Na MWANDISHI WETU-Mahakama, Geita
Tawi la Chama cha
Mahakimu na Majaji Tanzania (TMJA) Geita, tarehe 28 Agosti, 2026 lilipokea
ugeni kutoka Tawi la TMJA Bukoba kwa lengo la kuimarisha ujirani mwema,
mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama katika kutekeleza majukumu yao
ya kimahakama na kijamii.
Ugeni huo uliwasili na
kuongozwa na Mlezi wa Tawi la TMJA Bukoba, Jaji Mfawidhi, Mhe. David Patrick Ngunyale.
Ugeni huo ulipokelewa na Mlezi wa Tawi la TMJA Geita, Jaji Mfawidhi, Mhe. Projestus
Kahyoza.
Katika ziara hiyo, Majaji
na Mahakimu kutoka matawi hayo walishiriki katika shughuli mbalimbali za
kijamii na michezo, zikiwemo matendo ya huruma katika Hospitali ya Wilaya
ya Geita, bonanza la michezo mbalimbali pamoja na chakula cha jioni.
Siku ya pili yake, yaani
tarehe 29 Agosti, 2026 bonanza la michezo lilifanyika katika viwanja vya Geita
Gold Mining Limited (GGML), likihusisha michezo mbalimbali, ikiwemo mpira wa
miguu, mpira wa pete, mbio za yai na kijiko, kufukuza kuku pamoja na mchezo wa karata.
Katika michezo hiyo,
washiriki walionesha ushindani wa hali ya juu, huku wakidumisha mshikamano na
urafiki. Bonanza hilo lililenga kutumia michezo kama fursa ya kujenga urafiki
na mshikamano baina ya wanachama, kuimarisha afya na ustawi wa wanachama,
pamoja na kuimarisha mahusiano ya kikazi na kikanda katika utendaji wa huduma
za umma.
Baada ya kumalizika kwa
shughuli za Bbonanza na kuagana na wageni kutoka Bukoba, tarehe 30 Agosti 2026,
Tawi la TMJA Geita lilifanya Mkutano Mkuu wa Tawi katika Ukumbi wa Mahakama Kuu
Geita.
Mkutano huo ulilenga
kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utendaji wa chama, ustawi wa wanachama
pamoja na namna ya kuimarisha ushirikiano katika utekelezaji wa shughuli za
kimahakama.
Akifungua Mkutano Mkuu
huo, Mhe. Kahyoza alisisitiza umuhimu wa viongozi kuwa mstari wa mbele katika
kuonesha mfano bora wa uongozi, ushirikiano na uwajibikaji.
Mhe. Kahyoza aliwataka
viongozi kutanguliza maslahi ya chama na kuwa mfano katika kutekeleza majukumu
yao, akieleza kuwa uongozi bora ni msingi wa kujenga chama imara chenye uwezo
wa kuwahudumia wanachama wake kwa ufanisi.
Akitoa taarifa ya
shughuli za chama, Katibu wa TMJA Geita, Mhe. Ally Mgomba, alisema kuwa tawi
limeendelea kushiriki katika shughuli mbalimbali za kijamii kwa kushirikiana na
Ofisi ya Mlezi wa Tawi.
Alisema TMJA Geita
imekuwa ikitoa mchango na kuwafariji wanachama wakati wa misiba, kushiriki
katika matukio ya furaha, pamoja na kutekeleza shughuli mbalimbali za kijamii
zenye lengo la kuwasaidia watu wenye mahitaji.
Miongoni mwa shughuli
hizo ni ziara katika Shule yenye Mahitaji Maalumu Bukoba, ziara katika Magereza
ya Wilaya ya Chato, ziara za ujirani mwema kati ya matawi na kanda mbalimbali,
ikiwemo Bukoba na Kigoma, pamoja na ziara ya utalii katika Mgodi wa Geita Gold
Mining Limited (GGML), iliyotanguliwa na shughuli za matendo ya huruma katika
Hospitali ya Wilaya ya Geita.
Katika taarifa yake,
Katibu huyo alieleza kuwa tawi limepata mafanikio mbalimbali, ikiwa ni pamoja
na kuimarika kwa ushirikiano kati ya wanachama na uongozi wa tawi, pamoja na
kuendelea kushirikiana katika kuwasaidia watu wenye changamoto na kushiriki katika
matukio mbalimbali ya furaha ya wanachama.
Aidha, tawi limefanikiwa
kuimarisha mfuko wake, kufanya ziara mbalimbali za kujenga mahusiano na
ushirikiano na kupata tuzo mbalimbali kutokana na shughuli zake.
Pamoja na mafanikio hayo,
Mhe. Mgomba alibainisha kuwa moja ya changamoto zinazolikabili tawi ni ushiriki
mdogo wa wanachama katika mazoezi ya mwili. Alieleza kuwa hali hiyo inaweza
kuathiri ushiriki wa wanachama katika shughuli za michezo na juhudi za kuimarisha
afya na ustawi wao.
Kwa ujumla, ziara ya TMJA
Bukoba pamoja na Mkutano Mkuu wa TMJA Geita imekuwa fursa muhimu ya kuimarisha
ujirani mwema, mshikamano na ushirikiano miongoni mwa wanachama.
Aidha, shughuli hizo
zimetoa nafasi kwa wanachama kubadilishana uzoefu, kujadili mafanikio na
changamoto, pamoja na kuweka mikakati ya kuimarisha chama na ustawi wa
wanachama wake.









Hakuna maoni:
Chapisha Maoni