Alhamisi, 7 Agosti 2025

KITUO JUMUISHI TEMEKE, TAASISI ZA FEDHA WAJADILI MAREKEBISHO YA KANUNI ZA MIRATHI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama

Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke jana tarehe 6 Agosti, 2025 kilikutana na Wawakilishi wa Mabenki Mkoa wa Dar es salaam kujadili na kupata uelewa wa pamoja kuhusu marekebisho ya kanuni yaliyofanywa na Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania kwa Msimamizi wa Mirathi kufungua akaunti moja maalum ya kuhifadhi fedha za marehemu wakati wa usikilizaji wa mashauri ya mirathi.

Kutokana na marekebisho hayo, fedha za mirathi zitakuwa zinawekwa katika akaunti maalum inayoitwa ‘Special Mirathi Account’ badala ya kuwekwa katika akaunti ya mirathi ya Mahakama kwa utaratibu wa awali.

Msimamizi wa Mirathi atafungua akaunti hiyo itakayopokea fedha za mirathi za kutoka Taasisi mbalimbali za fedha badala ya fedha hizo kuwekwa katika akaunti ya mirathi mahakamani.

Akizungumza wakati anafungua majadiliano hayo, Jaji Mfawidhi, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa aliwaeleza Wadau hao kuwa kabla ya marekebisho ya Kanuni za Mirathi, kupitia Tangazo la serikali Na 429 la 2025, fedha za mirathi kutoka Taasisi za fedha zilikuwa zikiwekwa katika akaunti moja ya Mahakama inayoitwa ‘Judiciary Mirathi Account.’

Alieleza kuwa kufuatia marekebisho hayo wameona ni vema wakakutana na Wadau hao muhimu wa Mahakama hiyo ili kujadiliana na kuwa na uelewa wa pamoja namna ya utekelezaji, kwani kwa sasa takwa la kisheria kwa Msimamizi wa Mirathi ni kufungua akaunti maalum inayoitwa ‘Special Mirathi Account’ katika benki yoyote atakayoona inafaa kwa ajili ya kuhifadhi fedha za marehemu zitakazotoka katika taasisi nyingine za fedha, ikiwemo mabenki.

Jaji Mfawidhi alisema kuwa maoni ya Wadau hao ni muhimu kwa sababu yatasaidia kuweka utaratibu ambao ni sahihi ili mnufaika asiweze kupata changamoto yoyote na pia itasaidia kuondoa tofauti kati ya Taasisi moja na nyingine au benki moja na nyingine wakati wa utekelezaji wa marekebisho ya kanuni hizo.

‘Leo hii Mwenyezi Mungu ametujalia tupo hai, lakini hatuwezi kujua kesho tutakuwa hatupo. Kwa hiyo, tukiweka mifumo thabiti itatusaidia. Tukiondoka lazima tutaacha mali na moja ya mali ni fedha kwenye akaunti zetu ndani ya mabenki mbambali. Jambo la kujiuliza ni kwamba usimamizi wa hizo fedha utakuwaje ili wanufaika wazipate,’ alisema.

Alibainisha kuwa hapo awali mtu akifariki na kuteuliwa Msimamizi wa Mirathi, Msajili wa Mahakama Kuu au Hakimu Mfawidhi katika Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mwanzo walikuwa wanaandika barua kuomba kufunga akaunti na fedha katika mabenki kuhamishwa kwenda katika akaunti ya Mahakama.

‘Lakini, kutokana na mabadiliko ya Kanuni za Mirathi, kupitia Tangazo la Serikali Na 429 la 2025, kwa sasa fedha hizo zitakuwa hazipelekwi tena katika akaunti hiyo ya Mahakama. Msimamizi wa Mirathi anatakiwa kufungua akaunti moja maalum ya mirathi itakayopokea fedha toka taasisi nyingine kama mabenki mbalimbali, hata kama marehemu atakuwa na akaunti zaidi ya moja kwenye benki tofauti,’ Mhe. Mnyukwa alisema.

Jaji Mfawidhi aliwaeleza Wadau hao kuwa walikuwa wanakutana na changamoto nyingi wakati wa kuendesha akaunti moja ya Judiciary Mirathi Account, ikiwemo kutokujua mapema fedha zilizoingizwa zinatoka kwa marehemu yupi.

‘Ukimwandikia barua Msimamizi wa Mirathi kufunga akaunti ya fedha za marehemu kwenye mabenki, fedha zinaweza kuingia kwenye akaunti yetu, lakini kwa haraka tunaweza tusigundue ni za marehemu yupi...

‘Mkumbuke tunahudumia wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam, tuna Mahakama za Mwanzo, Mahakama za Wilaya na Mahakama Kuu na kwa siku moja zinaweza kutoka amri zaidi ya kumi na fedha zinaingia kwenye kapu moja,’ Mhe. Mnyukwa aliwaeleza Wadau hao.

Wakati wa majadiliano hayo, Kituo Jumuishi kilijadiliana na Wadau kwa kina ili kupata uelewa wa pamoja wa namna ya ufunguaji wa akaunti husika kwa kila marehemu anaefunguliwa maombi ya mirathi, usalama wa fedha za mirathi hiyo na namna ya kukabiliana na changamoto zinazoweza jitokeza katika utaratibu huo mpya.

Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa [juu na chini] akizungumza wakati anafungua majadiliano na Wawakilishi wa Mabenki Mkoa wa Dar es Salaam kujadili na kupata uelewa wa pamoja kuhusu marekebisho ya kanuni kwa Msimamizi wa Mirathi kufungua akaunti moja ya kuhifadhi fedha za marehemu wakati wa usikilizaji wa mashauri ya mirathi.


Wawakilishi wa Mabenki Mkoa wa Dar es Salaam [juu na chini] wakimsikiliza Jaji Mfawidhi wa Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia Temeke, Mhe. Mwanabaraka Mnyukwa wakati wa majadiliano hayo.


Picha na Bakari Mtaullah-Dar es Salaam

MAHAKAMA YA RUFANI YAHITIMISHA KIKAO CHAKE JIJINI MBEYA

Na Daniel Sichula – Mahakama, Mbeya

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Barkel Sahel ahitimisha vikao vya usikilizaji wa mashauri ya rufaani kwa mafanikio mashauri yaliyokuwa yakiendeshwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

Akisoma taarifa ya vikao hivyo Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Charles Magesa alisema kwamba mashauri 24 ya rufaa kati ya 25 yaliyopangwa kusikilizwa yalisikizwa na moja lilihairishwa kwa sababu zilizokua nje ya uwezo wa Mahakama hiyo, katika mashauri 24 yaliyosikilizwa mashauri 22 yametolewa maamuzi na mashauri 2 yanasubiri kutolewa maamuzi.

Mhe. Magesa ameongeza kuwa mafanikio waliyofikiwa ni sawa na asilimia 96 ya mashauri yote yaliyosikilizwa na asilimia 91 ni kwa mashauri 22 yaliyotolewa maamuzi.

Aidha, katika taarifa hiyo iliyotolewa iliainisha changomoto zilizojitokeza katika usikilizaji wa mashauri ya rufani kuwa ni pamoja sababu za rufaa kujirudia rudia na zingine kuchelewa kuwasilishwa.

Kwa upande wa Mashataka changamoto iliyojitokeza ni kushindwa kuleta mashahidi mahakamani hasa kwenye mashauri ya ubakaji na ulawiti kama vile Askari Polisi na Madaktari.

“Watu wa Mashtaka nawasisitiza kuwafikisha mashahidi mahakamani wakati wa usikilizaji wa mashauri ya rufani ili haki iweze kutendeka.” alisema Mhe. Sahel

Mhe. Sahel aliwashukuru wadaawa wote kwa kuweza kufika mahakamani kwa wakati na kwa ushirikiano walioutoa mpaka kufikia mafanikio na malengo ya usikilizaji wa mashauri kwa kiwango cha asilimia 96.

Wajumbe waliohudhuria kikao waliwapongeza Majaji wa Rufani kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kusikiliza mashauri hayo yaliyokuwa yamepangwa kusikiliza katika Jopo hilo.

“Waheshimiwa Majaji tunawapongeza sana kwa kazi mliyoifanya, tunaahidi changamoto zote zilizojitokeza tutazifanyia kazi na kuahidi kutojirudia tena kwa vikao vijavyo,” alisema mshiriki kutoka Ofisi ya Mashtaka.

Vilevile, katika kakio hicho kilihudhuriwa na Jaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa, Majaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Musa Pomo,

Wengine walioshiriki kikao hicho ni Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu, Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Bi.Mavis Miti, Mahakimu Mkoa wa Mbeya na Songwe, Mawakili wa Serikali na Wakujitegemea, Afisa Magereza, Askari Polisi pamoja na wawikilishi kutoka ofisi ya Waendesha Mashtaka wa Serikali.

Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Barkel Sahel (katikati) akiendesha kikao cha tathmini ya uendeshaji mashauri ya Rufani kilichoketi Mahakama Kuu jijini Mbeya 

Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufani Tanzania Mhe. Charles Magesa akitoa taarifa ya tathmini ya uendeshaji mashauri hayo.


Sehemu ya wajumbe walioshiriki katika kikao hicho cha mashauri yaliyokuwa yakiendeshwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.



Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa (kushoto), Majaji wa Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Musa Pomo (katikati) na Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu wakifuatilia kikao hicho. 


Sehemu ya wajumbe walioshiriki katika kikao hicho cha mashauri yaliyokuwa yakiendeshwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.

          

Jumatano, 6 Agosti 2025

MAFUNZO YA UTAFITI WA KISHERIA YATOLEWA KWA MAJAJI NA MAHAKIMU

Na. Yusufu Ahmedi - IJA

Katika kuimarisha utafiti wa kisheria na kuwezesha utoaji bora wa maamuzi ya Kimahakama, Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa kushirikiana na Taasisi ya Laws.Africa, AfricaLII na Shirika la Kimataifa la Ushirikiano la Ujerumani (GIZ) zimeendesha mafunzo ya wakufunzi (Training of the Trainers) ya utafiti wa kisheria kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Naibu Wasajili na Mahakimu Wakazi.

Mafunzo hayo yamefunguliwa na Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo Agosti 04, 2025 na yanafanyika katika Hoteli ya Four Points jijini Dar es Salaam.

Lengo kuu ni kuboresha uwezo wa washiriki katika utafiti wa kisheria na kuwaandaa kuwa wakufunzi kwa wenzao.

Katika hotuba yake, Mhe. Dkt. Kihwelo amesema kuwa utafiti wa kisheria ni nyenzo muhimu katika utoaji wa maamuzi ya Kimahakama nani nguzo katika utawala wa sheria.

Pia aliongeza kuwa maamuzi yanayotolewa ni muhimu yakajengwa katika utafiti wa kina, na kwamba uamuzi mzuri ni ule uliyofanyiwa utafiti.

“Maamuzi yetu lazima yajengwe juu ya utafiti wa kina, na usiobebwa na hisia za upendeleo. Uamuzi uliofanyiwa utafiti mzuri na kuandikwa kwa weledi hujenga uaminifu kwa umma, imani ni muhimu pia kwa Mahakama,” alisisitiza.

Pia alibainisha kuwa utafiti wa kisheria hauishii tu katika kutafuta kesi au sheria, bali unahusisha uchambuzi yakinifu wa vyanzo vya sheria na matumizi sahihi katika mazingira husika ili kutoa maamuzi yenye msingi thabiti.

Aidha alitoa shukrani zake za dhati kwa Taasisi ya Kimataifa ya Laws.Africa, AfricaLII kwa kushiriki kuandaa mafunzo pamoja na Shirika la Kimataifa la Ushirikiano la Ujerumani (GIZ) kwa ufadhili wa mafunzo hayo.

Hafla hiyo pia ilihudhuriwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Biashara Mhe. Dkt. Mwajuma Kadilu ambaye pia ni mwezeshaji wa mafunzo hayo, pamoja na wawakilishi kutoka GIZ Tanzania akiwemo Bw. Muhamet Brahimi, Meneja Mradi wa Ukuzaji wa Utawala wa Sheria na Mahakama Barani Afrika (ProLA).

Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akihutubia katika mafunzo hayo.

Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo (katikati) akiwa na Majaji wa Mahakama Kuu katika ya mafunzo ya wakufunzi (Training of the Trainers) ya utafiti wa kisheria. Kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tabora Mhe. Dkt. Adam Mambi na kulia ni  Bw. Muhamet Brahimi, Meneja Mradi wa Ukuzaji wa Utawala wa Sheria na Mahakama Barani Afrika (ProLA).




Washiriki wakiwa katika mafunzo hayo

Washiriki wakiwa katika mafunzo hayo



IJA, MAHKAMA ZANZIBAR ZASAINI MAKUBALIANO YA KUWAJENGEA UWEZO MAAFISA MAHAKAMA NA WATUMISHI

Na Yusufu Ahmadi- IJA

Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) na Mahkama ya Zanzibar zimesaini Hati ya Makubaliano  (MoU) ikiwa ni hatua muhimu katika kuimarisha ufanisi na uwezo wa Maafisa wa Mahakama na maafisa wengine wakiwemo Makadhi kupitia mafunzo, utafiti na uendelezaji wa uwezo wa kitaasisi.

Makubaliano hayo yamesainiwa leo tarehe 5 Agosti 2025 Chuoni Lushoto baina ya Maafisa wa Chuo na wa Mahkama ya Zanzibar na kushuhudiwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla pamoja na Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo.

Miongoni mwa maeneo ya makubaliano hayo ni kutoa mafunzo kwa maafisa wa Mahkama na wengineo wa Mahkama ya  Zanzibar,  kuandaa na kutoa mafunzo ya uongozi na usimamizi, na kukuza uwezo wa utafiti wa kisheria na uvumbuzi katika utendaji wa Mahakama.

Maeneo mengine ni kutoa mafunzo endelevu ya Kimahakama, mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa watendaji wa Mahkama ya Zanzibar pamoja na kuandaa kwa pamoja warsha, makongamano, semina na mikutano ya kitaaluma.

Akizungumzia utiaji saini huo Mhe. Dkt. Kihwelo amesema kuwa Chuo kitahakikisha makubaliano hayo yanafikia malengo yake kwa kutoa mafunzo kwa makundi yaliyokusudiwa katika makubaliano hayo.

Pia ameongeza: “Makubaliano haya ni sehemu ya Chuo kuimarisha upatikanaji wa haki kwa kuwajengea uwezo maafisa wenzetu wa Mahkama na makundi mengine na hivyo kuimarisha ufanisi wa utendaji.”

Kwa upande wake, Mhe. Abdalla ameelezea imani yake kuwa makubaliano haya yatazaa matunda.

“Ni matarajio yangu na Mahkama ya Zanzibar kwamba mashirikiano haya yatazaa matunda kwa maslahi ya Mahkama, Chuo na Tanzania kwa ujumla,” amesema Mhe. Abdalla.

Pia ameongeza kuwa IJA na Mahkama ya Zanzibar vimekuwa na ushirikiano kwa miaka mingi na kwamba makubaliano haya ni sehemu ya kurasimisha ushirikiano huo uliyodumu kwa muda mrefu.

Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee amebainisha kuwa walifanya tathminii ili kujua ni maeneo gani ya mafunzo wao hawako vizuri, na hivyo kuamua kuingia makubaliano na IJA ili kuwezesha maeneo hayo.

Makubaliano hayo yameshuhudiwa na wajumbe wengine wa Mahkama ya Zanzibar na Wajumbe wa Menejimenti ya Chuo.

 Wajumbe wa IJA wakiwa katika hafla hiyo ya utiaji saini.

 

Maafisa wa IJA na wa Mahkama ya Zanzibar wakisaini hati za makubaliano

Mkuu wa Chuo Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo akizungumza katika hafla hiyo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee akisema jambo.


Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla akizungumza katika hafla hiyo

Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa  Menejimenti ya IJA.

Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Mahkama ya Zanzibar wakati wa hafla ya kusaini Hati ya Makubaliano (MoU) baina ya IJA na Mahkama hiyo ya Zanzibar. Kushoto ni  Mkuu wa Chuo Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) ambaye pia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani Mhe. Dkt. Paul F. Kihwelo na kulia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mafunzo ya Mahkama ya Zanzibar ambaye pia ni Jaji wa Mahkama Kuu Zanzibar, Mhe. Khadija Shamte Mzee.


Ijumaa, 1 Agosti 2025

KAMILISHENI KWA WAKATI MASHAURI YA KIKATIBA YANAYOHUSIANA NA UCHAGUZI; JAJI MKUU

  • Asisitiza pia uadilifu, ubunifu, umahiri katika kazi, kujiongeza, kuweka mbele maslahi ya Taifa kwa manufaa ya umma

 Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju amewataka Majaji na Mahakimu nchini kumaliza kwa wakati mashauri yote ya kikatiba yaliyopo mahakamani yanayohusiana na mchakato wa uchaguzi ili kuleta imani kwa umma dhidi ya Mahakama pamoja na kutoa fursa kwa watu waliofungua mashauri hayo kuwa na uhakika na kinachoendelea kuhusu mchakato wa uchaguzi. 

Mhe. Masaju alitoa rai hiyo jana tarehe 31 Julai, 2025 jijini Dodoma wakati akitoa salamu kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania waliokuwa wakishiriki katika Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court).

“Sote tunajua tutakuwa na Uchaguzi Mkuu mwezi wa 10 mwaka huu, lakini hapa katikati tunafahamu kuwa, kuna watu wamefungua kesi mahakamani zinazohusiana na hizo sheria za uchaguzi na mchakato wa uchaguzi kwa ujumla, ushauri wangu ni kwamba hizi kesi tuzimalize mapema ili kutoa fursa watu kuwa na uhakika na kinachoendelea kuwa na (certainty of electoral process) na kama kuna sababu yoyote ya kuchelewesha iwe ni sababu ya msingi ya kufanya hivyo,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju amesema kuwa, suala la kutochelewesha haki ni takwa la kikatiba kwa Mahakama na ni kwa mujibu wa Ibara ya 107A (2) na Dira ya Mahakama ya Tanzania nayo inahimiza kutoa haki inayopatikana kwa wote mapema ipasavyo.

Jaji Mkuu alisema kuwa, wananchi wana imani kubwa na Mahakama katika kutafsiri sheria na kutoa haki hivyo ni muhimu kusikiliza mashauri hayo na mashauri mengine yaliyopo mahakamani mapema iwezekanavyo ili kuendeleza imani ambayo wananchi wanayo juu ya Mahakama.

Aidha, Jaji Mkuu aliwakumbusha Majaji, Mahakimu, Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea kurejea hotuba yake aliyowasilisha tarehe 03 Julai, 2025 jijini Dodoma wakati wa Sherehe za Kuwakubali Mawakili wapya ambapo pamoja na mambo mengine aliwataka kuendelea kuzisoma Sheria za Uchaguzi na kuzifahamu ipasavyo ili ziweze kuwasaidia wakati wa mchakato wa uchaguzi na uendeshaji wa mashauri ya uchaguzi.

Alizitaja Sheria hizo kuwa ni pamoja na Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Madiwani na Wabunge, Sheria ya Vyama vya Siasa, Sheria ya Polisi na sheria zote zinazosimamia mchakato mzima wa uchaguzi.

Akizungumzia kuhusu Mafunzo ya Siku moja ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Masaju alimpongeza Jaji Kiongozi, Watoa Mada, Waratibu na Kamati ya Jaji Mkuu ya Mafunzo kwa ubunifu wa kuandaa mafunzo hayo na kuwataka Majaji hao kuuliza, kuchangia na kutoa ushauri ili kuwa na uelewa wa pamoja katika ushughulikiaji wa mashauri ya uchaguzi.

Kadhalika, Jaji Mkuu amesema pia, kuwa ni muhimu kwa Majaji na watumishi wote wa Mahakama nchini kuzingatia mambo muhimu katika utumishi wa umma na utawala wa sheria ambayo ni pamoja na umakini katika masuala yanayohusu haki kwa kuhakikisha kuwa haki inasimamiwa ipasavyo, kuwa na uadilifu, umahiri katika kazi, ubunifu, kujiongeza katika kazi na kuweka mbele maslahi ya Taifa ambayo pia ni maslahi ya umma.

“Kuna vitu ambavyo ningependa kuwashirikisha, vinavyohusu utumishi wetu wa kila siku hapa mahakamani na hivi inabidi tuviongeze kwenye Tunu zetu za Mahakama, kama mnavyofahamu sisi wajibu wetu ni kutenda haki na katika Mihimili mitatu ya Dola ambayo ni Serikali, Bunge na Mahakama, Mahakama ndio yenye kauli ya mwisho kwenye kutoa haki, hivyo sisi tuliopewa jukumu hili tuna wajibu mkubwa wa kusimamia uadilifu, ubunifu, umahiri katika kazi, kujiongeza katika kazi na kuweka mbele maslahi ya Taifa kwa manufaa ya umma,” alisisitiza Mhe. Masaju.

Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Jaji Kiongozi na Majaji wote wa Mahakama Kuu, Jaji wa Mahakama Kuu-Kituo Jumuishi cha Masuala ya Familia- Temeke, Mhe. Sarah Mwaipopo alimshukuru Jaji Mkuu kwa maneno ya hekima aliyowapatia na kumuahidi kwamba watayazingatia na kumpatia ushirikiano utakaowezesha kutekeleza ipasavyo jukumu la utoaji haki kwa wananchi.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju.




 

 

 

 

 

 

 

 

MAHAKIMU MAHAKAMA ZA MWANZO UBUNGO, KINONDONI WAKUMBUSHWA UTEKELEZAJI MAELEKEZO YA JAJI MKUU

Na EUNICE LUGIANA, Mahakama-Dar es Salaam

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni/Kinondoni-Dar es Salaam, Mhe. Is-haq Kuppa amewakumbusha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo za Wilaya ya Kinondoni na Ubungo kutekeleza maelekezo ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. George Mcheche Masaju juu ya watuhumiwa Mahakama za Mwanzo kudhaminiwa kwa masharti rahisi.  

Mhe. Kuppa aliyasema hayo jana tarehe 31 Julai, 2025 wakati wa  ufunguzi wa kikao kazi kilichojumuisha Mahakimu wa Mahakama hizo kilichofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni.

Mahakimu hao walikumbushwa pia, kwa Mahakama za Mwanzo ambazo makosa pamoja na adhabu zake kwa kuwa ni ndogo, zisizokuwa na taratibu ngumu za kisheria katika kushughulika nayo hawapaswi kuwa na uwepo wa Mahabusu kama miongozo mbalimbali kama vile muongozo wa kushugulikia dhamana (Bail Guideline) unavyoongoza.   

Aidha, Mfawidhi hyo aliendelea kusema kwamba, sambamba na hilo shauri linapofika siku ya kwanza mahakamani halipaswi kuahirishwa kwa kuwa wahusika wote yaani mlalamikaji na mshtakiwa huwepo.

Likifanyika hili litasaidia pia kutochelewesha mashauri na yatamalizika mapema na kwa wakati hivyo kupelekea dhana ya utoaji haki kwa wakati itimie, alisisitiza Mhe. Kuppa.

Pamoja na maelekezo hayo, ulitolewa mwongozo wa kutumia Mfumo wa Ki-elektroniki wa Upimaji wa Wazi Utendaji Kazi wa Maafisa wa Mahakama (e-JOPRAS), Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo wakiwa kama sehemu ya Maafisa hao walijulishwa kwamba kwa kuwa wanapimwa moja kwa moja na Mahakimu Wafawidhi wa Wilaya zao wanapaswa kutekeleza ujazaji wake mara tu wanapopimwa na viongozi wao.

Ilisisitizwa kwamba,  mfumo huo ni  wa wazi na wanapaswa kuwajibika kwa mujibu wa vipengele vilivyowekwa kama vile uadilifu, ubunifu na kutojihusisha na vitendo vya ukiukwaji wa maadili kama vile rushwa na kadhalika kwa kuwa watakuwa wanapimwa na kupewa alama ambazo zitakuwa za wazi na stahiki na kila mtu atakayepimwa kwa mujibu wa mwenendo wake hivyo ni jukumu la kila mmoja kuwajibika juu ya hilo. 

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Mhe. Jacqueline Rugemarila aliwaelekeza wahusika kwa vitendo juu ya mfumo wa e-JOPRAS ambapo kila mwenye changamoto alisaidiwa hapohapo kwa msaada wa karibu wa Afisa TEHAMA wa Kituo hicho, Mhandisi Delphina Mwakyusa.

Kikao kazi hicho ni matokeo ya   msisitizo wa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi aliotoa katika kikao cha viongozi Kanda hiyo mapema mwezi Julai mwaka huu ambapo moja ya maazimio yake ni kufanya vikao kazi ili kukumbushana majukumu.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mahakimu Wakazi Wafawidhi wa Mahakama za Wilaya Kinondoni na Ubungo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni/Kinondoni, Mhe. Is-haq Kuppa (aliyesimama) akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo za Wilaya za Kinondoni na Ubungo kilichofanyikia jana 31 Julai, 2025 katika Ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Kinondoni.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Kinondoni, MheJacqueline Rugemarila akiwaelekeza Mahakimu  wa Mahakama za Mwanzo namna ya kujaza taarifa za utendaji kwenye Mfumo wa Ki-elektroniki wa Upimaji wa Wazi Utendaji Kazi wa Maafisa wa Mahakama (e-JOPRAS).

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)





Alhamisi, 31 Julai 2025

MAJAJI MAHAKAMA KUU YA TANZANIA WAJIANDAA KWA UENDESHAJI MASHAURI YA UCHAGUZI

·       Jaji Kiongozi asisitiza uendeshwaji wa mashauri hayo kwa weledi na kukamilika kwa wakati

 Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani ametoa rai kwa Majaji wa Mahakama Kuu nchini kuhakikisha usikilizwaji na uamuzi wa mashauri yote ya uchaguzi unakuwa wa haki, haraka kadri inavyopaswa pamoja na kutojifunga na mbinu za kiufundi.

 Mhe. Dkt. Siyani ametoa rai hiyo leo tarehe 31 Julai, 2025 jijini Dodoma wakati akifungua Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court).

Mhe. Dkt Siyani ametumia fursa hiyo kuwakumbusha Majaji wa Mahakama Kuu juu ya nafasi ya Mahakama katika kuimarisha amani na utulivu wa nchi na hivyo kujenga mazingira ya kukua kwa uchumi. Aidha, Jaji Kiongozi amewataka washiriki wa mafunzo hayo kuhakikisha wanaweka utaratibu madhubuti wa kushughulikia mashauri hayo kwa haraka, haki, na ufanisi mkubwa, ili kudumisha imani ya wananchi kwa chombo hiki muhimu cha utoaji wa haki.

Akisisitiza juu ya umuhimu wa kuamuliwa kwa mashauri ya uchaguzi kwa haraka, Jaji Kiongozi ameeleza kuwa, mchakato wa uchaguzi huendana na uwepo wa mivutano ya kisiasa, hisia kali za jamii, na matarajio makubwa kutoka kwa wadau wa demokrasia, hivyo ni wajibu wa Mahakama kuhakikisha mashauri yatokanayo na migogoro hiyo ya uchaguzi, yanapewa kipaumbele na kusikilizwa kwa wakati.

“Kama ilivyo kwa aina nyingine za mashauri, ni muhimu sana kwa Majaji watakaosikiliza mashauri ya uchaguzi, kuwa waadilifu, wenye weledi wa hali ya juu na kasi katika usikilizaji wa mashauri hayo. Ni kwa kufanya hivyo wananchi watakaochagua viongozi wao kwa kuwapigia kura na viongozi wataochaguliwa kwa kupigiwa kura, wapate fursa ya kuendelea na ujenzi wa nchi.” Ameeleza Dkt. Siyani

Jaji Kiongozi amesema kuwa, mafunzo hayo yanayofanyika wakati ambao Taifa letu linaelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani, yamelenga kuimarisha uwezo na uelewa wa Majaji kuhusu misingi ya kikatiba na kisheria kuhusu mashauri ya uchaguzi nchini na hivyo amewataka washiriki kutumia mafunzo hayo, kujiweka tayari kutimiza wajibu wao kwa ufanisi.

“Matumaini yangu ni kuwa mafunzo haya na mengine yatakayofuatia, yatawawezesha kuwa na viwango vya juu vya weledi, ufanisi na maadili zaidi katika kutimiza majukumu yenu. Muhimu ambalo ningependa kulisisitiza ni kuwa mchakato wa uchaguzi na utatuzi wa migogoro inayotokana na mchakato huo, ni kipimo kwa Mahakama,” amesisitiza Mhe. Dkt. Siyani.

Jumla ya Majaji 103 wa Mahakama Kuu wameshiriki mafunzo hayo ya siku moja kwa njia ya mtandao.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akifungua Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court) leo tarehe 31 Julai, 2025.

Sehemu ya washiriki (Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania) walioshiriki Mafunzo ya Uendeshaji wa Mashauri ya Uchaguzi kwa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania yaliyofanyika kwa njia ya Mahakama Mtandao (Virtual Court) leo tarehe 31 Julai, 2025.

(Picha na INNOCENT KANSHA, Mahakama)


 

Jumatano, 30 Julai 2025

'LAZIMA TUONGEZE UMAKINI KATIKA KUSIMAMIA MAHAKAMA ZETU' ; JAJI MAHIMBALI

Na SETH KAZIMOTO, Mahakama-Arusha

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali amewaelekeza viongozi wa Mahakama ngazi zote Kanda ya Arusha kusimamia ipasavyo vituo vyao vya kazi ili kuhakikisha vituo hivyo vinamaliza mashauri mengi zaidi ya yale yanayosajiliwa.

Mhe. Mahimbali ametoa rai hiyo leo 30 Julai, 2025 katika Kikao cha Menejimenti ya Kanda ya Arusha ambapo amesisitiza kuwa kazi ya msingi ya Mahakama ni usikilizaji wa mashauri, hivyo, ni lazima uhalisia huo ujioneshe katika ufanyaji kazi wa kila siku kwa kuhakikisha kuwa viongozi wanatimiza wajibu wao ipasavyo na hatimaye kuondokana na kutengeneza mashauri ya mlundikano yasiyo na sababu za msingi.

“Kila ngazi ya Mahakama ikae na kutafsiri vizuri takwimu za mashauri zilizowasilishwa hapa na kujiwekea mikakati yao wenyewe kuhakikisha hali ya usikilizaji wa mashauri inakuwa bora na kuepuka kuwa na mashauri ya mlundikano yasiyokuwa na sababu za msingi,” amesema Jaji Mahimbali.

Aidha, Mhe. Mahimbali amewaelekeza pia viongozi katika ngazi zote za Mahakama Kanda ya Arusha kuhakikisha kuwa hawatengenezi malalamiko yanayotokana na wateja kutopewa nakala za hukumu kwa wakati, kuzingatia utunzaji wa majengo ya Mahakama, kuhakikisha hati za umiliki wa maeneo ya Mahakama zinapatikana, viongozi na watumishi kujua mikakati na mipango ya Kitaifa na Mahakama kama vile Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 na mipango mbalimbali ya Mahakama inayoendelea kutekelezwa.

Jaji Mfawidhi huyo amesisitiza pia ushirikiano baina ya viongozi na kuepuka migogoro isiyo na tija kazini pamoja na kuhakikisha kwamba watumishi wote wanafanya kazi kwa uadilifu, weledi na uwajibikaji wa hali ya juu.

Akiwasilisha taarifa ya mashauri, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Elia Mrema amesema kuwa, hali ya usikilizaji wa mashauri inakwenda vizuri na kwamba katika kipindi cha kuanzia mwezi Aprili hadi Julai 29, 2025 Mahakama Kuu Arusha ilipokea jumla ya mashauri 411 na kwamba jumla ya mashauri 756 yalisikilizwa katika kipindi hicho.

Kadhalika, Mhe. Mrema ametoa pia taarifa ya mashauri ya Mahakama za Hakimu Mkazi, Wilaya na Mwanzo kwa pamoja kuwa hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2025 Mahakama hizo zimesikiliza jumla ya mashauri 5,245 na kubakiwa na mashauri 1,541 yanayoendelea kusikilizwa.

Naibu Msajili huyo ametaja changamoto zinazojitokeza wakati wa zoezi zima la ufunguaji wa mashauri ambazo ni baadhi ya wadaawa kukosea dirisha la kufungulia mashauri katika mfumo wa kielektroniki wa mashauri (e-CMS), baadhi ya wadaawa kutofautisha majina wanayoandika katika mfumo wa kielektroniki na yale yanayoonekana kwenye nyaraka ngumu (hardcopy pleadings) wanazowasilisha Mahakamani kwa ajili ya kufungua kesi.

Ametaja changamoto nyingine ni pamoja na wadaawa na Mawakili kufuata namba ya malipo (control number) mahakamani wakati wangepata namba hizo za malipo katika mfumo waliotumia kusajili mashauri yao (e-CMS) na kukiri kuwa hali hiyo imekuwa ikileta usumbufu na kuchukua muda mwingi kwa mtoa huduma mahakamani kuwahudumia.

Naye Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama Kuu Kanda ya Arusha pamoja na mambo mengine, amesema kuwa Mahakama katika Mkoa wa Arusha imeweka mpango wa mafunzo ndani ya Kanda katika mwaka huu wa 2025/2026 kwa lengo la kuwapa maarifa watumishi wa kada zote na hatimaye kuboresha utendaji kazi wa watumishi wa Mahakama.

Sambamba na hilo, Bi. Grace amesema pia kwamba ukarabati wa Mahakama za Mwanzo utaendelea kupewa kipaumbele katika mwaka huu wa fedha hususani katika Mahakama za Mwanzo Arusha Mjini, Mto wa Mbu, Mbuguni na Endabash.

Kikao hicho kimejadili masuala mbalimbali yanayohusu usimamizi wa shughuli za Mahakama katika Kanda ya Arusha na namna ya kuboresha utendaji kazi kwa lengo la kuhakikisha kuwa Kanda hiyo inakuwa mfano bora wa kuigwa katika kutoa huduma bora kwa wananchi na kwa wakati.

Viongozi wa Mahakama wa ngazi mbalimbali mkoani Arusha wamehudhuria kikao hicho na wameaswa kuzingatia taratibu na maadili ya kazi wanapofanya majukumu yao na kuhakikisha kuwa watumishi walio chini yao wanafanya kazi kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Mhe. Frank Mahimbali akifungua kikao cha Menejimenti cha Kanda hiyo leo tarehe 30 Julai, 2025 kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha. Kushoto ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama.

Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Amir Msumi akifafanua jambo wakati wa Kikao cha Menejimenti cha Kanda ya Arusha leo tarehe 30 Julai, 2025 kilichofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa  Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Arusha, Mhe. Elia Mrema (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya mashauri wakati wa Kikao cha Menejimenti cha Kanda ya Arusha kilichofanyika leo tarehe 30 Julai, 2025 katika ukumbi wa Mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Kaimu Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, Bi. Grace Kapama akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za Mahakama wakati wa Kikao cha Menejimenti cha Kanda ya Arusha kilichofanyika leo tarehe 30 Julai, 2025 katika ukumbi wa Mikutano wa  Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

Wajumbe mbalimbali waliohudhuria Kikao cha Menejimenti ya Mahakama Kanda ya Arusha  kilichofanyika leo tarehe 30 Julai, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Arusha.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)

Jumatatu, 28 Julai 2025

WANACHAMA WA TUGHE MAHAKAMA SHINYANGA WATAKIWA KUKUTANA KUJADILI CHANGAMOTO ZAO

  • Watakiwa kushiriki michezo mbalimbali kuimarisha afya

Na EMMANUEL OGUDA, Mahakama-Shinyanga

Watumishi wa Mahakama wanachama wa Chama Cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) Mkoa wa Shinyanga wametakiwa kufanya vikao vya mara kwa mara kwa ajili ya kujadili masuala mbalimbali yanahusu maslahi yao ya kiutumishi.

Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa TUGHE Mahakama ya Tanzania, Bw. Michael Masubo alipokutana na wanachama hao tarehe 25 Julai, 2025 Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga kwa lengo la kujitambulisha na kuwapa elimu kuhusu umuhimu wa kujiunga na chama hicho cha Wafanyakazi.

Akielezea faida za kujiunga na Chama hicho, Bw. Masubo alisema kuwa, moja ya faida za kujiunga na chama hicho kuimarisha mshikamano na umoja miongoni mwa watumishi mahala pa kazi.

Bw. Masubo aliwataka pia wanachama kuipitia Katiba ya Chama hicho kwani kuna mambo mengi yaliyoainishwa ambayo yana faida kubwa kiutumishi ikiwemo uboreshaji wa maslahi ya watumishi wa Mahakama kwa ujumla. 

Kwa upande mwingine, Bw. Masubo alisisitiza juu ya uundwaji wa Kamati za Wanawake ambazo zimekuwa chachu ya kudhibiti mienendo isiyofaa kwa wanachama wanawake mfano mavazi na kuimarisha tabia njema kwa watumishi wanawake.

Aidha, aliwataka Wenyeviti na Makatibu wa Matawi ya TUGHE Mahakama kuhudhuria vikao vya Menejimenti kuelezea changamoto mbalimbali za wanachama wao kwani wao ni wajumbe wa vikao hivyo kwakuwa kushiriki katika vikao hivyo husaidia kupunguza malalamiko na stahiki zao kushughulikiwa kwa wakati. 

Hali kadhalika, Bw. Masubo aliwahamasisha watumishi ambao sio wanachama wa TUGHE Shinyanga kujiunga na Chama hicho kwani kina faida nyingi ikiwemo kutambua maslahi yao na kuyafuatilia kupitia vikao mbalimbali na hatimaye hoja za jumla kupata fursa ya kuwasilishwa katika vikao vya Baraza la Wafanyakazi wa Mahakama Taifa linaloketi kila mwaka.

Katika hatua nyingine, Bw. Masubo aliipongeza Timu ya Mpira wa Miguu ya Mahakama FC (wanaume) ya Kanda ya Shinyanga kwa kuibuka mshindi wa kwanza katika mashindano ya Mei Mosi, 2025 na kujinyakulia zawadi mbalimbali zikiwemo jezi, mipira na tuzo maalum kwa Mshindi. Aliongeza kwa kuwasisitiza watumishi kushiriki katika michezo mbalimbali na kufanya mazoezi kuimarisha afya pamoja na kukabiliana na magonjwa yasiyoambukizwa kama vile Shinikizo la Damu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, watumishi wa Mahakama ambao pia ni wananchama wa TUGHE Shinyanga walisema kuwa, wamefarijika kupata elimu na kufahamu faida za kujiunga na chama hicho. Waliwasilisha maoni mbalimbali kwa Katibu huyo, kuhusu uimarishwaji wa Matawi ya TUGHE katika ngazi za Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya.

Katibu Mkuu wa Chama Cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) Mahakama ya Tanzania, Bw. Michael Masubo akihamasisha watumishi wa Mahakama Shinyanga kujiunga na Chama hicho.

Msaidizi wa Kumbukumbu Mahakama Kuu ya Tanzania, Bi. Editha Haule akichangia jambo wakati wa kikao hicho.

Sehemu ya Watumishi na wananchama wa TUGHE Shinyanga wakimsikiliza kwa makini Katibu Mkuu wa TUGHE Mahakama ya Tanzania (hayupo katika picha) wakati alipokutana na watumishi wa Mahakama Shinyanga.

Katibu Mkuu wa TUGHE Mahakama ya Tanzania, Bw. Michael Masubo (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na watumishi na Wanachama wa TUGHE Shinyanga wakati alipowatembelea wanachama hao tarehe 25 Julai, 2025.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma)