Ijumaa, 10 Oktoba 2025

JAJI DINGO’HI AFANYA ZIARA YA UKAGUZI MKOANI LINDI


  • ·Apongeza kasi ya uondashaji wa Mashauri Mahakamani
  • ·Awaasa watendaji kukaza buti kwenye matumizi ya TEHAMA
  • ·Asisitiza kufanya kazi kwa uadilifu

Na. Hilary Lorry – Mahakama, Lindi

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara, Mhe. Saidi Dingo’hi amefanya ziara ya ukaguzi katika Mkoa wa Lindi na kukagua Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi, Mahakama za Wilaya tano (5) za Mkoa wa Lindi, Mahakama ya Wilaya ya Lindi, Kilwa, Liwale, Ruangwa, Nachingwea na Mahakama za mwanzo zilizopo katika Mkoa huo.

Akizungumza na watumishi wa Mahakama kwa nyakati tofauti wakati wa ziara hiyo Mhe. Dingo’hi alisema nimeshuhudia kazi nzuri mnayofanya alipokuwa akikagua Mahakama za Wilaya hizo na kuwakumbusha watumishi kufanya kazi kwa bidii na kwa uadilifu wa hali ya juu.

Aidha, Mhe. Dingo’hi aliwapongeza watumishi katika mkoa huo kwa kuchukua jitihada za makusudi  katika ufanyaji wa  kazi kwa bidii hasa Mahakimu kwa  kusikiliza mashauri kwa wakati  bila kuzalisha mashauri ya muda mrefu (mashauri ya Mlundikano)  na kutokuwa na mashauri mengi yanayoendelea mahakamani (pending cases) hiyo ni kutokana na kasi ya usikilizaji na umalizaji wa mashauri kwa wakati.

“Nawapongeza Mahakimu wote  kwa kutekeleza jukumu lenu la  msingi la usikilizaji na uondoshaji wa Mashauri kwa wakati lakini pia niwatake mtekeleze jukumu hilo kwa uadilifu ili haki isionekene tu bali ionekane ikitendeka hii itarejesha imani ya jamii kwa Mahakama” alisisitiza Jaji Dingo’hi.

Aidha, Mhe. Dingo’hi aliwaasa watumishi katika mkoa huu kuachana kabisa na matumizi ya karatasi na kujikita zaidi  katika matumizi  ya Mifumo ya TEHAMA, pamoja na mifumo ya uratibu wa Mashauri na Mifumo Mingene yote iliyoanzishwa au kutumiwa na Mahakama ya Tanzania  kwani lengo ni  kurahisishia utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Vilevile, Mhe. Dingo’hi aliwataka watumishi kuwachukulia wateja wote kwa usawa  bila kujali vyeo vyao, hadhi  zao hili kuwachukulia kwa usawa Mawakili wa Serikali na Mawakili wakujitegemea vyivyo hivyo.

Aidha, Jaji Dingo’hi aliwataka watumishi kuendelea kuleana kielimu (Mentorship) ikiwa ni mwendelezo wa utekelezaji wa agizo la Jaji Mfawidhi Kanda ya Mtwara Mhe.Edwin Kakolaki.

Mhe.Dingo’hi pia alitembelea na kukagua Mradi wa Ujenzi wa Kituo Jumuishi (IJC) Lindi pamoja na gereza la Wilaya ya Lindi.

Kwa upande wao viongozi wengine walioambatana na Jaji Dingo’hi katika ziara hiyo ya ukaguzi ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Seraphina Nsana, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkoa wa Lindi Mhe. Consolata Peter Singano, Mtendaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Bw. Yusuph Msawanga na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela  kwa nyakati tofauti wakati wa ziara hiyo waliwataka watumishi kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kwa nidhamu.

Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe.Saidi Dingo’hi (katikati) akiteta Jambo na watumishi (hawapo kwenye picha) wakati wa ziara ya ukaguzi.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe.Consolata Peter Singano akisoma taarifa ya Mahakama ya Mkoa wa Lindi Mbele ya Mhe.Jaji Dingo’hi.

Mtendaji wa Mahakama Kuu kanda ya Mtwara Bw. Yusuph Msawanga akiteteta jambo na watumishi katika ziara hiyo ya ukaguzi.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Godfrey Mbeyela akieleza jambo wakati wa ukaguzi.





Jaji wa Mahakama kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi akipanda Mti wa Kumbukizi alipotembelea Mahakama ya Mwanzo Mandawa iliyopo Wilaya ya Ruangwa.

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi wakiwa katika Picha ya pamoja na Jaji wa mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi (aliyesimama katikati).

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mtwara Mhe Saidi Dingo’hi na Jopo lake wakionyeshwa mwenendo wa Ujenzi wa Mradi wa chumba cha Mahakama Mtandao kinajojengwa Gereza kuu Lindi.


Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.

Watumishi wa Mahakama ya Wilaya ya Ruangwa wakiwa katika Picha ya pamoja na Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Saidi Dingo’hi wakati wa ziara yake ya ukaguzu wilaya ya Ruangwa.

Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.

Picha ikionyesha zoezi la ukaguzi wa mradi wa Ujenzi wa kituo Jumuishi (IJC) Lindi.







KIKAO CHA MENEJIMENTI MKOA WA MBEYA CHAKETI

Na. Muksini Nakuvamba – Mhakama, Mbeya

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, Mhe. Said Kalunde amengoza kikao cha menejimenti mkoa wa Mbeya kilichofanyika jana tarehe 09 Oktoba 2025 katika ukumbi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya.

 Akiwasilishwa taarifa ya utendaji kazi kwa kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2025/2026 Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya ambaye pia alikuwa Katibu katika kikao hicho Bi. Mervis Miti alitoa taarifa ya rasilimali watu ambapo ilieleza kuhusu hali ya watumishi wa Mahakama Mkoa wa Mbeya, upimaji wa watumishi na motisha za watumishi.

Aidha, taarifa hiyo ilieleza kuhusu taarifa ya usimamizi wa rasilimali fedha, vyombo vya usafiri, taarifa ya mashauri, taarifa ya matumizi ya TEHAMA na ushughulikiaji wa malalamiko na mapendekezo, utoaji wa elimu kwa umma na hali ya majengo mbalimbali ya Mahakama mkoa wa Mbeya.

Vilevile, taarifa hiyo ilifafanua juu ya mafanikio kadhaa ikiwemo kupokea watumishi 18 wa ajira mpya, ukarabati na uboreshaji wa baadhi ya majengo ya Mahakama, kusimamia nidhamu ya watumishi, matengenezo ya magari ya ofisi na kupokea na kuanza kutumika kwa Majengo mapya matatu yaliyojengwa kwa ufadhili wa Benki ya Dunia.

Kwa upande mwingine, taarifa hiyo ilieleza changamoto kadhaa ikiwemo uchakavu wa magari na majengo ya ofisi kama majengo ya Mahakama za mwanzo na nyumba ya kuishi Jaji Mfawidhi hali inayopelekea kupanga nyumba mtaani kwa gharama kubwa.

Changamoto zingine ni usajili wa mashauri kwa jina moja la wadaawa au washitakiwa kwa mashauri ambayo yana washitakiwa zaidi ya mmoja, sambamba na hilo pia kumekuwa na changamoto ya uwepo wa vielelezo vya muda mrefu katika mahakani, alisema Mtendaji huyo.

Taarifa hiyo pia ilifafanua juu ya mikakati kadhaa ya kuimarisha mifumo ya TEHAMA kwa kuhakikisha upatikanaji wa nishati na mtandao, kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa majengo na kuendelea kulipa mirathi kwa wakati.

Aidha, iliwasilishwa taarifa ya mashauri kwa Mahakama zote za mkoa wa Mbeya na Mahakama Kuu, Kanda ya mbeya, taarifa hiyo iliwasilishwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba.

“Baki ya mashauri hadi mwezi juni ni 639 na yaliyofunguliwa kuanzia julai hadi septemba ni 2481, yaliyomalizika kati ya julai hadi septemba ni 2501 na mashauri yaliyobaki hadi kufikia Septemba ni mashauri 619,” alisema Mhe. Mlimba.

Aidha, kikao kilijadili taarifa za Mirathi kwa Mahakama zote za Wilaya Mkoa wa Mbeya ambapo Mahakimu Wafawidhi wa Mahakama zote waliwasilisha taarifa zao.

Mtendaji hiyo wa Mahakama aliwasilisha taarifa ya mirathi inayowataka kushirikiana katika kufanya tathimini ya fedha zote zilizopo kwenye akaunti ya mirathi kwa Mahakama zote na kuzilipa kwa haraka na kutuma taarifa ya utekelezaji wa jambo hilo kabla ya tarehe 05 novemba, 2025.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya ambaye ni mwenyekiti katika kikao hicho akifuatilia mawasilisho.


Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya ambaye pia alikuwa Katibu katika kikao hicho Bi. Mervis Miti akitoa taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kanda hiyo.

Sehemu ya wajumbe wa kikao

Hakimu mkazi mfawidhi mahakama ya wilaya Rungwe Mhe. Jackson Banobi (aliyesimama) akiwasilisha taarifa ya mirathi mahakama ya wilaya Rungwe

Afisa Hesabu Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Bi. Nancy Rwebembela (aliyesimama) Akichangia Hoja katika kikao hicho

Sehemu ya wajumbe wa kikao

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (kulia) akiwasilisha taarifa ya mashauri na mirathi kwa Mahakama za Mkoa wa Mbeya.

 

SHEREHE ZA KUWAAGA WASTAAFU KANDA YA MTWARA YAFANA

Na. Hilary Lorry – Mahakama, Lindi

Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara ikijumuisha na Mikoa ya Lindi na Mtwara, imefanya sherehe ya kuwaaga watumishi waliostaafu utumishi wa umma kufikia October 2025,

Sherehe hiyo iliyofanyika ndani ya Hoteli ya Sea View Beach Resort iliyoko wilayani Lindi ikiwakutanisha viongozi mbalimbali wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara akiwemo Jaji Mfawidhi Mhe.Edwin Kakolaki, Jaji Saidi Ding’ohi,Jaji Martha Mpaze ,Naibu Msajili Mhe. Seraphine Nsana, Hakimu Mkazi Mfawidhi Lindi Mhe. Consolata Singano, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mtwara Mhe. Charles Mnzava ambaye pia ndiye aliekuwa Mshereheshaji wa shughuli hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Kanda ya Mtwara Mhe. Edwin Kakolaki katika sherehe hiyo aliwapongeza watumishi waliostaafu kwa utumishi wao uliotukuka katika kutoa huduma kwa wananchi kwa kipindi chote walichotumikia muhimili wa Mahakama.

“Kuna msemo unaosema “Life begins at forty” kwa maana Maisha yanaanza ukiwa na miaka arobaini. Lakini hiyo inatuhusu sisi tulio kazini. Ila kwa nyinyi wastaafu tunasema “Life begins at sixty” hivyo kwenu nyie Maisha ndo kwanza yameanza.” alisisitiza Mhe. Jaji Kakolaki.

Kwa nyakati tofauti Watendaji wa Mahakama Kuu Mtwara Bw. Yusuph Msawanga na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi.Quip Mbeyela waliwashukuru sana watumishi waliostaafu kwa utumishi wenye nidhamu kwa kipindi chote cha utumishi wao.

Aidha, amewaomba watumishi waliopo kazini kudumisha nidhamu mahala pa kazi na kuchapa kazi kwa bidii kwani ni moja kati ya misingi ya ufanisi kazini.

Wastaafu walioagwa walishukuru uongozi wa Mahakama Kanda ya Mtwara ukiongozwa na Mhe. Jaji Kakolaki kwa kuwaandalia sherehe hiyo ambayo hawakutarajia ingefana kwa kiasi hicho.

Pongezi nyingi zilielekezwa kwa Mwenyekiti wa maandalizi ya sherehe hiyo Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi. Mhe. Consolata Singano   Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Mbeyela na kamati nzima ya maandalizi ya Sherehe hiyo.

Sherehe hiyo pia ilihudhuriwa na Watendaji wa Mahakama ya Lindi na Mtwara, Mahakimu Wafawidhi wa Wilaya zote, Mahakimu Mahakama za Mwanzo na Maafisa wengine wa Mahakama Kanda ya Mtwara.

Wastaafu wakiwa ukumbini tayari kwa kuagwa

Wabobezi katika zoezi la ufunguzi wa Shampeni wakitekeleza jukumu hilo kwa umaridadi  mkubwa.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Edwini Kakolaki (wa pili kushoto) akiwa na, Jaji Saidi Ding’oi, wakiingia uwanjani kusakata rhumba.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Edwini Kakolaki (wa pili kushoto) akitoa zawadi kwa mmoja wa wastaafu katika sherehe hiyo

Wastaafu wakikata keki katika sherehe hiyo 

Bango lenye ujumbe wa kuwaaga wastaafu wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara na wakati huo Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Edwini Kakolaki  akiwahutubia waalikwa wote katika sherehe hiyo.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara Mhe. Edwini Kakolaki akigonga glass na Wastaafu kutakiana afya njema.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara Mhe. Edwini Kakolaki (wa tatu kulia) wakigonga glass kutakiana afya njema katika sherehe hiyo.

Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya sherehe ya kuwaaga wastaafu Kanda ya Mtwara Mhe. Consolata Singano (aliyesimama mbele) akitoa taarifa fupi ya sherehe hiyo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Lindi Mhe. Subilaga Mwakalobo (kushoto) akiwa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya wilaya ya Lindi Mhe. Khalfan O. Khalfan wakifuatilia sherehe hiyo.





JAJI KAHYOZA AFANYA ZIARA YA UKAGUZI WA MAHAKAMA KIGOMA

  • Awapongeza watumishi kwa kuchapa kazi, kutunza mazingira

Na AIDAN ROBERT-Mahakama, Kigoma

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza, kwa siku tano kuanzia tarehe 3 Octoba, 2025 alifanya ziara ya ukaguzi wa Mahakama za Wilaya ili kuangalia maeneo mbalimbali, ikiwemo usikilizaji wa mashauri, utekelezaji wa maagizo ya Viongozi wa juu na utunzaji wa mazingira.

Akizungumza katika moja ya Mahakama sita alizokagua, Mhe. Kahyoza alisema “Nawapongeza kwa kuchapa kazi, umalizaji wa mashauri kwa kiwango kizuri ni jibu kuwa mnatimiza wajibu wenu vema. Nawapongeza kwa weledi, ushirikiano, kwa kuendelea kutunza maadili na nidhamu na kwa  utunzaji mzuri wa mazingira.”

Jaji Kahyoza aliendelea kusisitiza kuwa yapo maelekezo ya Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju yanayowataka kuongeza ushirikiano kwa wadau wa Mahakama, kulinda maadili na nidhamu za Maofisa Mahakama na kutoa kipaumbele cha kusikiliza mashauri ya kiuchumi, biashara na kuhakikisha nakala za hukumu zinatolewa kwa wakati.

Alitoa rai kwa Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo Kanda ya Kigoma kuweke mkakati imara wa umalizaji wa mashauri kwa kiwango cha juu ili kuondoa na kuzuia mlundikano.

Naye, Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa alimshukuru Jaji Kahyoza kwa pongezi na maelekezo yake kwa shughuli za usikilizaji wa mashauri kwa Mahakama za Kanda ya Kigoma.

Aliahidi kuongeza kasi ya usimamizi na ufuatiliaji wa karibu wa maelekezo yote ili utekelezaji wake uwe msaada mkubwa kwa Mahakama na wadau kwenye mnyororo wa utoaji haki kwa wakati.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay alisema kuwa ataendelea kuongeza kasi ya usimamizi wa shughuli za Mahakama katika Kanda, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mazingira ya watumishi yanaendelea kuboreshwa ili kumrahisishia kutimiza majukumu yake.

Alibainisha Mahakama katika Kanda hiyo itaendelea kutumia rasilimali zilizopo kuhakikisha shughuli za usikilizaji wa mashauri zinafanyika vizuri katika Mahakama zote kanda ya Kigoma.

Mahakama zilizokaguliwa katika ziara hiyo ni Mahakama za Wilaya Kigoma, Kibondo, Kasulu, Uvinza na Kakonko pamoja na Baraza la Aridhi Wilaya Kasulu.


Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza akisisitiza jambo alipokuwa katika ziara ya ukaguzi wa Mahakama kwenye Kanda hiyo.

 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza akipanda mti wa matunda (Palachichi) katika Mahakama ya Wilaya Uvinza.

 Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza (wa kwanza kulia) akisikiliza maelezo toka kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Buhigwe, Mhe. Venance Mwakitalu (katikati) kuhusu ubunifu wa utunzaji wa mazingira. Kushoto ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Mwanzo Manyovu, Mhe. Straton Mosha.

Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay akisisitiza jambo kwa watumishi wa Mahakama ya Wilaya Kibondo kuhusu utendaji wa shughuli za Mahakama.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa akisisitiz jambo alipokuwa anaeleza hali ya ujenzi wa uzio wa Mahakama ya Wilaya Kasulu kwa Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza.

 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Kigoma, Mhe. Projestus Kahyoza (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Kigoma, Mhe. Fadhili Mbelwa (kushoto), Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Kigoma, Bw. Filbert Matotay (kulia), Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Mhe. Misana Majula (wa kwanza kulia), Ofisa Tawala wa Mahakama ya Wilaya Uvinza, Bw. Tumaini Panga (wa kwanza kushoto) na waliosimama ni sehemu ya watumishi wa Mahakama ya Wilaya Uvinza.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

 

 

 

 

Alhamisi, 9 Oktoba 2025

JAJI MKUU ASISITIZA UWAJIBIKAJI KWA WADAU WA HAKI MADAI

Asisitiza kuwa Dira ya Mahakama ni Haki Sawa kwa Wote Mapema Ipasavyo.

Awataka wadau wa Haki Madai kuzingatia haki, weledi na kujituma katika kutekeleza majukumu yao.

Na HABIBA MBARUKU, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewasisitiza wadau wa Haki Madai kuwajibika na kutekeleza wajibu wao ipasavyo ili kufikia malengo na kufanikisha ustawi wa wananchi ambalo ni jukumu la Serikali kwa mujibu wa Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Masaju aliyasema hayo jana tarehe 08 Oktoba, 2025 alipokuwa akifunga Mkutano wa wadau kuhusu mikakati na hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia mashauri ya kodi, biashara, mabenki na ushindani wa kibiashara, uliofanyika katika ukumbi wa mkutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

"Nilikuwa naangalia hapa michango yote iliyotoka ni ile ya kujenga ambayo imetoka kwa nia njema, na inaonesha utayari wa sisi sote tulioko hapa kila mmoja kutekeleza wajibu wake kwa ufanisi ipasavyo ili malengo haya yafikiwe. Nilipokuwa nazungumza juu ya zile 'softwares' nilikuwa nimezingatia mahusiano ya kijamii, kisiasa na kiuchumi yanayoendelea kuwepo katika Taifa letu. Sisi tukiwa watendaji na watumishi wa umma, tuna wajibu sasa kwenda sambamba na kuwepo kwa uhusiano wa kijamii, kisiasa na kiuchumi ili tunapotekeleza wajibu wetu tuzingatie kwamba tunawajibika kufanikisha ustawi wa wananchi ambalo ndio jukumu la Serikali kwa mujibu wa Ibara ya 8 ya katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania" alisema Jaji Mkuu.

Aidha, Mhe. Masaju alisisitiza kuwa lengo la Mahakama ni kutoa haki sawa kwa wote mapema ipasavyo na kuwahimiza wadau wengine kama vile Benki Kuu na Chama cha Wanasheria Tanganyina kuwajibika ipasavyo, kujituma na kuwa wabunifu katika kutimiza majukumu yao kwa ufanisi.

"Sisi kwenye Mahakama labda lengo letu ni nini, lengo letu sisi ni haki sawa kwa wote mapema ipasavyo na lengo la TRAT ni nini, lengo la TRAB ni nini, lengo la Benki Kuu ni nini, lengo la TLS ni nini, lengo la wadau wote ni nini, kila mmoja akijipima akiangalia hiyo, kwa vyovyote vile atakuwa mwenye kujituma, mwenye ubunifu, mwenye kuwajibika, yaani atataka kutekelea majukumu yake kwa umahiri" alisisitiza Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju aliongeza kuwa Taasisi zote zinazohusika na migogoro, utekelezaji wa majukumu yake utapaswa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya utumishi kwenye sekta mbalimbali katika Taifa na kuwa kila mtu anawajibika kuifuata na kuitekeleza Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na sheria zake kwa mujibu wa Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

"Mkakati wetu mkubwa ni kila Taasisi, Taasisi zote zinazohusika na migogoro na utekelezaji wa majukumu yake, zitapaswa tu kuzingatia Katiba, sheria na maadili yetu ya utumishi katika sehemu tunazotumikia katika Taifa hili, nazungumza juu ya uwajibikaji kwa sababu kila mtu anawajibika kuzifuata na kuzitekeleza Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na sheria zake, Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, ndicho kitu kinachoitwa utawala wa sheria, na sisi wote hapa tunafanya kazi kwa kufuata au kwa mujibu wa majukumu tuliyopewa kwa sheria mbalimbali," aliongeza Jaji Mkuu.

Jaji Mkuu pia alizungumzia suala la uwajibikaji na kujituma, na kuwataka wajumbe wote kujituma, kuwa waadilifu, kuwa waaminifu na kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya pamoja na malengo ya mtu mmoja mmoja ambayo yanaweza kusaidia katika kufikia malengo ya pamoja na malengo yaliyowekwa kwa mujibu wa sheria.

"Ukiangalia ule uwajibikaji, kwenye Ibara ya 25 ambayo napenda kuielezea, pale kuna mambo yamezungumzwa, kuna kujituma, uaminifu,  na uaminifu. Tunaweza kuchukulia pia ndio uadilifu, halafu kutimiza nidhamu, nidhamu ya kazi yetu ni ipi, na kujitahidi kufikia malengo, malengo ya pamoja kwa mfano sisi wote hapa kwenye hili tunapaswa tuwe na malengo ya pamoja, lakini na malengo ya kwetu binafsi, ambayo yanaweza kupelekea kufikia malengo ya pamoja, lakini na yale malengo ambayo tumewekewa sasa kwa mujibu wa sheria na pamoja na yaliyowekwa na sheria, kwa mfano Mahakama ya Tanzania ni malengo yapi tuliyowekewa na sheria, Taasisi nyingine ni malengo yapi, kwa hiyo haya ni msingi tukayazingatia sana," alisema.

Jaji Mkuu pia alizungumzia suala la mabadiliko ya kifikra katika mfumo wa utekelezaji wa majukumu, akirejelea Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 ili kuhakikisha inatekelezwa kwa ufanisi.

Alisema kuwa, Serikali imeweka mfumo imara wa usimamizi unaozingatia malengo yake mahususi, malengo yake mahususi ni yapi, mfumo huu umekusudia kuhimiza uwajibikaji, ukihitaji uongozi ulio mahiri na makini katika ufuatiliaji, aidha mfumo unahimiza matumizi ya mbinu zinazotoa matokeo yanayopimika.

"Ndio maana lazima tukutane tuangalie hivi siku ile tulikubaliana kufanya kitu gani, tuone kama tumepiga hatua na wapi tulipokosea, twende tuchukue hatua tujirekebishe," alisema.

Jaji Mkuu pia aliongeza  kuwa "msingi wa mkakati huu ni mabadiliko makubwa ya kifikra yakilenga vitendo badala ya maneno, na matokeo badala ya ahadi, uongozi, Taasisi pamoja na watendaji na wadau wote wanapaswa kuwajibika ili kutimiza malengo ya dira kwa ufanisi.

Alisema kwamba Taasisi imara na mifumo madhubuti inayolenga kuondoa uzembe, inayohimiza uwajibikaji na kuchochea ufanisi itakuwa nguzo kuu ya utekelezaji wa Dira ya 2050, ambayo imeweka mfumo madhubuti wa utawala unaohakikisha utekelezaji unafanyika kwa nidhamu, sera zinasomana, Taasisi zinakuwa imara na kila sekta na wadau wote wanashirikiana.

Aidha, Mhe. Masaju alisema kuwa mfumo wa kidigitali wa ufuatiliaji tathmini na kujifunza utawezesha utekelezaji himilivu utakaobadili misukosuko ya kiuchumi, mabadiliko ya tabia ya nchi  na maendeleo ya kiteknolojia pamoja na matumizi ya akili unde.

"Matumizi ya teknolojia yanazoendelea kama vile akili unde, mifumo ya taarifa za kijiografia, uchambuzi wa data kwa wakati halisi yataleta ufanisi wa sera, ufuatiliaji na mgawanyo wa rasilimali na mwisho, ili kuimarisha uwajibikaji viashiria vya utendaji katika maeneo hayo vitatumika kufuatilia maendeleo. Ndicho alichokuwa anatukumbusha hapa Naibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, ili kuimarisha uwajibikaji viashiria vya utendaji vitatumika kufuatilia maendeleo, kutambua changamoto na kuboresha utendaji, " aliongeza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju alisema kuwa, mfumo wa motisha na adhabu utaongeza uwajibikaji kwa watumishi, kuondoa uzembe pamoja na kuhakikisha kuwa utekelezaji wa majukumu unaleta matokeo yenye manufaa kwa Taifa.

"Mfumo wa motisha na adhabu utaimarisha utamaduni wa uwajibikaji ukihamasisha ubora na kuondoa uzembe na kuhakikisha kuwa utekelezaji unaleta matokeo yenye manufaa," alisisitiza.

Mkutano huo umejadili mikakati ya kuboresha utendaji kazi ambayo ni pamoja na wadau wote wa mnyororo wa haki pale inapowezekana watumie njia ya usuluhishi kutatua migogoro kwa mashauri ya kodi, biashara, mabenki na ushindani wa kibiashara kabla hayajafika mahakamani.

Kila Taasisi ambayo ni mdau wa mnyororo wa haki mahakamani iwajibikie ipasavyo kutekeleza jukumu lake kwa kuzingatia Katiba, Sheria na maadili ya utumishi wa Taasisi husika. Wadau wote wa haki madai wenye mashauri mahakamani, wawe tayari kuhudhuria na kuyaendesha kikamilifu ili kuwezesha haki kupatikana mapema ipasavyo.

Mahakama na wadau wa mnyororo wa haki waimarishe mawasiliano miongoni mwao kwa lengo la kuchukua hatua haraka pale changamoto zinapojitokeza.

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akifunga Mkutano wa Wadau Kuhusu Mikakati na Hatua Zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Sehemu ya Wadau waliohudhuria Mkutano
 wa Wadau Kuhusu Mikakati na Hatua Zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (wa pili kulia) akijadiliana jambo na baadhi ya Wadau wa Haki Madai walioshiriki katika Mkutano wa Wadau Kuhusu Mikakati na Hatua Zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.





 

JAJI MKUU AWAAGIZA MAJAJI, MAHAKIMU KUMALIZA MASHAURI YA KODI, BIASHARA, MABENKI IFIKAPO DESEMBA 15

·       Aitisha Kikao cha Wadau kueleza mikakati ya Mahakama na kuweka mikakati ya pamoja

·       Asema hatua hiyo ni moja ya mikakati ya kufikia Dira ya Mahakama sanjari na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050

·       Asema mashauri hayo yana mchango mkubwa katika ukuaji wa Uchumi wa Nchi

·       Awasihi Wadau wa Haki Madai kutoa ushirikiano na kila mmoja kutekeleza wajibu wake ipasavyo

·       Wadau wakiwemo Tume ya Mipango, Benki Kuu, Mwanasheria waipongeza Mahakama kwa hatua hiyo

Na MARY GWERA, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju amewataka Majaji na Mahakimu nchini kukamilisha mashauri yote ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Ardhi ifikapo tarehe 15 Desemba, 2025, huku akiwataka wadau wote wa haki madai kutoa ushirikiano wa dhati kwa kila mmoja kuwajibika ipasavyo ili kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Mahakama ya Utoaji Haki Sawa mapema ipasavyo ili kuchangia kukuza uchumi wa nchi na kuvutia mazingira ya uwekezaji.

Akizungumza jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma alipokuwa akifungua Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi, Mhe. Masaju alisema mkakati huo unaenda sambasamba na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 katika eneo la kuboresha utoaji haki.

“Sisi Mahakama ni wadau muhimu katika hili eneo ambalo linagusa uchumi na tumejipanga, Mahakama tunatambua wajibu wetu kwenye utatuzi wa migogoro, ndio maana tumeitisha kikao hiki ili kuwashirikisha mikakati tunayochukua sisi na hatua tunazozichukua kuhakikisha kwamba mashauri haya ambayo yapo mahakamani yanaamuliwa mapema ipasavyo ili watu waendelee na shughuli zao, fedha ambazo zimefungiwa huku ziweze kufunguliwa ziingie kwenye mzunguko wa uchumi ili ziweze kuwanufaisha Watanzania,” alisema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju alieleza kuwa, azma hiyo itafanikiwa endapo Mahakama itapata ushirikiano wa wadaawa wanaokuja mahakamani  ambapo alisema, “tunataka kama vile ambavyo Mahakama imejitoa hata kwa rasilimali kidogo sana na wakati fulani kulazimika kuchukua hela fulani kwenye matumizi fulani kuzileta huku, lakini ukweli ni kwamba sisi haya tunafanya kwa nia njema na hii ikifanikiwa itatusaidia sana kwenda mbele, hivyo tumejipanga tunataka twende, hatutaki kukwamishwa na mtu.”

Kadhalika, Jaji Mkuu alisema kwamba, pamoja na kuwashirikisha Wadau hao kuhusu mikakati ya Mahakama ya kushughulikia migogoro yote na kuimaliza mapema ipasavyo amewaeleza kuwa na Dira ya Mahakama isemayo; ‘Haki sawa kwa wote mapema ipasavyo’ nayo inataka kutoa haki mapema ipasavyo, lakini katika kutekeleza Dira hiyo, Mahakama inajifungamanisha na Dira ya Taifa ya Maendeleo, hivyo ni muhimu kwa Wadau kushirikiana ili kwa pamoja kufanikisha Dira hizo.

Mhe. Masaju aliongeza kuwa, katika jitihada za kuhakikisha huduma za haki zinawafikia wananchi kwa karibu zaidi, Mahakama imepanga kushusha huduma za Mahakama ya Rufani katika Kanda na kwa kuanzia itakuwa katika Mikoa ya Dar es Salaam na Mikoa mingine yenye mashauri mengi.

“Kwahiyo sasa katika kuwashirikisha hii mikakati yetu tutapata fursa na pengine na ninyi kujua kinachoendelea hapa, mtatusaidia na ninyi kuboresha wapi ambapo hatufanyi vizuri, muwe huru mseme ndio maana ya mkutano, muwe huru labda mtusaidie hata kuboresha mikakati yetu, lakini pia pale ambapo hatufanyi vizuri mtueleze kwa sababu kufanikiwa kwa Taasisi moja kwenye suala hili ambalo ni mtambuka Taasisi nyingine zikiwa hazikufanikiwa hatutakuwa tumepiga hatua. Kwa hiyo tumewaita ili tushirikishane, tusemane hapa kwa nia njema ya kwenda mbele, tumewaita wote hapa mkiwa wote ni wahusika wakuu kwa mfano tumewaita watu wa TLS, Mabenki, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Gavana wa Benki Kuu na wadau  wengine,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu alisema kwamba, kupitia mkutano huo watapata fursa ya kuambiana madhaifu ya kila Taasisi lengo likiwa ni kwenda mbele. Ameeleza kuwa, “sisi wakati tunaweka hii mikakati ya kutekeleza wajibu wetu wa kutoa haki sawa mapema ipasavyo na ninyi sasa ambao ni wadau wetu mtusaidie namna gani mtaungana na sisi katika kulifanikisha hili ili wote twende pamoja.”

“Kwa ujumla mapinduzi makubwa yanahitajika katika kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini hususani katika kubadilisha Sekta ya Umma kutoka kuwa mdhibiti kwenda kuwa Mwezeshaji wa biashara na uwekezaji na katika hii ya mwisho ndio na sisi pia tunaingia pale na Mahakama ina mchango mkubwa kwenye hili suala,” amesisitiza Mhe. Masaju.

Mhe. Masaju aliishukuru Wizara ya Fedha kwa kuendelea kutambua umuhimu wa Mahakama na kuiwezesha kufanya kazi zake vizuri, huku akiwataka wadau wengine kama Umoja wa Mabenki Tanzania (TBS), Madalali na Wasambaza Nyaraka wa Mahakama na wadau wengine kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu bila kuzalisha migogoro.

Aidha, Mhe. Masaju alisema, mashauri hayo ni eneo ambalo linagusa masuala ya uwekezaji na biashara, “Na mimi ninachoweza kusema ni kwamba tumeanza utekelezaji wa Dira mpya ya Taifa ya Maendeleo 2050 na Dira hii mnafahamu ina msingi mkuu ambao msingi mkuu unahusu Utawala, Amani, Usalama na Utulivu lakini na vipaumbele vyake ambavyo viko vinne, cha kwanza kabisa ni Utawala Bora na Haki, halafu cha pili Serikali imara za Mitaa na Ufanisi lakini kipengele cha tatu ni Uwajibikaji utumishi wa Umma lakini kipengele cha nne ni Amani, Usalama, Utulivu hivyo ndio vipaumbele vya msingi mkuu wa Dira.”

Aidha, Jaji Mkuu alieleza kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 imebeba nguzo tatu ambapo nguzo ya kwanza inahusu uchumi imara, jumuishi na shindani.

“Na mkiangalia haya mashauri ambayo sisi tumewashirikisha, mkakati ambao tunachukua yana mchango mkubwa sana katika Uchumi na unaposoma ukurasa 21 wa Dira hiyo inasema Uchumi imara, jumuishi na shindani ni moja ya nguzo kuu ya kujenga Taifa lenye ustawi kwani nguzo hii inafungua fursa za kiuchumi na hivyo kuweka mazingira ya kupunguza umaskini na kuboresha hali ya maisha ya wananchi wote, Uchumi imara utahakikisha kwamba maendeleo ya kiuchumi yanakua na taswira chanya kwa jamii na kuwanufaisha wananchi wote,” amesema Mhe. Masaju.

Jaji Mkuu amesema katika moja ya vipengele vya nguzo hii ya Uchumi imara ni mazingira wezeshi ya biashara na uwekezaji ambapo ukurasa wa 25 wa Dira; ‘Uchumi imara na endelevu unategemea kuwepo kwa mazingira mazuri ya kufanya biashara.’

Aidha, aliongeza kwamba, mwaka 2018, Tanzania ilizindua Mpango Mkakati wa Mageuzi ya Sheria ya kuboresha mazingira ya biashara nchini ambao ulilenga kuimarisha ufanisi katika mifumo ya kisheria, kurahisisha michakato ya usajili na usimamizi wa biashara na kuongeza uwazi na uwajibikaji ambapo vipengele vikuu ilikuwa ni kupitia upya sheria na kanuni, kupunguza kodi na ada zisizo na ufanisi na kuboresha uwezo wa Taasisi za kudhibiti ili kuzifanya zijielekeze zaidi katika kuchangia ukuaji wa Sekta ya Biashara badala ya kuweka mkazo katika makusanyo ya mapato pekee.

“Pamoja na juhudi hizo, changamoto mbalimbali zimeendelea kuyagubika mazingira ya biashara nchini ikiwemo gharama na muda mkubwa wa usajili na ukosefu wa mitaji, kikwazo kingine ni urasimu katika utendaji jambo linaloongeza muda ambao Wawekezaji wanachukua kukamilisha taratibu za awali za kuidhinisha biashara na uwekezaji,” amesema Mhe. Masaju.

Aidha, Jaji Mkuu amebainisha kuwa, uendeshaji wa biashara umeendelea kuwa na uthibiti uliokithiri ukiathiri utaratibu wa kodi na mapato kwa bidhaa zenye thamani kubwa, migongano ya Sera, Sheria na Kanuni na kuwepo kwa miingiliano ya majukumu ya Taasisi za Udhibiti, ambapo ameeleza kuwa, “suala hili limezifanya biashara kubeba mzigo mkubwa wa kodi, ada na ongezeko la gharama kutokana na masharti mengi ya leseni na vibali.”

Ameongeza kwamba, ili kushughulikia changamoto hizo ni lazima kujenga mazingira wezeshi ya kibiashara yatakayochochea ukuaji wa Uchumi na kuvutia uwekezaji na kwamba mageuzi hayo yanapaswa kurahisisha taratibu, kupunguza vikwazo vya kisheria, kuondoa tozo zisizo na tija na kufungamanisha Sera na Taasisi ili kuimarisha mazingira ya biashara yenye ushindani na ufanisi.

Kadhalika, Jaji Mkuu pia alisisitiza suala la uwajibikaji na uadilifu kwa Mahakama na wadau wote wa Haki Madai kuwajibika na kujituma ipasavyo, na kuweka wazi kuwa suala la kuwajibika ni suala la kikatiba hivyo kila mmoja anapaswa kuwajibika huku akitimiza malengo yake binafsi na yale ya pamoja.

"Kwetu sisi wenyewe huku Mahakamani tumekuwa na mafunzo na tunawajibishana, sasa na ninyi, wakati Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 inazungumza juu ya uwajibikaji kwa watumishi wa umma, hili suala ni la kikatiba, Ibara ya 25 ibara ndogo ya kwanza ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema hivi, 'kazi pekee ndio uzao tajiri wa mali katika jamii ndilo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha utu na kila mtu ana wajibu wa (a) kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali na (b) kutimiza nidhamu ya kazi na kujitahidi kufikia malengo ya uzalishaji mali ya binafsi na yale malengo ya pamoja yanayotakiwa au yaliyowekwa na sheria.'

Kupitia Mkutano huo Wadau hao wa Haki Madai walipata fursa ya kujadiliana masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na changamoto zilizopo na kuweka mikakati thabiti ya kuondokana na changamoto hizo na hatimaye kuweza kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Wadau mbalimbali waliohudhuria katika Mkutano huo ambao ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba, Mahakama Kuu ya Tanzania Divisheni ya Biashara, Mahakama Kuu ya Tanzania, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Msajili wa Hazina, Tume ya Taifa ya Mipango, Baraza la Ushindani, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Wizara ya Fedha, Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA), Mamlaka ya Uwekezaji na Maeneo maalum ya Kiuchumi (TISEZA), NBC, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Baraza la Rufani za Kodi, Chama cha Madalali Tanzania, na Wasambaza Nyaraka za Mahakama.


Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Imani Aboud akitoa neno la utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju 
(hayupo katika picha) kufungua Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Morogoro ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Ushindani (FCT) akichangia jambo wakati wa 
Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kushoto ni Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba.

Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania, Bw. Emmanuel Tutuba (kushoto) akichangia jambo wakati wa Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Kulia ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza Johari.
Wadau mbalimbali wa Mkutano huo wakichangia majadiliano

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Kuu, Mhe. Abdi Kagomba akichangia jambo wakati wa mkutano huo.



Jaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha za pamoja na makundi mbalimbali ya wadau waliohudhuria katika Mkutano wa Wadau kuhusu Mikakati na Hatua zinazochukuliwa na Mahakama ya Tanzania kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki na Ushindani wa Kibiashara na Ardhi jana tarehe 08 Oktoba, 2025 kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jaji Mkuu Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Amidi wa Mahakama hiyo, Mhe. Imani Aboud na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, Mhe. Dkt. Juliana Masabo.