashauri ya Rufani hivi karibuni, Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania alisema kuwa, mashauri 38 yalipangwa kusikilizwa ambapo kati ya hayo, 12 yalikuwa Rufaa za Jinai, 25 Rufaa za Madai, na moja ilikuwa Maombi ya Madai. Idadi ya mashauri yaliyosikilizwa ni 31 na mashauri yaliyoahirishwa ni 7.

Mhe. Mtarania ameongeza kwa kusema kuwa, Mashauri saba yaliyoahirishwa ni kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kukosekana kwa nyaraka muhimu za Baraza la Ardhi, Vifo kwa baadhi ya Wadaawa na Wasimamizi wa Mirathi kutoongezwa shaurini, kukosekana kwa wadaawa katika anuani zilizowekwa kwenye rekodi za rufaa na kutofautiana kwa majina ya wadaawa kwenye nyaraka za Mahakama Kuu.

Naibu Msajili huyo aliyataja mafanikio kadhaa yaliyopatikana katika kikao hicho kuwa ni pamoja na Mashauri yaliyopangwa kusikilizwa na kumalizika kwa asilimia 82, Wadaawa wote waliopata wito walihudhuria mahakamani kwa wakati, hivyo kuwezesha usikilizaji wa mashauri kwa wakati na Maamuzi yaliyosomwa kutolewa kwa wadaawa kwa wakati na kupandishwa katika Maktaba Mtandao ya Mahakama (TanzLII).

Kikao hicho cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani Kanda ya Arusha kilifanyika sanjari na vikao vingine tisa katika Kanda za Mwanza, Shinyanga, Moshi, Bukoba, Dar es Salaam, Iringa, Mbeya, Sumbawanga na Dodoma.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Jopo la Majaji, Mhe. Lillian Mashaka akiongoza Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Aliyeketi kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu na kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Imani Aboud. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Gerson Mdemu (kushoto) akifafanua mambo kadhaa wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akichangia jambo wakati wa Kikao hicho. Aliyeketi upande wa kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Aisha Bade. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi (IJC) Arusha.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Arusha, Mhe. Seif Kulita akichangia jambo wakati wa Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu Arusha, Mhe. Nyigulila Mwaseba. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Flora Mtarania akiwasilisha Taarifa ya Tathmini ya Kikao cha Mashauri ya Mahakama ya Rufani kilichofanyika mkoani Arusha.



Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Tathmini ya Usikilizaji wa Mashauri ya Mahakama ya Rufani mkoani Arusha. Kikao hicho cha tathmini kilifanyika hivi karibuni kwenye ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.


(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Morogoro)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni