Jumamosi, 20 Septemba 2025

USHIRIKIANO KATI YA MAHAKAMA YA TANZANIA NA JESHI LA MAGEREZA WAZAA MATUNDA

·       Kamishna Mkuu wa Magereza asema umepunguza kwa kiasi kikubwa idadi ya malalamiko ya Wafungwa, Mahabusu

·       Waipongeza Mahakama kwa kuondoa zaidi ya asilimia 80 ya changamoto zilizokuwa zikiwakabili Wafungwa na Mahabusu

·       Asema idadi ya Mahabusu yapungua na hakuna Mahabusu wa Mahakama za Mwanzo gerezani

·       Wapongeza matumizi ya Mahakama Mtandao ambapo zaidi ya mashauri 10,000 yamesikilizwa kwa njia hiyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, (CGP) Jeremia Yorum Katungu ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa ushirikiano mkubwa inaoupatia Jeshi hilo ambao umewezesha kupatikana kwa mafanikio lukuki ikiwemo kupungua kwa idadi ya malalamiko ya Wafungwa na Mahabusu.

CGP Katungu alieleza hayo jana tarehe 19 Septemba, 2025 alipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma lengo likiwa ni kusalimiana na kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali kwa ustawi wa utendaji kazi wa vyombo hivyo.

“Matokeo ya ushirikiano huu Mhe. Jaji Mkuu, kwanza magerezani kumekuwa na kupungua kwa malalamiko ya wafungwa na mahabusu kuhusiana na changamoto za mashauri, miaka ya nyuma ilikuwa ukiingia gerezani unaweza kusikiliza malalamiko kuanzia asubuhi mpaka jioni malalamiko yalikuwa mengi sana, lakini sasa hivi nikuhakikishie malalamiko sio kwamba tumeyamaliza yote lakini yamepungua kwa kiasi kikubwa sana na tafsiri yake ni kwamba ni ushirikiano uliopo katika utatuzi wa malalamiko hayo ambayo yamefanya wafungwa na mahabusu kuridhika na hivyo kusababisha utulivu gerezani,” alisema Kamishna Mkuu huyo wa Jeshi la Magereza.

CGP Katungu alishukuru kwa dhati ushirikiano huo ambao umekuwepo kati ya Mahakama pamoja na Jeshi la Magereza na kukiri kuwa, kumekuwa na ziara za mara kwa mara za Majaji na Mahakimu akiwemo Jaji Mkuu ambaye alifanya ziara yake ya kwanza katika Gereza la Isanga tarehe 10 Julai, 2025.  

Kamishna Mkuu huyo alikiri kwamba, ziara hizo zimekuwa na manufaa mengi ikiwemo ushughulikiaji wa mashauri ya wafungwa na mahabusu.

“Usikilizaji wa mashauri ya wafungwa na mahabusu kupitia Mahakama Mtandao ni eneo ambalo pia tumekuwa tukishirikiana vizuri, kama utakumbuka miezi kadhaa iliyopita mlitusaidia kutupa makasha 10 ambayo yanatumika kama vyumba vya Mahakama mtandao lakini pia mmeendelea kutusaidia vifaa vya TEHAMA ambavyo vinatumika kwenye Mahakama mtandao kwakweli tunashukuru katika eneo hilo na tumeendelea kuona ufanisi katika usikilizaji wa mashauri kupitia Mahakama mtandao,” alieleza CGP Katungu.

Kamishna Mkuu huyo wa Magereza alisema kwamba, kuanzia mwaka 2021 ndipo ulianza ushirikiano wa huduma ya wafungwa na mahabusu kusikiliza mashauri yao kwa njia ya Mahakama Mtandao ambapo kufikia Septemba, 2025 huduma ya Mahakama mtandao imeendelea kutolewa katika vituo 97 na mpango uliopo ni kuwa na huduma hiyo katika Magereza yote nchini.

“Katika kipindi cha mwaka 2021 mpaka sasa, zaidi ya mashauri 10,000 yamesikilizwa kwa njia ya huduma ya Mahakama Mtandao katika Vituo hivyo 97 na baadhi maamuzi yamefanyika kwa utaratibu wa Mahakama mtandao na hii kwakweli imekuwa na manufaa sana kuondokana na changamoto za ucheleweshaji wa mashauri,” alisema CGP Katungu.

Aliongeza huku akirejea maelekezo ya Jaji Mkuu alipofanya ziara katika Gereza la Isanga tarehe 10 Julai mwaka huu kuhusu kuondoa mahabusu wa Mahakama za Mwanzo gerezani kwamba maelekezo hayo yamefanikiwa kwa ufanisi mkubwa na sasa.

“Nikupongeze kwa dhati kabisa, maelekezo hayo yamefanikiwa kwa kiasi kikubwa, tumekuwa na mawasiliano ya karibu sana na watendaji  wako kuhusu suala hili na matokeo yanaonekana, sasa ulipokuja Gereza la Isanga kulikuwa na Mahabusu 6, 415 lakini kwa tarehe 18 Septemba, 2025 idadi ya mahabusu waliopo ni 4,658, utaona kuna idadi ya zaidi ya mahabusu 1,757 wamepungua na hayo ni matokeo ya ziara ambayo ulifanya na maelekezo uliyotupa ambayo utekelezaji wa maelekezo yako umeanza kuzaa matunda, na kitu cha kujivunia sana ni kwamba, tunavyozungumza sasa Mahabusu wa Mahakama za Mwanzo hatuna magerezani,” alieleza.

Aliongeza kuwa, Mahakama na Magereza inashirikiana pia ni katika eneo la kubadilishana taarifa ambapo alirejea maelekezo ya Jaji Mkuu alipofanya ziara katika Gereza la Isanga ambapo pamoja na mambo mengine aliomba kupatiwa taarifa za kila siku za idadi za Wafungwa na Mahabusu waliopo katika magereza mbalimbali nchini, amesema kazi hiyo wanaitekeleza kwa dhati kwa kuwa manufaa yake wameanza kuyaona ikiwemo kupungua kwa mashauri pengine hayakuwa na ulazima wa kukaa kwa muda mrefu.

“Lakini kuna kupungua kwa idadi ya waliopo gerezani hususani Mahabusu, Mhe. Jaji Mkuu nitoe tu takwimu kidogo ulifanya ziara tarehe 10 Julai, 2025, maelekezo uliotoa tunaendelea kuyatekeleza, lakini wakati unafanya ziara ile idadi ya wafungwa na mahabusu ilikuwa 25,784 lakini hadi kufikia tarehe 18 Julai mwaka huu idadi ilikuwa 24,761 kwahiyo idadi imepungua hususani ya mahabusu na kwamba Serikali imepunguza gharama kubwa ya kuwahudumia mahabusu na wafungwa,” alisema CGP Katungu.

Aidha, alizungumzia kuhusu changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni pamoja na vikao vya Mahakama Kuu kuchukua muda mrefu kufanyika, changamoto ya kupatikana kwa mtandao kwenye Mahakama mtandao, mahitaji ya vifaa vya TEHAMA,

“Magereza mengi hayana miundombinu inayowezesha urekebishaji wa wafungwa, kuna haja ya kuwa na viwanja vya michezo na burudani ndani ya viwanja vya Magereza, kuna haja pia ya kuwa na vyumba maalum vya kutumika kama madarasa. Kwahiyo sasa hivi magereza nyingi tunazojenga tunajitahidi kuweka miundombinu muhimu itakayowezesha urekebishaji,” alisema.

Kamishna Mkuu huyo alieleza kuwa, kuna changamoto ya baadhi ya Wilaya kukosa Magereza na kwamba lengo ni Wilaya zote ziwe na Magereza ili kurahisisha usafirishaji wa wafungwa na mahabusu. Ameongeza kwamba kwa sasa kuna ujenzi unaendelea wa jumla ya magereza 12.

Aliongeza kwamba vitendea kazi bado ni changamoto hasa magari, Serikali inaendelea kutoa fedha kwa ajili ya kununua magari na hivi karibuni wamepokea jumla ya magari 10 aina Land Cruiser pick up 10.

Naye, Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza kutoka Jeshi Magereza nchini (CP) Nicodemus Tenga alisema kuwa, kwa sasa Jeshi hilo lina Wanasheria zaidi ya 264 na wamesambazwa kwenye vituo mbalimbali vya Magereza ikiwemo Magereza ya mikoani na wilayani.

Aidha, CP Tenga ameishukuru Mahakama kwa kuwafundisha wanasheria hao jinsi ya kutumia Mfumo wa Kieletroniki wa Usimamizi wa Mashauri (e-CMS) na kuwezesha magereza zote nchini kutumia mfumo huo na kuondokana na matumizi ya karatasi na imesaidia kupungua zaidi ya asilimia 80 ya changamoto kufuatia matumizi ya mfumo.

Akizungumza mara baada ya kupokea taarifa kutoka kwa Kamishna Mkuu wa Magereza nchini, naye Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju alimpongeza Kamishna huyo kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akifanya ambayo matokeo yanaonekana.

“Niwapongeze kwa haya mambo makubwa ambayo mmekuwa mkiyafanya naona unayatekeleza kwa kiwango kikubwa sana licha ya changamoto, nashukuru sana kwa hii taarifa ambayo umetupatia ni taarifa ambayo imejitosheleza ambayo itatusaidia sisi kuboresha huduma         zetu ili kuhakikisha kwamba wajibu wetu katika utekelezaji wa haki jinai unatekelezwa kwa ufanisi ipasavyo,” alisema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu alisema kwamba, kuna umuhimu mkubwa wa kuwa ushirikiano na uhusiano mzuri baina ya Wadau wa Haki Jinai wakiwemo Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Jeshi la Polisi, TAKUKURU, Mamlaka ya Kupambana na Kuzuia Madawa ya Kulevya, Jeshi la Uhamiaji na wananchi ambalo lengo lake ni kupata na kuboresha utekelezaji wa majukumu kwa ufanisi kila sehemu ili lengo lililokusudiwa lifanikiwe.

Aidha, Mhe. Masaju amemtaka Kamishna huyo kuwa kama kuna changamoto zozote zinazohusu Mahakama ambazo zitaendelea kujitokeza asisite kuijulisha Mahakama na kwamba kwa sasa hatatembelea Magereza hadi atakapohakikisha kuwa changamoto zilizopokelewa wakati wa ziara yake katika Gereza la Isanga zifanyiwe kazi/ziishe.

“Nawashukuru kwa ushirikiano mkubwa ambao mmeendelea kutupatia hususani utoaji taarifa, na kwamba kuna taarifa au changamoto zaidi msisubiri tuwaombe nyie andikeni tuyafanyie kazi,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Aidha, amewashauri Viongozi hao wa Jeshi la Magereza kushughulikia mapema mapema maombi ya wafungwa wanaosubiri msamaha wa Rais kwa sababu kuna Kamati mahsusi ya kumshauri Rais kuhusu msamaha kwa wafungwa wanaosubiri adhabu ya kifo kwa kufuata utaratibu husika, kwa sababu itasaidia kupungua idadi ya wafungwa.

Aidha, Mhe. Masaju amemuomba Kiongozi huyo wa Jeshi la Magereza kuandaa taarifa kuhusu utekelezaji wa Kifungu cha 134 cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai, ili kujua kama kweli mashauri hayo yanamalizika ndani ya miezi sita.

“Tunatengeneza pia Kanuni ambazo zitawezesha katika mashauri yanayosikilizwa na Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya wao nao Mahakama na washtakiwa wawe nao sasa wanapata ushahidi wa upande wa kesi za mashtaka ili iwasaidie na wao kujitetea kwa ufanisi ipasavyo, haitoshi tu kwamba kumpa haki ya kusikilizwa lakini akiwa hana taarifa za tuhuma na ushahidi uliopo dhidi yake hapo hakutakuwa na haki ya kusikilizwa aliyopewa itakuwa imenyofolewa kwa kiasi fulani na itakuwa inakiuka Ibara ya 13 ya Katiba inayotaka usawa mbele ya sheria,” alisisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju alilipongeza Jeshi la Magereza kwa kazi kubwa ya urekebishaji wanaofanya na kulishauri Jeshi hilo kuangalia uwezekano wa kuwarudisha hadi mipakani wafungwa kutoka nchi za Jirani za Jumuiya ya Afrika Mashariki ambao wanamaliza kutumikia mifungo vyao badala ya kuendelea kujaza idadi ya wafungwa magerezanina kuwa na wahamiaji haramu nchini.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akizungumza jambo na Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini (CGP), Jeremia Yoram Katungu alipotembelewa na Mkuu huyo wa Jeshi la Magereza ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akizungumza na ujumbe kutoka Jeshi la Magereza nchini ulioongozwa na Mkuu wa Jeshi hilo, CGP Jeremia Yorum Katungu walipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Walioketi kulia ni sehemu ya Viongozi wa Mahakama.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo na 
Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, (CGP) Jeremia Yorum Katungu (hayupo katika picha) na Viongozi wengine wa Jeshi hilo waliomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, (CGP) Jeremia Yorum Katungu akifurahia jambo wakati wa mazungumzo na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania alipokutana na kufanya mazungumzo naye jana tarehe 19 Septemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, (CGP) Jeremia Yorum Katungu akisaini kitabu cha wageni alipowasili ofisini kwa Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju kwa lengo la kusalimiana na kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali ya utendaji kazi wa Mahakama na Jeshi la Magereza.

Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza kutoka Jeshi Magereza nchini (CP) Nicodemus Tenga akizungumza jambo wakati wa mazungumzo kati ya Jaji Mkuu na Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini yaliyofanyika jana tarehe 19 Septemba, 2025 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

 Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Hubert (kushoto) akizungumza jambo wakati wa mazungumzo hayo. Kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama ambaye pia ni Msaidizi wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi.
Mazungumzo yakiendelea..

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Kamishna Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, (CGP) Jeremia Yorum Katungu (wa pili kushoto). Wa pili kulia ni Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza kutoka Jeshi Magereza nchini (CP) Nicodemus Tenga, wa kwanza kushoto ni Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. George Hubert.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)





 

 

Ijumaa, 19 Septemba 2025

TLS YAKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA JAJI MKUU WA MAHAKAMA YA TANZANIA

Matukio katika picha wakati Viongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) walipokutana na kufanya mazungumzo na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 19 Septemba, 2025.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (aliyeketi mbele) akiwa na sehemu ya Viongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 19 Septemba, 2025.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza jambo na sehemu ya Viongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) waliomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 19 Septemba, 2025.

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bw. Boniface Mwabukusi (kulia) akizungumza jambo na Jaji Mkuu (hayupo katika picha) wakati viongozi wa Chama hicho walipomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma leo tarehe 19 Septemba, 2025. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa TLS, Bi. Mariam Othman.
Mazungumzo yakiendelea.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akimkabidhi Majarida ya Mahakama ya Tanzania (HAKI Bulletin) Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bw. Boniface Mwabukusi walipomtembelea Jaji Mkuu leo tarehe 19 Septemba, 2025 ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Viongozu kutoka TLS walipomtembelea ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Wa nne kushoto ni Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Bw. Boniface Mwabukusi, wa tatu kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa TLS, Bi. Mariam Othman na Viongozi wengine wa Chama hicho.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)








MBEYA YAFANYA MAANDALIZI YA VIKAO VYA USIKILIZAJI MASHAURI YA MAUAJI

Na. Daniel Sichula – Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga afungua kikao cha awali cha maandalizi ya usikilizwaji wa mashauri ya kesi za mauaji kwa mwaka 2025/2026 ambapo mashauri hayo yataendeshwa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya na Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe.

Akitoa taarifa ya tathimini Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu alisema kuwa mashauri 16 yamepangwa kusikilizwa kuanzia tarehe 22 Septemba 2025 ambapo Mashauri 08 yatasikilizwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe mbele ya Jaji Mfawidhi wa Mahakama kuu Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga na mashauri 08 yatasikilizwa Mbeya mbele ya Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa.

Baada ya kupokea taarifa ya tathimini kutoka kwa Mhe. Temu wajumbe walijadili juu ya changamoto zinzoweza kujitokeza na namna ya kuzitatua kabla ya usikilizwaji wa mashauri kuanza ikiwepo ya mahabusu walioko mbali na sehemu ambako mashauri yao yatasikilizwa.

 Akiwasilisha hoja Afisa Magereza alisema Mhe. Jaji watu wote wapo mahabusu ila kuna baadhi ya mahabusu wapo Mbeya na mashauri yao yatasikilizwa Songwe na bado hawajafuatwa.

Akijibu hoja hiyo Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Mbeya, Mhe. Temu alisema kuwa “maandalizi yote yameshakamilika na wadaawa wamepelekewa wito wa kuitwa Mahakamani wakiwemo walioko Songwe na muda wowote kuanzia hivi sasa mahabusu hao watakuwa wamesha fuatwa kwa ajili ya kusikiliza mashauri yao huko Songwe”.

Akiwasilisha taarifa kutoka Ofisi ya waendesha mashtaka mkoa wa Mbeya (NPS), kuwa kwa upande wao hakuna changamoto yoyote kwenye mashauri yatakayoingia kwenye vikao hivyo.

“Mhe. Jaji, mashahidi wamepigiwa simu na kupewa wito wa kufika mahakamani na wametoa ushirikiano wa kutosha na kuthibitisha kuwa wapo tayari kuja kutoa ushahidi wao” alisema mwakilishi kutoka ofisi ya mwendesha mashitaka mkoa wa Mbeya (NPS).

Kwa upande wa Ofisi ya Mwendesha Mashitaka Mkoa wa Songwe waliwasilisha taarifa za mashauri 08 yanayotarajiwa kusilikilizwa mkoani Songwe na walithibitisha kuwa hakuna changamoto yoyote na wapo tayari kwa vikao hivyo.

Aidha, Mawakili wa utetezi nao pia walitoa taarifa zao kuwa nao hawana changamoto yoyote mandalizi yanaendelea vizuri na wako tayari kwa vikao hivyo kuwasimamia wateja wao.

“Niwapongeze washiriki wote, Ofisi ya NPS, Ofisi ya RCO Mbeya na Songwe na Mawakili wa kujitegemea kwa hatua mlizofikia na kuonesha kuwa hadi sasa hakuna changamoto yoyote na mupo tayari kwa ajili ya usikilizaji wa mashauri yaliyopo mbele yetu na kuwasisitiza muda tuliokubalina hapa wa kuanza kusikiliza mashauri yaliyopo mbele yetu tuuzingatie,” alisema Mhe. Tiganga

“Matarajio ni kumaliza kesi zote za vikao hivi vilivyoandaliwa na ninawahakikishia kuwa tumejipanga na kesi zote zitasikilizwa na kumalizika, ninawasisitiza kuwa wepesi kubadilika kuendana na mazingira ya hali yoyote ya mabadiliko itakayojitokeza.” Mhe. Jaji Tiganga alisema.

Kikao hicho kilihudhuriwa na Mtendaji wa Mahakama Kuu Mbeya Bi. Mavis Miti, Mawakili wa Serikali, Mawakili wa Kujitegemea, Mwakilishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Gereza Mbeya, Ofisi ya Upelelezi Mkoa wa Mbeya na Songwe na Ofisi ya Waendesha Mashtaka (NPS) Mkoa wa Mbeya na Songwe.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga (kushoto) akiwa na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu wakiongoza kikao cha awali cha tathimini usikilizaji wa mashauri ya mauaji kwa Mahakama Kuu Mbeya na Mahakama Mkoa wa Songwe.

Sehemu ya washiriki katika kikao cha awali cha tathimini usikilizaji wa mashauri ya mauji.

Sehemu ya washiriki katika kikao cha awali cha tathimini usikilizaji wa mashauri ya mauji.

Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Mbeya Bi. Mavis Miti akiwa mmoja ya washiriki wa kikao hicho

Afisa Magereza akichangia maoni yake katika kikao hicho

Sehemu ya washiriki katika kikao cha awali cha tathimini usikilizaji wa mashauri ya mauji

TANZIA; MTUMISHI WA MAHAKAMA KUU KANDA YA MWANZA AFARIKI DUNIA

 TANZIA

Bi. Febronia John Mayala enzi ya uhai wake 

Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza inasikitika kutangaza kifo cha mtumishi wake Bi. Febronia John Mayala ambaye alikuwa Msaidizi wa Kumbukumbu daraja la I kilichotokea mnamo tarehe 16 Agosti 2025 katika hospitali ya Kamanga Wilaya ya Nyamagana Mkoa wa Mwanza

Kwa mujibu wa Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza Bw. Tutubi Mangazeni marehemu Bi. Febronia aliajiriwa mnamo tarehe 21 Septemba, 2015 katika kada ya Msaidizi wa Kumbukumbu II.

Baada ya kuajiriwa alipangiwa Kituo chake cha kwanza cha kazi cha ajira huko Mahakama ya Wilaya Sengerema na baada ya hapo akahamishiwa Mwanza IJC ambapo alipangiwa Mahakama ya Wilaya Ilemela na baadaye kuhamishiwa Mahakama ya Hakimu Mkazi mpaka umauti ulipomfika

Ameajiriwa na elimu ya Stashahada ya utunzaji wa kumbukumbu (Diploma in Record Management) katika Chuo cha Utumishi wa Umma tawi la Tabora

Marehemu Bi. Febronia anatarajiwa kuzikwa Mwanza katika makaburi ya Buhongwa leo tarehe 19 Septemba, 2025.

Bwana ametoa na Bwana ametwaa Jina la Bwana Lihimidiwe


Alhamisi, 18 Septemba 2025

MAFUNZO YA UENDESHAJI MASHAURI YA UCHAGUZI KWA MAJAJI, MAHAKIMU YAHITIMISHWA

·       Jaji Mkuu asema ipo haja ya kufanya marekebisho ya Kanuni za uchaguzi

·       Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman ashiriki kutoa uzoefu kuhusu mashauri ya uchaguzi

·       Jumla ya washiriki 381 wanufaika na mafunzo hayo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi yaliyokuwa yakitolewa kwa Majaji, Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na za Wilaya nchini yamehitimishwa leo, huku Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akishauri kwamba Kanuni za Uchaguzi zifanyiwe marekebisho ili kuwawezesha Majaji na Mahakimu kusikiliza ipasavyo mashauri hayo.

Akizungumza leo tarehe 18 Septemba, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma wakati akifunga mafunzo hayo yaliyohusisha washiriki wa kundi la mwisho la Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Masaju amesema majadiliano mbalimbali pamoja na changamoto zilizowasilishwa na washiriki wa Mafunzo yameonesha kuwa, kanuni hizo zina mapungufu na hivyo kuwa na haja ya kuzifanyia mabadiliko.

“Niwashukuru kwa kukubali kufanya mabadiliko ya kanuni hizi zinazotungwa na Jaji Mkuu, tumepata ushauri mzuri hapa na Jaji Mkuu Mstaafu ametushauri maeneo ya kuangalia , tuna pa kuanzia na wawezeshaji wetu ni mahiri na ninyi wenyewe ni mahiri mna ustadi mkubwa kwenye maeneo haya na hili tutalifanya kabla ya tarehe ya uchaguzi wenyewe na litakuwa zoezi shirikishi lakini  maboresho ya mwisho yatakayotolewa lazima yapate kibali cha Mahakama maana sisi ndio wenye ile sheria na mwenye mamlaka ya kuitunga ile sheria ni Jaji Mkuu,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa, lengo la kufanyia marekebisho kanuni hizo ni kwa sababu ni sheria za uchaguzi zimekusudia kufikia lengo la wananchi la kupata Serikali ambayo itawajibika kwao kwa ajili ya ustawi wao wananchi kama inavyotajwa kwenye Ibara ya 8 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambapo pamoja na mambo mengine inasema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi ya kidemokrasia na inayofuata haki ya kijamii na kwamba mamlaka ya Serikali hiyo yatapatikana kutoka kwa wananchi.

‘.... Na kwamba wananchi ndio msingi wa mamlaka yote na Serikali itapata madaraka na mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii na lengo kuu la Serikali ikiwa ni ustawi wa wananchi na Serikali ikiwajibika kwa wananchi,’ amenukuu Mhe. Masaju akirejea Ibara ya 8 ya Katiba.

Ameongeza kuwa, lengo lingine la kufanya maboresho kwenye kanuni hizo ni kuleta uwazi zaidi katika kupata tafsiri sahihi ya migogoro ya uchaguzi inayoletwa mahakamani na kujua kama uchaguzi ulikuwa huru na wa haki.

Amesema kuwa, katika mazingira kama hayo, Mahakama ambayo ina jukumu la kutunga kanuni za kusimamia mashauri ya uchaguzi lazima ijiridhishe kama kanuni hizo zinakidhi matarajio ya wananchi ili watu wanaokuwa na mashauri ya uchaguzi mahakamani yaamuliwe kwa namna ambayo wanaridhika kwamba maamuzi hayo yamefanyika kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi.

Ameeleza kuwa, baadhi ya changamoto zilizoonekana katika Kanuni hizo ni pamoja na kukosekana kwa uwazi na uhakika pamoja na mapungufu mengine yatakayobainika baada ya kuzipitia kanuni hizo.

Kufuatia maelekezo ya Jaji Mkuu kuhusu mabadiliko ya kanuni za uchaguzi, Majaji wa Mahakama ya Rufani kwa pamoja wamepanga kukutana Jumatatu tarehe 22 Septemba, 2025 ili kupitia kanuni hizo za uchaguzi na kutoa mapendekezo ya maboresho yake.

Aidha, Mhe. Masaju ameeleza kwamba, mashauri yanayotokana na migogoro ya uchaguzi yatasikilizwa katika Mahakama zilizopo nchini na kuwataka watu wanaohitaji kufuatilia mashauri hayo kufika katika Mahakama husika wasikilize kwa amani na kwa kufuata na kuheshimu taratibu za Mahakama. Ametoa rai kwa mtu ambaye hataridhika na uamuzi wa Mahakama ya ngazi fulani ana haki ya kukata rufaa kwa kuwa ni haki ya kikatiba.

Mhe. Masaju amesisitiza kuwa, Mahakama inalo jukumu la kudumisha utawala wa sheria katika nchi kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba ambapo amethibitisha kwamba Mahakama itahakikisha inaendelea kufanya hivyo.

“Pamoja na mamlaka tuliyo nayo ya kikatiba na kisheria, mamlaka yetu pia yapo katika uwezo wetu wa kufanya maamuzi ya Mahakama kwa maslahi ya sheria, amesema Jaji.

Kadhalika, Jaji Mkuu ameeleza kwamba hakutakuwa na urushaji mubashara (live streaming) ya mashauri hayo na kusisitiza kuwa, “hakutakuwa na ‘live streaming’ ya mashauri hayo huku akirejea kinachozungumziwa kwenye Ibara ya 18 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa; ni haki ya kupata taarifa sio haki ya kutangazwa wakati wote.

Katika hatua nyingine amewashukuru waandaaji wa mafunzo hayo Mahakama na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, wawezeshaji pamoja na washiriki wote wa mafunzo hayo kushiriki kikamilifu.

“Nawashukuru washiriki wote, waandaaji na Wawezeshaji wa Mafunzo haya ambayo niliyafungua tarehe 28 Agosti, 2025 lakini katika ngazi mbalimbali, tulianza na Mahakama Kuu kwa pamoja, Naibu Wasajili, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na za Wilaya, zoezi ambalo limefanyika kwa ustadi mkubwa sana,” amesema Mhe. Masaju.

Kwa upande wake Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman ametoa uzoefu wake kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani juu ya mashauri yatokanayo na migogoro ya uchaguzi ambapo ameshauri juu ya menejimenti fasaha ya mashauri ya uchaguzi kwa kuwa yanagusa Taifa, kuwa na matumizi fasaha ya lugha na mengine.

“Tuwajibike ipasavyo na tutumie uchaguzi huu kujiimarisha kama Mahakama kupitia maamuzi yetu kujenga ‘integrity’ ya Mahakama,” amesema Mhe. Chande.

Jaji Mkuu huyo Mstaafu amesisitiza mambo ya kuzingatia kuwa ni pamoja na Mahakama kuangalia Sheria na wajibu wake kwenye masuala ya uchaguzi, usikilizwaji wa mashauri ya uchaguzi mapema ipasavyo na Mahakama iwe na uwazi na yenye kufikika kwa kuwa mashauri hayo yana maslahi ya umma.

Mhe. Chande amesema, mafunzo hayo yamekuja wakati muafaka kwa kuwa uchaguzi na migogoro ya uchaguzi kwa kiasi kikubwa ni muingiliano kati ya siasa na sheria. 

Majaji wengine walioshiriki kutoa uzoefu wao kuhusu mashauri ya migogoro ya uchaguzi ni Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ferdinand Wambali na Mhe. Issa Maige.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto yalifunguliwa na Jaji Mkuu tarehe 28 Agosti, 2025 lengo likiwa ni kuimarisha uwezo wa Maofisa Mahakama, yaani Majaji na Mahakimu katika namna bora ya kuendesha mashauri ya uchaguzi ili kuwaweka tayari kushughulikia mashauri hayo kwa weledi na mapema ipasavyo pale ambapo wadaawa watakuwa wamegonga milango ya Mahakama kutafuta haki.

Kwa mujibu wa Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama (IJA) Lushoto, Mhe. Dkt. Paul Kihwelo mafunzo hayo yametolewa kwa jumla ya washiriki 381 wakiwemo Majaji wa Mahakama Rufani, Majaji wa Mahakama Kuu, Naibu Wasajili, Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Hakimu Mkazi na za Wilaya.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi leo tarehe 18 Septemba, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ferdinand Wambali.

Sehemu ya Washiriki wa mafunzo  ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi wakifuatilia hotuba ya ufungaji wa mafunzo hayo iliyokuwa ikitolewa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) leo tarehe 18 Septemba, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Jaji Mkuu Mstaafu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Mohamed Chande Othman akizungumza jambo na Majaji wa Mahakama ya Rufani waliokuwa wakishiriki katika Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi leo tarehe 18 Septemba, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija (kushoto) akizungumza jambo wakati wa Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi leo tarehe 18 Septemba, 2025 yaliyokuwa yakitolewa kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani katika ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju.

Washiriki wa mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi wakifuatilia kinachojiri wakati wa majadiliano.
Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (kulia) akiwa katika picha ya pamoja na Jaji Mkuu Mstaafu, Mhe. Mohamed Chande Othman alipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake jijini Dodoma na kupata fursa ya kushiriki kutoa uzoefu wa uendeshaji wa mashauri ya uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama wa Mahakama ya Rufani waliokuwa wakishiriki katika Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mkuu wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) akizungumza jambo wakati wa mafunzo hayo.

Sehemu ya Majaji wa Mahakama ya Rufani wakifuatilia kwa umakini kinachojiri katika Mafunzo ya Namna Bora ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi.


Jaji wa Mahakama ya Rufani na Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Mary Caroline Levira akitoa neno la shukrani wakati wa hafla ya kufunga Mafunzo ya namna Bora ya Uendeshaji Mashauri ya Uchaguzi yaliyokuwa yakitolewa kwa Majaji wa Mahakama ya Rufani leo tarehe 18 Septemba, 2025 jijini Dodoma. Kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Ferdinand Wambali.
 

Sehemu ya Majaji na Viongozi wengine wa Mahakama ya Rufani wakifuatilia kinachojiri.Wa kwanza kulia ni Mtendaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bw. Victor Kategere na anayefuatia ni Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. George Hubert.


(Picha na MARY GWERA, Mahakama)






 

 









JAJI MWARIJA ATOA RAI KWA MACHIFU KUWA MABALOZI WA UTOAJI ELIMU YA MAHAKAMA

·  Jaji Kiongozi naye asema Machifu wana mchango mkubwa katika usuluhishi wa migogoro

   Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija ametoa rai kwa Machifu nchini kuendelea kuwa mabalozi wa utoaji elimu ya Mahakama kwa jamii.

Mhe. Mwarija alieleza hayo tarehe 16 Septemba, 2025 wakati Machifu kutoka Mikoa ya Kusini walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama jijini Dodoma.

Jaji Mwarija alisema kuwa, suala la utoaji elimu ya Mahakama ni muhimu kuzingatiwa ambapo alisema, “kuna desturi moja ya watu wetu, mtu anayeshinda kesi ananyamaza kimya, anayeshindwa anapiga kelele kwahiyo ukiona Mahakama inalaumiwa mara nyingi ni wale ambao wameshindwa kesi kwa mujibu wa sheria kabisa lakini wale walioshinda hawatokezi wakisema kuna haki mahakamani, kwa hiyo sasa nyie kwa vile mpo karibu zaidi na jamii ni muhimu mlisemee hilo na kuelimisha jamii ili kujua kuwa Mahakama inafanya kazi kwa mujibu wa sheria.”

Mhe. Mwarija alisema, sasa hivi, Mahakama ina Mahakimu hadi wa Mahakama za Mwanzo ambao wana Shahada za Sheria kwahiyo wapo karibu zaidi na kule ambako Machifu wapo hivyo inapotokea kwamba wanahitaji kujifunza kuhusu jambo fulani hasa kuhusu masuala ya haki inawezekana kwa wakati wowote.

Aliongeza kwa kuwaomba Machifu hao kuendelea kuwa macho ya Mahakama na kushiriki kutoa baadhi ya mitazamo hasi ya jamii kwa Mhimili huo. 

Akizungumzia kuhusu Kongamano la Machifu wa Mikoa ya Kusini, Mhe. Mwarija amewapongeza Machifu hao na kusema kwamba wamefanya vizuri na kurudisha mshikamano baina yao na kwamba Mahakama pia ipo tayari kushirikiana nao.

Kadhalika, Mhe. Mwarija aliwasihi Machifu hao kuendelea kusimamia maadili ya vijana kwa kuwa yanaporomoka kwa kiasi kikubwa.

“Maadili ya vijana kwakweli yanaporomoka sana labda sio vijana tu lakini hata watu wazima kwa hiyo sasa kazi ya Machifu inazidi kuwa ni ya muhimu sana na naunga mkono kama mlivyosema mtambulike kisheria, nadhani Jaji Mkuu yupo kwenye nafasi nzuri ya kusaidia kuhimiza hili ili mamlaka husika ziweze kusaidia katika hili,” alisema Jaji Mwarija.

Aidha, Mhe. Mwarija aliwapongeza Machifu hao kwa kuwa na maono mpaka ya kuanzisha Asasi ambapo alisema kwamba ni hatua nzuri kwani Machifu wa sasa wanakwenda kulingana na mazingira ya sasa tofauti na wale wa zamani.

“Niseme tu kwamba ugeni huu ambao umetutembelea ni wa baraka sana na muhimu pia kwetu Mahakama kwa sababu ya majukumu ya Machifu wanakuwa sehemu ya wadau wetu wa haki kwa sababu wanasimamia maadili ya jamii, utamaduni na hata kulinda mazingira,” alisema Jaji Mwarija.

Akitoa neno wakati wa mazungumzo kati ya Machifu hao na Jaji Mkuu, kwa upande wake Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani alisema kuwa mchango wa Machifu katika kuhakikisha kwamba jamii zinakaa kwa amani na usalama ni mkubwa na haupaswi kuupuzwa.

“Sisi kama Mahakama tumeanza kushirikiana nao japo si kwa ukubwa sana lakini tumeanza kuwatambua, Kituo chetu kile cha Usuluhishi Mahakama Kuu Dar es Salaam kwa miaka kama miwili sasa mfululizo kimekuwa kikiwatambua Viongozi wa jadi na Machifu wanaofanya vizuri kwenye usuluhishi,” alisema Jaji Kiongozi.

Aliongeza kwa kutoa mfano wa mwaka jana Mahakama ilipata Machifu wawili ambapo mmoja ni Chifu wa Morogoro (Kingalu) ambaye anafanikiwa kwa kiasi kikubwa kwenye usuluhishi na mwingine ni wa Lindi ambaye kwa kiasi kikubwa alifanya usuluhishi kusababisha Mahakama ya Mwanzo kukosa kesi.

“Kwakweli usuluhishi ambao ndio hasa Viongozi wetu wa asili na Machifu wamekuwa wakiufanya una nafasi kubwa sana ya kuleta utulivu tofauti kabisa na sisi tunavyosikiliza mashauri, sisi tunaposikiliza mashauri mmoja tu atashinda na mwingine atashindwa hakuna nafasi ya kutoka sawa ‘draw’ na hiyo inatengeneza uadui, aliyeshindwa atatengeneza uadui kwa Hakimu lakini pia kwa yule aliyeshinda,” alisema Mhe. Dkt. Siyani.

Kadhalika, Jaji Kiongozi alisema kwamba, Machifu wanafanya kazi kubwa ambayo inatakiwa kutambulika zaidi kwa kuwa historia ya nchi pia inaonesha mchango wao hivyo ni muhimu kuangalia namna ya kuwatumia vizuri zaidi bila kuleta mgongano wa majukumu.

Kadhalika, Mhe. Dkt. Siyani alitoa rai kwa Machifu hao kuendelea kutoa elimu na kuangalia namna ambavyo wanaweza kufanya kazi zao katika mazingira ya sasa bila kuleta mgongano ya kuonesha kwamba pengine wanaingilia majukumu ya Mahakama au kuingilia majukumu ya Mabaraza ya Kata.

Machifu hao kutoka Mikoa ya Kusini inayojumuisha mikoa ya Lindi, Ruvuma, Mtwara, Iringa, Morogoro, Njombe, Rukwa, Songwe na Mbeya waliongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Akida Wabu (AWADEF), Prince Ibrahim Samata ambaye pamoja na mambo mengine alimueleza Jaji Mkuu kwamba lengo la kuanzisha Shirika hilo kuwa ni kuhifadhi urithi wa kitamaduni wa Tanzania, uhifadhi na utunzaji wa mazingira, utawala bora, kukuza maendeleo endelevu na kuwezesha kuunga mkono juhudi za Serikali za kuboresha maisha ya Watanzania.

“Tumepanga kufanya Semina ya kuwajengea uwezo Machifu wa Mikoa hiyo ya kusini ambayo itakusanya Machifu takribani 200 kutoka kwenye mikoa hiyo tisa ili pamoja na mambo mengine kuwajengea uwezo katika masuala ya uongozi, masuala ya maadili, masuala ya malezi na makuzi na kuwaongezea uelewa juu ya mifumo ya Taasisi mbalimbali zinavyofanya kazi ikiwemo Mahakama kama Chombo cha haki ambacho kimeendelea kuaminiwa na Watanzania tangu enzi hizo na enzi hizi,” alisema Prince Samata.

Ugeni wa Machifu hao umekuwa na faida kwa Mahakama kufuatia Mahakama kupatiwa ardhi ya hekari 56 wilayani Ikungi ambayo imetolewa na Chifu Adamu Gwau wa Wilaya hiyo na Machifu wengine wa Mikoa ya Kusini nao wameahidi kutoa ardhi kwa Mahakama kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ili kuwafikia wananchi hadi katika ngazi za Kata.

Jaji wa Mahakama ya Rufani na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija akizungumza na sehemu ya Machifu kutoka Mikoa ya Kusini (hawapo katika picha) wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania tarehe 16 Septemba, 2025 ofisini kwako Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza na sehemu ya Machifu kutoka Mikoa ya Kusini (hawapo katika picha) wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania tarehe 16 Septemba, 2025 ofisini kwako Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Mazungumzo kati ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Machifu kutoka Mikoa ya Kusini yakiendelea wakati Machifu hao walipomtembelea Jaji Mkuu ofisini kwake Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma tarehe 16 Septemba, 2025.
Mazungumzo yakiendelea.

 
Picha ya pamoja na Machifu. Katikati ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju, wa pili kushoto ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Augustine Mwarija, wa pili kulia ni Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, wa kwanza kushoto ni Chifu Mkuu wa Wayao Tanzania na Mwenyekiti wa Asasi ya Maendeleo ya Akida Wabu (AWADEF), Chifu Saad Wabu Mussa Mitondo II na wa kwanza kulia ni Chifu wa Wilaya ya Ikungi-Singida, Bw. Adam Gwau.

(Picha na MARY GWERA, Mahakama)