Ijumaa, 28 Januari 2022

WANANCHI MOROGORO WAFURIKA KWENYE MABANDA KUPATA ELIMU, HUDUMA ZA KISHERIA

 Na Evelina Odemba - Morogoro

Wananchi mkoani Morogoro wamejitokeza kwa wingi katika mabanda mbalimbali yaliyoandaliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, kupata elimu na huduma za kisheria kutoka kwa Majaji, Mahakimu na wadau mbalimbali.

Mabanda hayo yameandaliwa kama sehemu ya Wiki ya Sheria inayoadhimishwa kote nchini. Maadhimisho hayo yanafanyika kitaifa jijini Dodoma. Baadhi ya wananchi waliohudhuria kwenye mabanda hayo wameonyesha kufurahia namna walivyopokelewa na hatimaye kupata huduma za kisheria walizokuwa wakihitaji.

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msendo alikuwa ni miongoni mwa wana Morogoro waliofika katika mabanda hayo kupata ufafanuzi wa masuala kadhaa yanayohusu Mahakama ya Tanzania.

Kwa upande mwingine, maafisa wa Mahakama, wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe wamekuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu ya kisheria kwa wananchi kwa njia mbalimbali.

Mhe. Ngwembe alitembelea katika kituo cha Televisheni cha Abood mjini Morogoro ambapo alizungumzia masuala mbalimbali ya kisheria, huku Jaji mwingine kutoka katika Kanda hiyo, Mhe. Said Kalunde akashiriki kutoa ufafanizi wa mambo ya kisheria kupitia kituo cha Radio cha Abood.

Mahakimu mbalimbali pamoja na wasaidizi wa sheria wa Majaji nao hawakusita kutembelea maeneo kadhaa, ikiwemo katika mashule hapa mjini Morogoro kwa lengo la kutoa elimu ya kisheria kwa wananchi.

Mahakama ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, ilizindua Wiki ya Sheria tarehe 24 Januari, 2022 ambapo Mhe. Ngwembe aliwahakikishia Watanzania kuwa hawatabaki nyuma katika kutekeleza jukumu la utoaji haki na wapo tayari kwenda na mabadiliko yatokanayo na Mapinduzi ya Nne ya Viwanda.

Alisema kuwa Mahakama Mkoani Morogoro haipo nyuma kwenye mabadiliko ya kiteknolojia yanayoendelea hivi sasa ambapo tayari wamefunga televisheni tatika gereza la Mahabusu ambapo mashauri mbalimbali yameanza kusikilizwa kupitia mtandao (video conference).

Aidha Jaji Mfawidhi huyo aliongeza kuwa kwa sasa nakala za hukumu hutolewa siku ya kusomwa kwa hukumu na ili kuhakikisha jambo hilo linafanikiwa Mahakama imenunua Kompyuta Mpakato kwa Waheshimiwa Mahakimu kote nchini kuwarahisishia kuandika hukumu kwa wakati.

Mhe. Ngwembe alitumia fulsa hiyo kuwakaribisha wananchi wote kufika katika vituo vya kutolea elimu ili waweze kujifunza maswala mbalimbali yanayohusu Mahakama pamoja na wadau wake.

Alivitaja vituo hivyo kuwa ni viwanja vya Mahakama Kuu- Kituo Jumuishi( IJC)- Kihonda -Morogoro, viwanja vya shule ya msingi kiwanja cha Ndege, Soko kuu la Kingalu, stendi kuu ya mabasi Msamvu na soko la Chamwino.

Maafisa wa RITA, ambao ni wadau wa Mahakama ya Tanzania wakiwasililiza kwa makini wananchi waliojitokeza kwa wingi kupata huduma za kisheria kwenye mabanda mbalimbali.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Paul Ngwembe akifafanua jambo alipokuwa akitoa elimu ya sheria kwa umma kupitia Televisheni ya Abood  kama sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Sheria yanayoendelea. Kulia ni mtangazaji wa kituo hicho, Bw. Ally Chiholo.



Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Said Kalunde akieleza taratibu mbalimbali za kisheria kwa wananchi kupitia kituo cha Radio Abood.
Katibu wa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Lameck Mwamkoa (mwenye suti) akizungumza na wanafunzi wa Shule ya Msingi Mkwajuni alipowatembelea kutoa elimu katika masuala mbalimbali ya kisheria kama sehemu ya kuadhimisha Wiki ya Sheria.

Sehemu ya wanafunzi katika Shule ya Sekondari Kihonda wakimsikiliza mmoja wa maafisa wa Mahakama (hayupo katika picha) alipowatembelea kutoa elimu mbalimbali za kisheria.

Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, Mhe. Albert Msendo akipata ufafanuzi juu ya shughuli za kimahakama alipotembelea moja ya mabanda hayo.
Wasaidizi wa sheria wa Majaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Morogoro wakiwa katika kituo cha Televisheni cha Imani wakiongozwa na Mwandishi wa Kituo hicho (kulia) kutoa ufafanuzi wa masuala kadhaa ya kisheria.


Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Shida Nganga (katikati) akiwahudumia wananchi waliofika kwenye moja ya mabada yaliyoandaliwa kwa ajili ya kutoa elimu mbalimbali za kisheria.


Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Mhe. Shida Nganga (katikati) akifafanua jambo kwa wananchi (hawapo katika picha) waliofika kwenye moja ya mabanda hayo.




Maoni 3 :

  1. Iwe endelevu kazi nzuri a ana. Inaonesha jinsi wananchi wa mkoa wa Morogoro walivyo na kiu ya kupata huduma za kisheria

    JibuFuta
  2. Pia mahakama itoe nafasi kwa wadau na wananchi kutoa maoni

    JibuFuta
  3. Elimu iwe endelevu kila baada ya muda Fulani ili wananchi waendelendee kufaidika na elimu

    JibuFuta