·
Aitisha Kikao cha Wadau kueleza
mikakati ya Mahakama na kuweka mikakati ya pamoja
·
Asema hatua hiyo ni moja ya mikakati
ya kufikia Dira ya Mahakama sanjari na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050
·
Asema mashauri hayo yana mchango
mkubwa katika ukuaji wa Uchumi wa Nchi
·
Awasihi Wadau wa Haki Madai kutoa
ushirikiano na kila mmoja kutekeleza wajibu wake ipasavyo
·
Wadau wakiwemo Tume ya Mipango, Benki
Kuu, Mwanasheria waipongeza Mahakama kwa hatua hiyo
Na
MARY GWERA, Mahakama-Dodoma
Jaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Majaji na Mahakimu nchini kukamilisha
mashauri yote ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Ardhi
ifikapo tarehe 15 Desemba, 2025, huku akiwataka wadau wote wa haki madai kutoa
ushirikiano wa dhati kwa kila mmoja kuwajibika ipasavyo ili kufanikisha utekelezaji
wa Dira ya Mahakama ya Utoaji Haki Sawa mapema ipasavyo ili kuchangia kukuza uchumi
wa nchi na kuvutia mazingira ya uwekezaji.
Akizungumza jana tarehe
08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama
ya Tanzania jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati
na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya
Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi, Mhe. Masaju
alisema mkakati huo unaenda sambasamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya
Maendeleo 2050 katika eneo la kuboresha utoaji haki.
“Sisi Mahakama ni wadau
muhimu katika hili eneo ambalo linagusa uchumi na tumejipanga, Mahakama
tunatambua wajibu wetu kwenye utatuzi wa migogoro, ndio maana tumeitisha kikao
hiki ili kuwashirikisha mikakati tunayochukua sisi na hatua tunazozichukua
kuhakikisha kwamba mashauri haya ambayo yapo mahakamani yanaamuliwa mapema ipasavyo
ili watu waendelee na shughuli zao, fedha ambazo zimefungiwa huku ziweze
kufunguliwa ziingie kwenye mzunguko wa uchumi ili ziweze kuwanufaisha
Watanzania,” alisema Jaji Mkuu.
Mhe. Masaju alieleza
kuwa, azma hiyo itafanikiwa endapo Mahakama itapata ushirikiano wa wadaawa
wanaokuja mahakamani ambapo alisema, “tunataka
kama vile ambavyo Mahakama imejitoa hata kwa rasilimali kidogo sana na wakati
fulani kulazimika kuchukua hela fulani kwenye matumizi fulani kuzileta huku,
lakini ukweli ni kwamba sisi haya tunafanya kwa nia njema na hii ikifanikiwa
itatusaidia sana kwenda mbele, hivyo tumejipanga tunataka twende, hatutaki
kukwamishwa na mtu.”
Kadhalika, Jaji Mkuu alisema
kwamba, pamoja na kuwashirikisha Wadau hao kuhusu mikakati ya Mahakama ya
kushughulikia migogoro yote na kuimaliza mapema ipasavyo amewaeleza kuwa na
Dira ya Mahakama isemayo; ‘Haki sawa kwa wote mapema ipasavyo’ nayo inataka
kutoa haki mapema ipasavyo, lakini katika kutekeleza Dira hiyo, Mahakama
inajifungamanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo, hivyo ni muhimu kwa Wadau
kushirikiana ili kwa pamoja kufanikisha Dira hizo.
Mhe. Masaju aliongeza
kuwa, katika jitihada za kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi kwa
karibu zaidi, Mahakama imepanga kushusha huduma za Mahakama ya Rufani katika
Kanda na kwa kuanzia itakuwa katika Mikoa ya Dar es Salaam na Mikoa mingine
yenye mashauri mengi.
“Kwahiyo sasa katika
kuwashirikisha hii mikakati yetu tutapata fursa na pengine na ninyi kujua
kinachoendelea hapa, mtatusaidia na ninyi kuboresha wapi ambapo hatufanyi
vizuri, muwe huru mseme ndio maana ya mkutano, muwe huru labda mtusaidie hata
kuboresha mikakati yetu, lakini pia pale ambapo hatufanyi vizuri mtueleze kwa
sababu kufanikiwa kwa Taasisi moja kwenye suala hili ambalo ni mtambuka Taasisi
nyingine zikiwa hazikufanikiwa hatutakuwa tumepiga hatua. Kwa hiyo tumewaita
ili tushirikishane, tusemane hapa kwa nia njema ya kwenda mbele, tumewaita wote
hapa mkiwa wote ni wahusika wakuu kwa mfano tumewaita watu wa TLS, Mabenki,
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Gavana wa Benki Kuu na wadau wengine,” amesisitiza Mhe. Masaju.
Jaji Mkuu alisema kwamba,
kupitia mkutano huo watapata fursa ya kuambiana madhaifu ya kila Taasisi lengo
likiwa ni kwenda mbele. Ameeleza kuwa, “sisi wakati tunaweka hii mikakati ya
kutekeleza wajibu wetu wa kutoa haki sawa mapema ipasavyo na ninyi sasa ambao
ni wadau wetu mtusaidie namna gani mtaungana na sisi katika kulifanikisha hili
ili wote twende pamoja.”
“Kwa ujumla mapinduzi
makubwa yanahitajika katika kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji
nchini hususani katika kubadilisha Sekta ya Umma kutoka kuwa mdhibiti kwenda
kuwa Mwezeshaji wa biashara na uwekezaji na katika hii ya mwisho ndio na sisi
pia tunaingia pale na Mahakama ina mchango mkubwa kwenye hili suala,”
amesisitiza Mhe. Masaju.
Mhe. Masaju aliishukuru
Wizara ya Fedha kwa kuendelea kutambua umuhimu wa Mahakama na kuiwezesha
kufanya kazi zake vizuri, huku akiwataka wadau wengine kama Umoja wa Mabenki
Tanzania (TBS), Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama na wadau wengine
kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu bila kuzalisha migogoro.
Aidha, Mhe. Masaju alisema,
mashauri hayo ni eneo ambalo linagusa masuala ya uwekezaji na biashara, “Na
mimi ninachoweza kusema ni kwamba tumeanza utekelezaji wa Dira mpya ya Taifa ya
Maendeleo 2050 na Dira hii mnafahamu ina msingi mkuu ambao msingi mkuu unahusu
Utawala, Amani, Usalama na Utulivu lakini na vipaumbele vyake ambavyo viko
vinne, cha kwanza kabisa ni Utawala Bora na Haki, halafu cha pili Serikali
imara za Mitaa na Ufanisi lakini kipengele cha tatu ni Uwajibikaji utumishi wa
Umma lakini kipengele cha nne ni Amani, Usalama, Utulivu hivyo ndio vipaumbele
vya msingi mkuu wa Dira.”
Aidha, Jaji Mkuu alieleza kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imebeba nguzo tatu ambapo nguzo ya kwanza inahusu uchumi imara, jumuishi na shindani.
“Na mkiangalia haya mashauri ambayo sisi tumewashirikisha, mkakati ambao tunachukua yana mchango mkubwa sana katika Uchumi na unaposoma ukurasa 21 wa Dira hiyo inasema Uchumi imara, jumuishi na shindani ni moja ya nguzo kuu ya kujenga Taifa lenye ustawi kwani nguzo hii inafungua fursa za kiuchumi na hivyo kuweka mazingira ya kupunguza umaskini na kuboresha hali ya maisha ya wananchi wote, Uchumi imara utahakikisha kwamba maendeleo ya kiuchumi yanakua na taswira chanya kwa jamii na kuwanufaisha wananchi wote,” amesema Mhe. Masaju.
Jaji Mkuu amesema katika moja ya vipengele vya nguzo hii ya Uchumi imara ni mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji ambapo ukurasa wa 25 wa Dira; ‘Uchumi imara na endelevu unategemea kuwepo kwa mazingira mazuri ya kufanya biashara.’
Aidha, aliongeza kwamba, mwaka 2018, Tanzania ilizindua Mpango Mkakati wa Mageuzi ya Sheria ya kuboresha mazingira ya biashara nchini ambao ulilenga kuimarisha ufanisi katika mifumo ya kisheria, kurahisisha michakato ya usajili na usimamizi wa biashara na kuongeza uwazi na uwajibikaji ambapo vipengele vikuu ilikuwa ni kupitia upya sheria na kanuni, kupunguza kodi na ada zisizo na ufanisi na kuboresha uwezo wa Taasisi za kudhibiti ili kuzifanya zijielekeze zaidi katika kuchangia ukuaji wa Sekta ya Biashara badala ya kuweka mkazo katika makusanyo ya mapato pekee.
“Pamoja na juhudi hizo, changamoto mbalimbali zimeendelea kuyagubika mazingira ya biashara nchini ikiwemo gharama na muda mkubwa wa usajili na ukosefu wa mitaji, kikwazo kingine ni urasimu katika utendaji jambo linaloongeza muda ambao Wawekezaji wanachukua kukamilisha taratibu za awali za kuidhinisha biashara na uwekezaji,” amesema Mhe. Masaju.
Aidha, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, uendeshaji wa biashara umeendelea kuwa na uthibiti uliokithiri ukiathiri utaratibu wa kodi na mapato kwa bidhaa zenye thamani kubwa, migongano ya Sera, Sheria na Kanuni na kuwepo kwa miingiliano ya majukumu ya Taasisi za Udhibiti, ambapo ameeleza kuwa, “suala hili limezifanya biashara kubeba mzigo mkubwa wa kodi, ada na ongezeko la gharama kutokana na masharti mengi ya leseni na vibali.”
Ameongeza kwamba, ili kushughulikia changamoto hizo ni lazima kujenga mazingira wezeshi ya kibiashara yatakayochochea ukuaji wa Uchumi na kuvutia uwekezaji na kwamba mageuzi hayo yanapaswa kurahisisha taratibu, kupunguza vikwazo vya kisheria, kuondoa tozo zisizo na tija na kufungamanisha Sera na Taasisi ili kuimarisha mazingira ya biashara yenye ushindani na ufanisi.
Kadhalika, Jaji Mkuu pia alisisitiza suala la uwajibikaji na
uadilifu kwa Mahakama na wadau wote wa Haki Madai kuwajibika na kujituma
ipasavyo, na kuweka wazi kuwa suala la kuwajibika ni suala la kikatiba hivyo
kila mmoja anapaswa kuwajibika huku akitimiza malengo yake binafsi na yale ya
pamoja.
"Kwetu sisi wenyewe huku Mahakamani tumekuwa na
mafunzo na tunawajibishana, sasa na ninyi, wakati Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050
inazungumza juu ya uwajibikaji kwa watumishi wa umma, hili suala ni la
kikatiba, Ibara ya 25 ibara ndogo ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania inasema hivi, 'kazi pekee ndio uzao tajiri wa mali katika jamii
ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha utu na kila mtu ana wajibu
wa (a) kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji
mali na (b) kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya
uzalishaji mali ya binafsi na yale malengo ya pamoja yanayotakiwa au
yaliyowekwa na sheria.'
Kupitia Mkutano huo Wadau
hao wa Haki Madai walipata fursa ya kujadiliana masuala mbalimbali ikiwa ni
pamoja na changamoto zilizopo na kuweka mikakati thabiti ya kuondokana na
changamoto hizo na hatimaye kuweza kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Wadau mbalimbali
waliohudhuria katika Mkutano huo ambao ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe.
Hamza Johari, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, Mahakama
Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA), Msajili wa Hazina, Tume ya Taifa ya Mipango, Baraza la
Ushindani, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Wizara ya
Fedha, Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA), Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo maalum
ya Kiuchumi (TISEZA), NBC, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Baraza la
Rufani za Kodi, Chama cha Madalali Tanzania, na Wasambaza Nyaraka za Mahakama.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) kufungua Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Ushindani (FCT) akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba. 
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba (kushoto) akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari.
Wadau mbalimbali wa Mkutano huo wakichangia majadiliano
Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba akichangia jambo wakati wa mkutano huo.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya wadau waliohudhuria katika Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Imani Aboud na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo.