Alhamisi, 1 Januari 2026

MAOMBI MANNE YA MAHAKAMA TAMISEMI

  • Waziri ayakubali, atoa maelekezo

Na FAUSTINEKAPAMA-Mahakama, Lushoto

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, ameyakubali maombi yaliyowasilishwa na Mahakama ya Tanzania, ikiwemo kusamehe tozo zinazotakiwa kulipwa wakati wa utekelezaji wa miradi ya ujenzi nchini.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, aliwasilisha maombi hayo jana tarehe 31 Desemba, 2025 kwenye hafla ya kukabidhi eneo itakapojengwa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto kwa gharama ya fedha za ndani Shilingi za Kitanzania Bilioni 4.272. Mhe. Prof. Shemdoe alikuwa Mgeni Rasmi kwenye hafla ya makabidhiano hayo iliyofanyika wilayani Lushoto.

Katika maombi hayo, Prof. Ole Gabriel, kwa niaba ya Jaji Mkuu, aliomba Mahakama isitozwe gharama sizizo za kisheria, ikiwemo zinazohusu utawala wa kihalmashauri, pale panapohitajika viwanja vya ujenzi wa majengo ya Mahakama, ama kwa ajili ya huduma za Mahakama au makazi.

Mtendaji Mkuu alimweleza Waziri kuwa huduma zitakazotolewa na Mahakama baada ya kutekeleza miradi ya ujenzi huo itawanufaisha wananchi wa halmashauri husika. ‘Tunakuomba Waziri, kama ikikupendeza, kusamehewa hizi gharama za kiutawala ili kazi nyingine ziweze kuendelea,’ alisema.

Prof. Ole Gabriel alitoa mfano katika Mkoa wa Tanga ambapo gharama za kiutawala kwenye halmashauri ni Shilingi za Kitanzania 250,970,000 kwa mchanganuo kwenye mabano kwa kila Wilaya za Korogwe [12m/=], Lushoto [10m/=] na Muheza kuna viwanja tisa [31,500,000/=].

Kwa upande wa Pangani kuna viwanja nane [14m/=], Tanga [3.9m/=], Handeni kuna viwanja 12 [22.99m/=], Mkinga [13m/=], Kilindi [24m/=] na pia kuna viwanja kwa ajili ya nyumba za Majaji ambavyo vinafanyiwa upembuzi [118m/=].

Ombi lingine linahusu utoaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama na nyumba za makazi kwa Majaji na Mahakimu. Prof. Ole Gabriel ameomba Wakuu wa Mikoa kuendelea kuratibu maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu TAMISEMI kushirikiana na Mahakama ya Tanzania na Wizara ya Fedha kuhakikisha Kata na Wilaya zote nchini zinapata majengo yake.

‘Haya maelekezo aliyatoa tarehe 5 Aprili, 2025 akiwa anazindua jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Naomba nikupe taarifa kwamba kuna pa kuanzia. Wapo Wakuu wa Mikoa watatu, Rukwa, Katavi na Tanga, ambao tayari wameshalibeba kidedea suala hili,’ amesema.

Ombi lingine linahusu Wakuu wa Mikoa kutenga fedha kwa ajili ya kuwezesha kufanyika kwa Kamati za Maadili za Mahakimu. Mtendaji Mkuu alimweleza Waziri kuwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya ni Wenyeviti wa Kamati hizo katika ngazi husika.

Amemuomba Waziri kushajirisha suala hilo ili Wakurugenzi ili watenge bajeti kwa ajili ya kuimarisha Kamati hizo na watambue kuwa zipo kwa mujibu wa Sheria, kwani pale haki inapotendeka, haki pia inatamalaki na ndiyo hasa Dira ya 2050 inavyoelekeza.

Ombi la nne linahusu ujenzi wa barabara itakayowezesha wananchi kufika kwa urahisi kwenye Mahakama hiyo mpya. Mtendaji Mkuu alimuomba Waziri kuwaelekeza TARURA kutengeneza barabara angalau kwa changalawe kwa kuanzia kabla ya kiwango cha lami ili kumwezesha Mkandarasi kuendelea na ujenzi.

Akijibu maombi hayo kwa kuanzia na suala la gharama za utawala, Prof. Shemdoe amemwelekeza Katibu Mkuu wa TAMISEMI kuona namna kama kufutwa kwa tozo hizo hakutavunja sheria. ‘Nadhani milioni 250 siyo fedha nyingi kihivyo, zinaweza kuondolewa na mambo mengine haya ya Mahakama yakaendelea,’ amesema.

Akizungumzia suala la Kamati za Maadili, Mhe. Prof. Shemdoe pia amemwelekeza Katibu Mkuu kutoa mwongozo kwa mamlaka za Serikali za Mitaa ili kutenga bajeti kuwawezesha Wakuu wa Mikoa na Wilaya kusimamia Kamati hizo kwa ajili ya watendaji wa Mahakama.

“Hili ni jambo la msingi ambalo lipo kisheria na lipo kwenye utaratibu wa kazi za Viongozi hawa. Naomba utoke waraka wa kuweza kuwaelekeza Wakurugenzi kutenga bajeti kwenye eneo hili,” amesema.

Kuhusu kuwepo kwa majengo ya Mahakama kwenye kila Kata na Wilaya, Waziri Shemdoe alisema kuwa tarehe 16 Desemba, 2025 alisaini barua kwenda kwa Wakuu wa Mikoa kuhakikisha wanalichukulia zoezi hilo kwa uzito mkubwa.

Alifurahi kusikia kuwa Wakuu wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Tanga wamekuwa mstari wa mbele, hivyo kwa mara nyingine aliwaelekeza Wakuu wa Mikoa 23 iliyobaki kulifanyia kazi jambo hilo na kulichukulia uzito unaostahili.

Kuhusu TARURA, Waziri Shemdoe ameielekeza Taasisi hiyo kuanzia Wilaya ya Lushoto, Mkoa wa Tanga na Makao Makuu kuhakikisha kwenye bajeti inayofuata wanatenga fedha kwa ajili ya barabara ya kwenda kwenye jengo hilo.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi nyaraka na eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akisisitiza jambo wakati wa hafla hiyo. 

Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tanga, Bw. Jumanne Muna akitoa utambulisho wa Viongozi na wageni mbalimbali waliohudhuria hafla ya makabidhiano hayo. Picha chini ni Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Lushoto, Mhe. Rose Ngoka.



Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi mbalimbali [juu na chini] kwenye halfa hiyo.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Viongozi wa dini [juu] na Wadau [chini] kwenye halfa hiyo.


Meza Kuu inayoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Prof. Riziki Shemdoe [katikati waliokaa] ikiwa katika picha ya pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya Lushoto [juu] na watumishi wa Mahakama [chini] kwenye halfa hiyo. Picha ya pili chini ni Wakandarasi wa mradi wa ujenzi huo.




 

Jumatano, 31 Desemba 2025

UJENZI WA MAHAKAMA MPYA YA WILAYA LUSHOTO WAIVA

Na FAUSTINEKAPAMA-Mahakama, Lushoto

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, leo tarehe 31 Desemba, 2025 amekabidhi kwa Mkandarasi Namis Cooperate Limited michoro na eneo itakapojengwa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto kwa gharama ya fedha za ndani Shilingi za Kitanzania Bilioni 4.272.

Makabidhiano hayo yalifuatiwa na utiaji saini wa mkataba wa ujenzi uliofanywa na Prof. Ole Gabriel, kwa upande wa Mahakama, na Bw. James Msumali, kwa niaba ya Mkandarasi.

Hafla hiyo imeshuhudiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, pamoja na Viongozi wengine.

Viongozi wengine waliokuwepo ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batlida Buriani, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Mhe. Zephania Sumaye, Wabunge na wengine kutoka Taasisi mbalimbali, Mahakama ya Tanzania na Wadau.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mtendaji Mkuu amemtaka Mkandalasi kukamilisha mradi huo wa ujenzi ndani ya siku 395 kwa mujibu wa mkataba na kuonya kuwa hapatakuwepo na muda wa nyongeza.

‘Nimeshamwelekeza Mkandarasi kuwa inapofika tarehe 15 Februari, 2027 saa 4 asubuhi, tutakuwa hapa kwa ajili ya kupokea jengo letu zuri, nikuombe Waziri, Mkuu wa Mkoa na Viongozi wengine muwepo siku hiyo…

‘Hatutakuwa na muda wa nyongeza, hatutakuwa na nyogeza ya gharama na hatutakuwa na utani kwenye suala la kazi hii, ni kazi muhimu, wananchi wanasubiri Mahakama hii kwa shauku kubwa,’ amesema.

Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa Mahakama hiyo ni ya kisasa na yenye mfano kwani itakuwa kama maabara inayowawezesha Wanafunzi wanaosoma Sheria katika Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto kufanya mazoezi kwa vitendo.

Kwa upande wake, Mhe. Prof. Shemdoe amemtaka Mkandalasi kununua vifaa vya ujenzi ndani ya Wilaya ya Lushoto, ikiwemo mbao, misumari na vingine, jambo litakalowezesha fedha kuzunguka na kuwanufaisha wananchi wa eneo hilo.

Ameelekeza pia vijana waliopo katika maeneo ya karibu kupatiwa ajira kwenye mradi huo na kusisitiza kazi ya ujenzi kukamilika kwa wakati. Hivyo akamhimiza Mkandarasi kuweka mpango kazi ili kuhakikisha anakabidhi jengo hilo mwezi Februari, 2027.

‘Mimi kama Mbunge wa Jimbo hili, tutakwenda sambamba, nitahakikisha ninafuatilia kwa ukaribu sana. Sina wasiwasi na usimamizi wa jengo hili,’ amesema.

Naye Mkuu wa Mkoa ameeleza kuwa ujenzi wa Mahakama hiyo utasaidia wananchi kupata haki mapema ipasavyo na bila kutumia gharama.

Ametumia fursa hiyo kuwakumbusha wananchi waliojitokeza kushuhudia tukio la makabidhiano hayo kuwa Mahakama ya kwanza Tanganyika ilijengwa Tanga, hivyo ujenzi wa Mahakama hiyo mpya ya Wilaya ni kuendeleza historia katika Mkoa huo.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Lushoto ameihakikishia Mahakama ya Tanzania kuwa uongozi wa Wilaya yake utakuwa bega kwa bega kuhakikisha usalama kuanzia kwenye vifaa vya ujenzi na kutoa ushirikiano wowote watakaouhitaji wakati wa utekelezaji wa mradi huo.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Bi. Victoria Chilewa, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuidhinisha fedha za utekelezaji wa mradi huo.

Amesema kuwa ujenzi wa Mahakama hiyo utasaidia kuimarisha huduma za utawala bora na kusogeza huduma za utoaji haki karibu na wananchi. Amesema kuwa kama halmashauri wataendelea kutoa ushirikiano utakakaohitajika katika sekta zote.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [kulia] akibadilishana na Mkandalasi nyaraka za ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto leo tarehe 31 Desemba, 2025 Lushoto Mkoani Tanga.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel [kulia] pamoja na Bw. James Msumali wakitia saini mkataba wa ujenzi wa Mahakama hiyo. Picha chini wakionesha mkataba huo.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Lushoto, Mhe. Prof. Riziki Shemdoe, akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya mradi wa ujenzi wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akifafanua jambo wakati wa hafla hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe. Balozi Dkt. Batlida Buriani akizungumza kwenye hafla hiyo. Picha chini ni Mkuu wa Wilaya ya Lushoto, Mhe. Zephania Sumaye.


Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, Bi. Victoria Chilewa, akizungumza neno kwenye hafla hiyo. Picha chini ni Mkurugenzi wa Maendeleo na Usimamizi wa Miliki wa Mahakama ya Tanzania, Mhandisi Moses Lwiva akitoa maelezo mafupi ya mradi wa ujenzi wa Mahakama hiyo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel, akiwaonesha Viongozi mbalimbali michoro na mwonekano wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto.. Picha chini Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania akiwaonesha Viongozi sehemu Mahakama hiyo itakapojengwa.



Mwonekano wa sasa wa Mahakama ya Wilaya Lushoto [juu na chini].


Mwonekano wa Mahakama mpya ya Wilaya Lushoto mara ujenzi utakapokamilika tarehe 15 Februari, 2027.


Alhamisi, 25 Desemba 2025

JAJI MKUU AMUAPISHA HAKIMU MKAZI MPYA, MHE. CLARENCE MHOJA

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amefanya uapisho wa Hakimu Mkazi mmoja, Mhe. Clarence Josemary Mhoja na kumsisitiza juu ya uadilifu, utii wa Sheria na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sambamba na kuzingatia maadili ya utumishi wa umma.

Hafla fupi ya uapisho ilifanyika tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. 

Akizungumza mara baada ya uapisho huo, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba alimsisitiza Hakimu Mkazi huyo aliyeapishwa juu ya kumshirikisha Mungu katika kila jambo, kuwa muadilifu katika utendaji.

Kadhalika Mhe. Kagomba ameongeza kwa kumsisitiza Mhe. Mhoja kufanya kazi kwa weledi, kudumisha ushirikiano wakati wa kazi, kujiendeleza kielimu, kuwa mzalendo, pamoja na kuhakikisha kuwa taarifa za kiofisi hazitoki nje ya ofisi bila maelekezo maalum.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimuapisha Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Anayeshuhudia katikati ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya.

Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja akila kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha). Hafla ya uapisho ilifanyika tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akisaini hati ya kiapo mara baada ya kumuapisha Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja (hayupo katika picha) tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania -Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba akizungumza jambo mara baada ya uapisho wa Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja (hayupo katika picha) tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja aliyemuapisha tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Hakimu Mkazi mpya, Mhe. Clarence Mhoja (kulia). Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba mara baada ya uapisho uliofanyika tarehe 24 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Picha na JEREMIA LUBANGO, Mahakama-Dodoma)

 

 

 

 

 

Jumatatu, 22 Desemba 2025

TIMIZENI WAJIBU WENU IPASAVYO, NINYI NDIO INJINI YA MAHAKAMA-JAJI MKUU

  • Awataka Wasajili & Naibu Wasajili wa Mahakama kufanya kazi kwa kujituma bila maelekezo ya Viongozi
  • Atoa rai kwa Majaji/Mahakimu kuyapa kipaumbele mashauri ya mirathi, ardhi……
  • Awakumbusha Wasajili hao kuwa waadilifu hata baada ya kuteuliwa kuwa Majaji 
  • Asema ili kuendelea kuhudumia wananchi, Mahakama imeamua kufanya ugatuzi wa madaraka ya Mahakama ya Rufani kwenye Kanda

Na MARY GWERA & HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Wasajili na Naibu Wasajili wa Mahakama nchini kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kuwa wao ndio injini ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama.

Akizungumza wakati wa kikao kati yake na Wasajili na Naibu Wasajili wa Mahakama kilichofanyika leo tarehe 22 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu jijini Dodoma na kwa njia ya Mkutano Mtandao (Video Conference), Mhe. Masaju amesema kuwa, ni muhimu kwa Wasajili hao kujituma na kuwa wabunifu badala ya kutekeleza majukumu kwa kutegemea maelekezo ya Viongozi pekee.

“Ninyi ndio injini ya shughuli za Mahakama, ndio mashine za utendaji wa shughuli za Mahakama, tunataka hata tunapofanya ugatuzi wa madaraka ya Mahakama ya Rufani kwenye Kanda tuendeleze jitihada za kuhakikisha haki inatolewa mapema ipasavyo,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju  amewataka Wasajili wa Mahakama nchini kuimarisha utendaji kazi, kuzingatia maadili ya kazi na kusimamia kikamilifu mashauri ili kuhakikisha haki inatolewa mapema ipasavyo na kwa mujibu wa sheria, licha ya kuwepo kwa changamoto katika uendeshaji wa mashauri, hususani ucheleweshaji wa mashauri unaosababisha wananchi kunyimwa haki zao za msingi.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu ameeleza kuwa, rufaa zisizo na msingi ni miongoni mwa sababu zinazochangia msongamano wa mashauri mahakamani, huku akiwataka Wasajili kutumia mamlaka yao kikamilifu katika kusimamia hatua za awali za mashauri.

Sambamba na hayo, amewaelekeza kuyapa kipaumbele mashauri ya mirathi pamoja na mashauri ya ardhi na mashauri yote kwa ujumla ili yakamilike mapema na shughuli nyingine za maisha ziweze kuendelea.

“Tuyape kipaumbele mashauri ya mirathi, hayana sababu ya kukaa kwa muda mrefu, tusishabikie vitu vinavyoweza kuweka majonzi kwenye familia, hivyo tuyamalize mashauri hayo mapema ipasavyo,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Masaju amesema kuwa, yeye hatampima Jaji au Hakimu kulingana na idadi/viwango vya uondoshaji wa mashauri vilivyowekwa, bali anavutiwa zaidi na ufanisi katika kazi.

"Ninatambua tulikuwa na sababu za msingi kwa nini tuliweka kanuni ya 'backlog', kwamba kesi itachukuliwa kwamba hii imechelewa kusikilizwa kama kwa mfano Mahakama ya Rufaa itakuwa tangu miaka miwili haijaikilizwa, Mahakama Kuu miaka miwili, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya mwaka mmoja, Mahakama ya Mwanzo miezi sita, huo ulikuwa utaratibu mzuri uliokusudia kushughulika na hii changamoto tuliyokuwa nayo ya wingi wa mashauri wakati ambapo tulikuwa na miundombinu ya Mahakama, unakuta Mahakama moja ya Wilaya inahudumia na Wilaya nyingine mbili, Mahakimu hawapo, rasilimali fedha hakuna lakini sasa tumetoka huko Mahakimuw apo hizo rtasilimali za kusikiliza mashauri zipo," ameeleza.

Ameongeza kwamba,  Mahakama zipo kwa hiyo haiwezi kuendeleza utaratibu huo, huku akihoji kwanini mashauri ya Mahakama za Mwanzo yachelewe? Na kwamba kwa upande wa Mahakama za Wilaya kuna mwongozo wa mashauri ya jinai tangu mwaka 2020 kwamba, shauri linapopokelewa mahakamani linaanza kusikilizwa siku hiyohiyo, watu wakikamatwa na Polisi mwongozo uliopo ni kwamba wanatakiwa kwenda na mashahidi, kila mmoja anaenda na mashahidi wake, hivyo hakuna sababu ya kuchelewesha shauri kwa kigezo cha kusubiri miezi sita na muda uliowekwa na ngazi nyingine za Mahakama.

"Sasa kama ni hivi, hizi Mahakama za Mwanzo kwa nini tuchelewe, kwa nini kesi za jinai zichelewe mpaka miezi sita, hiyo miezi sita kesi haijaisha tu kuna baadhi ambao hata hawana mashahidi wengi, kwa hiyo ni uzembe, tunatakiwa kuwahudumia wananchi wa Tanzania katika ukweli na haki," amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewakumbusha Wasajili kusimamia nidhamu ya kazi kwa watumishi wa Mahakama, akisisitiza kuwa vitendo vya uzembe, kutowajibika na ukiukwaji wa maadili haviwezi kuvumiliwa kwa kuwa vinadhoofisha taswira ya Mahakama kwa jamii.

“Sisi kama Viongozi tuna wajibu wa kushirikiana pamoja na watumishi wote wa Mahakama kubuni mikakati na kuchukua hatua za kukabiliana na changamoto zilizopo ili kuzitatua na kusonga mbele,” amesema Jaji Mkuu.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amewataka Wasajili kujishughulisha na shughuli halali katika kujipatia kipato, huku akisisitiza kuwa kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi halali afanye kazi huku akitimiza wajibu wake, akirejea Ibara ya 9 (e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) ambayo inasema ‘kwamba kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi anafanya kazi, na kazi maana yake ni shughuli yoyote ya halali inayompatia mtu riziki yake.’

Akizungumzia kuhusu changamoto mbalimbali zilizokuwa zikiikabili Mahakama, ambazo ni pamoja na changamoto ya miundombinu ya majengo, changamoto ya rasilimali watu na rasilimali fedha na changamoto za kimaadili, Jaji Mkuu amesema kwamba, Serikali imechukua hatua madhubuti katika kutatua changamoto hizo, ikiwa ni pamoja na kuendeleza ujenzi wa Mahakama katika Mikoa na Wilaya ambazo hazikuwa na Mahakama.

Ameongeza kuwa, kuna ya ujenzi wa Majengo mapya ya Mahakama Kuu- Masjala mpya za Simiyu, Katavi, Lindi, Njombe, Singida, Songwe na kwamba Masjala hizo zinatarajia kuanza kazi tarehe 02 Februari, 2026 huku ujenzi wa ukiendelea katika Mikoa ya Songea na Geita na inatarajiwa kukamilika tarehe 01 Februari 2026.

“Serikali imechukua hatua madhubuti kutatutua tatizo la miundombinu ya Mahakama, wakati huu katika Mahakama ya Tanzania hasa Tanzania bara Mahakama za wilaya ziko katika kila wilaya isipokuwa wilaya tatu ya Chamwino mkoani Dodoma, Ikungi na Mkalama za Mkoani Singida na Serikali iko katika mpango wa kujenga Mahakama katika kila Kata,” Amesema Mhe. Masaju.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewaeleza Wasajili hao kuhusu Sera ya Mahakama ya kuwa na Mahakama ya Mwanzo kila Kata maana yake zitajenga Mahakama za Mwanzo, ambapo ametoa rai kwao kuwa sehemu ya utafutaji wa maeneo/viwanja vizuri kwa ajili ya matumizi ya Mahakama sambamba na makazi ya Majaji/Mahakimu. 

Mhe. Masaju amesema katika hilo, TAMISEMI imetakiwa kutenga ekari 2 kwa kila Kata kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama mpya za Mwanzo ambazo zitasaidia upatikanaji wa haki karibu kwa wananchi, kuongeza ajira kwa wananchi katika kada mbalimbali na kuleta ustawi wa jamii ambao unasisitizwa pia katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara 146(2)(b) isemayo Utawala bora, Usalama na Ustawi wa jamii.

Aidha, katika kuhakikisha kuwa Haki inatolewa kwa wote mapema ipasavyo, Jaji Mkuu amewataka Wasajili/Naibu Wasajili wanapoandaa ratiba za mashauri (causelists) kuhakikisha kuwa, mashauri yote yaliyoiva kwa usikilizwaji yanasikilizwa.

"Sambamba na hili  nitawataka ninyi Wasajili mnaopopanga 'cause lists' zile kwa ajili ya Majaji iwe katika ngazi zote za Mahakama na hasa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani muhakikishe kwamba mashauri yote ambayo yameshaiva kusikilizwa kadri yalivyosajiliwa mahakamani yanapaswa kusikilizwa msiyaruke mkiyaruka ndio mnaleta hii dhana ya Mahakama kufanywa kuwa Sehemu ya kuegesha majalada," amesisitiza Mhe. Masaju. 

Kadhalika, amewataka Wasajili hao kuwa na Ushirikiano na Uwajibikaji kwa kuwa ushirikiano ni nguzo ya mafanikio. Na vilevile kuondoa matabaka ya vyeo kwa kujenga usawa, heshima na mshikamano kazini. Mhe. Masaju ameongeza kwa kutoa rai kwa Wasajili hao kuwa na Ubunifu na kubadili mitazamo na fikra kwakuwa ndio msingi wa ufanisi.

Mhe. Masaju ameongeza kwa kuwakumbusha Wasajili hao kuwa waadilifu hata baada ya kuteuliwa kuwa Majaji na kuacha dhana ya kutaka kuwa Waheshimiwa huku wakiwa wazembe na wavivu kutimiza majukumu yako, badala yake wawe wachapa kazi huku wakiendana na mabadiliko ya vyeo vyao kwa kuzidisha uadilifu na na unyeyekevu.

“Halafu sehemu fulani nimeona Mahakimu wanafanya vizuri wanateuliwa wanakuwa Majaji, baada ya kuwa Jaji akili inaharibika kabisa, unajiuliza hivi huyu mtu tulifanya makosa, mimi nitaendelea kuwafanyia 'monitoring' ili tunaowapendekeza kwenda kuteuliwa wawe ni wale ambao kwa kweli hawana tabia za uvivu, hatutaki cheo cha Ujaji kiwe cheo cha uheshimiwa, kile ni cheo cha utumishi tena cheo kikubwa sana, nilishawaambia kadri unavyokuwa na madaraka makubwa ni kwa kiwango hicho hicho ndivyo unavyopaswa kuwa mnyenyekevu, na kwa kiwango hicho hicho unakuwa mtumishi wa wote  kwa kiwango hicho hicho unakuwa tegemezi kwa wote, sasa wanaopata vyeo vya Ujaji halafu baadae wakaishi maisha ya kujitutumua hatutaki, tunataka mthibitishe kwamba mnaweza kufanya kazi kwa uadilifu,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amesisitiza juu ya vipaumbele vya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ambavyo ni Utawala wa Bora na Haki, Serikali za Mitaa Imara na zenye Ufanisi, Utumishi wa Umma Ulioimarika, pamoja na Amani, Usalama na Utulivu.

Amewataka pia kuwasimamia vizuri Mawakili wa Serikali na Mawakili wa kujitegemea, huku akisisitiza uwajibikaji bila kusubiri maelekezo na kama wakiona kuwa kuna kitu hakiendi sawa watoe ushauri, huku akiwakumbusha Mawakili wote kuwa wao ni Maofisa wa Mahakama hivyo, mashauri yanaposikilizwa wanatakiwa wawepo ili kusikiliza mashauri ya wateja wao.



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza na Wasajili na Naibu Wasajili wa Mahakama ya Tanzania leo tarehe 22 Desemba, 2025 wakati wa kikao kati yake na Wasajili hao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu jijini Dodoma. Kikao hicho kimefanyika kwa njia ya Mtandao (Video Conference) ambapo kilifuatiliwa na Wasajili wengine waliopo katika Kanda mbalimbali nchini.

Picha za makundi mbalimbali ya Wasajili na Naibu Wasajili wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu ya Tanzania wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju alipokuwa akizungumza nao leo tarehe 22 Desemba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu uliopo Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Ijumaa, 19 Desemba 2025

TANZIA; JAJI MSTAAFU WA MAHAKAMA KUU YA TANZANIA AFARIKI DUNIA

 


TANZIA

 Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Julius Benedicto Mallaba enzi za uhai wake.

Mahakama ya Tanzania inasikitika kutangaza kifo cha Jaji Mstaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Julius Benedicto Mallaba kilichotokea leo tarehe 19 Desemba, 2025, saa 10 alfajiri, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa amelazwa akipatiwa matibabu kwa ugonjwa wa sukari na shinikizo la damu.

Marehemu Jaji Mallaba alizaliwa tarehe 12 Machi, 1960. Aliteuliwa kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania tarehe 25 Julai, 2015 na kustaafu rasmi mnamo tarehe 12 Machi, 2020.

Kwa Mujibu wa Msemaji wa Familia, msiba upo nyumbani kwake Mbweni jijini Dar es Salaam. Taratibu nyingine za mazishi zitatolewa na Familia.

Mahakama ya Tanzania inaungana na ndugu, jamaa na marafiki kuomboleza msiba huu wa kuondokewa na mpendwa wetu.

BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LA BWANA LIHIMIDIWE.

    


Jumatano, 17 Desemba 2025

KAMATI YA TAIFA YA MAADILI YA MAWAKILI WA KUJITEGEMEA YAJIPANGA KUONDOSHA MASHAURI 45

  •  Wabainisha hayo walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju
  • Jaji Mkuu aipongeza Kamati hiyo kwa kazi nzuri

  • Jaji Karayemaha, Mwenyekiti wa Kamati hiyo azitaka Kamati za Mikoa za Maadili ya Mawakili kutekeleza majukumu yao ipasavyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. James Karayemaha  ametoa rai kwa Wadau kutoa ushirikiano kwa Kamati hiyo ili kufanikisha usikilizwaji wa   jumla ya mashauri 45 ya mashauri ya kimaadili ya Mawakili wa Kujitegemea ambayo yamepangwa kushughulikiwa ndani ya siku 30. 

Mhe. Karayemaha amebainisha hayo leo tarehe 17 Desemba, 2025 Ofisini kwa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati yeye pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Kamati hiyo walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju kwa lengo la kujitambulisha na kueleza shughuli zinazofanywa na Kamati hiyo.

“Katika kutenda kazi zake, Kamati hii mpaka sasa inazo kesi 45 na mkakati wa kuzisikiliza kesi hizo umeshawekwa vizuri na utaanza tarehe 21 Januari, 2026 na tunatarajia mpaka mwezi wa 3 mwaka 2026 kesi zote 45 ambazo zimesajiliwa ziwe zimekwisha,” amesema Jaji Karayemaha.

Aidha, Mhe. Karayemaha ametoa wito kwa wote waliowasilisha kesi hizo kwenye Kamati wafike ili waweze kutoa ushahidi wao, wasikilizwe na hatimaye haki iweze kutendeka.

Ameongeza pia kwa kutoa wito kwa wale ambao wanalalamikiwa watakapopewa wito wafike kwenye Kamati ambayo Ofisi zake zipo kwenye Jengo la Ofisi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali jijini Dar es Salaam.

“Kwa wale ambao wameleta malalamiko au maombi na ambao hawatafika Kamati kwa kutumia vifungu vya kisheria itafuta malalamiko yao au maombi yao, kwahiyo tunaomba sana mfike. Na wale Mawakili ambao wamelalamikiwa kama hawatafika, Sheria inaruhusu Kamati kusikiliza kesi hiyo upande mmoja, kwa hiyo ni rai yangu kama Mwenyekiti wa Kamati hii, kuwaomba nyote mfike mtakapopewa wito na kesi yako imepangwa tarehe tafadhali fika ili kesi yako iweze kusikilizwa,” amesisitiza Mhe. Karayemaha.

Kadhalika, Mwenyekiti huyo ametoa rai kwa wananchi wanaokumbana na changamoto kutoka kwa Mawakili kuwasilisha malalamiko yao kwenye Kamati hiyo ili yaweze kushughulikiwa.

Amezitaka pia Kamati za Mikoa za Maadili ya Mawakili kutekeleza majukumu yao ipasavyo kwa kuwa Kamati hizo zimeanzishwa ili kuwapunguzia usumbufu wananchi. Amesema, takwimu walizo nazo zinaonesha kuwa, Kamati hizo hazifanyi kazi yoyote isipokuwa watu wanawasilisha malalamiko yao moja kwa moja kwenye Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili.

Akizungumzia kuhusu Rufaa kutoka kwenye Kamati, Mwenyekiti wa Kamati hiyo amemueleza Jaji Mkuu kuwa, mpaka sasa kuna rufaa sita ambazo tatu zipo Mahakama Kuu na tatu nyingine zipo Mahakama ya Rufani ya Tanzania.

Kuhusu mafanikio ya Kamati hiyo, Mwenyekiti amesema ni pamoja na kusikiliza mashauri kwa haki bila kupendelea upande mmoja na kutoa uamuzi haki, kusikiliza mashauri kwa wakati hasa yale ambayo wadaawa wamefika mbele ya Kamati, kusikiliza kesi bila kubanwa sana na kanuni za kisheria (legal technicalities) ili kuweza kutenda haki kwa wote wanaojua sheria na wasioijua sheria.

Ametaja mafanikio mengine kuwa, ni pamoja na kuendeleza mahusiano mazuri na wadau kama vile Mahakama na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), kusuluhisha baadhi ya migogoro.

Mbali na mafanikio, Jaji Karayemaha amesema kwamba, Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili inakabiliwa pia na changamoto kadhaa ambazo ni pamoja na ukosefu wa bajeti, kukosa kanzidata na nyingine ambazo ameeleza kwamba jitihada mbalimbali zimefanywa na Kamati hiyo ili kutatua changamoto hizo.

Akizungumza mara baada ya kupokea Taarifa ya Utekelezaji wa Majukumu ya Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Jaji Mkuu ameipongeza Kamati hiyo kwa kazi nzuri wanayofanya katika utekelezaji wa majukumu yao na kuwaahidi kuendeleza ushirikiano kati ya Mahakama na Kamati hiyo.

Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili ni chombo kilichoundwa kisheria ili kusimamia Maadili ya Mawakili wa Kujitegemea. Kamati hii imeanzishwa chini ya Sheria ya Mawakili Sura ya 341 Marejeo ya mwaka 2023.

Kwa mujibu wa Jaji Karayemaha, Kamati hiyo ina mamlaka ya kusikiliza na kuamua mashauri yote ya kimaadili ya Mawakili wa Kujitegemea Tanzania bara. Mashauri hayo ni pamoja na; Maombi ya Wakili mwenyewe kuomba jina lake kuondolewa katika orodha ya Mawakili, maombi ya mtu mwingine kuomba jina la Wakili fulani kuondolewa katika orodha ya Mawakili na kusikiliza mashauri ya kimaadili ya Mawakili wa Kujitegemea.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. James Karayemaha (wa kwanza mbele upande wa kushoto) wakati Kamati hiyo ilipomtembelea na kufanya mazungumzo na Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. Wengine ni sehemu ya Viongozi wa Mahakama (kulia) na Wajumbe wa Kamati hiyo.

Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mjumbe wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. Samwel Maneno (kushoto) akizungumza jambo wakati wa kikao cha majadiliano na Jaji Mkuu walipomtembelea ofisini kwake leo tarehe 17 Desemba, 2025. Kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. James Karayemaha.


Wakiendelea na majadiliano.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akifuatilia kwa makini kinachojiri wakati wa mazungumzo kati yake na Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili iliyomtembelea leo tarehe 17 Desemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili waliomtembelea leo tarehe 17 Desemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. Wa pili kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. James Karayemaha, wa pili kushoto ni Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mjumbe wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. Samwel Maneno, wa kwanza kushoto ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert na wa kwanza kulia ni Katibu wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili ambaye pia ni Mwanasheria wa Serikali, Bw. Faraji Ngukah.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili waliomtembelea leo tarehe 17 Desemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma. Wa tatu kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Songea ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. James Karayemaha, wa tatu kushoto ni Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Mjumbe wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili, Mhe. Samwel Maneno, wa pili kushoto ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Herbert, wa kwanza kulia ni Naibu Msajili Mwandamizi Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Sundi Fimbo, wa pili kulia ni Katibu wa Kamati ya Taifa ya Maadili ya Mawakili ambaye pia ni Mwanasheria wa Serikali, Bw. Faraji Ngukah na wa kwanza kushoto ni Naibu Msajili na Mkurugenzi wa Maktaba Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Mhe. Kifungu Kariho.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)