Jumanne, 11 Agosti 2026

WATUMISHI IJC DODOMA WAVUTIWA NA UZURI WA ZIWA MANYARA

Na ARAPHA RUSHEKE – Mahakama, Dodoma

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma (IJC), tarehe 9 Agosti, 2026 walitembelea Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara kwa lengo la kujifunza, kujenga uelewa kuhusu uhifadhi wa mazingira na kutambua fursa mbalimbali za utalii zinazopatikana nchini Tanzania.

Ziara hiyo iliongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga. Wakiwa kwenye ziara hiyo, watumishi hao walipata fursa ya kujifunza kwa vitendo kuhusu historia, mazingira, wanyamapori pamoja na shughuli mbalimbali za utalii zinazopatikana katika hifadhi hiyo.

Akitoa elimu kwa watumishi hao, Afisa Utalii, Afande Clara Temu, alisema Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara ina ukubwa wa takribani kilomita za mraba 648.7, ambapo kilomita za mraba 386 ni eneo kavu huku sehemu nyingine ikiwa ni eneo la Ziwa.

Temu amesema hifadhi hiyo ina vivutio mbalimbali vinavyowavutia watalii kutoka ndani na nje ya Tanzania, ikiwemo Simba wanaopanda miti, chemchem za maji ya moto, Ziwa Manyara pamoja na utalii wa ndege, ambapo hifadhi hiyo ina zaidi ya aina 400 za ndege.

Ameongeza kuwa Ziwa Manyara pia ni muhimu kwa uhifadhi wa ndege wa majini na ni makazi ya wanyama mbalimbali wakiwemo viboko.

Katika ziara hiyo, watumishi hao walipata fursa ya kutembelea Tree Canopy Walkway, kivutio kinachowawezesha watalii kutembea juu ya njia zilizojengwa katikati ya miti na kupata mwonekano wa kipekee wa mazingira ya hifadhi.

Akitoa maelezo kuhusu kivutio hicho, Muongoza Watalii Regina Dunduli alisema Tree Canopy Walkway ilijengwa mwaka 2016 na kuanza kutumika mwaka 2017, ikiwa na madaraja tisa (9) pamoja na majukwaa 10.

Bi. Dunduli alisema kuwa njia hiyo imejengwa katikati ya miti ikiwemo miti ya mahogany na inawapa watalii fursa ya kuona kwa karibu aina mbalimbali za ndege, wanyama na mimea.

Alieleza kuwa watu wasiozidi wanne wanaruhusiwa kutumia sehemu hiyo kwa wakati mmoja, huku watalii wakitakiwa kuzingatia maelekezo ya waongoza watalii na taratibu za usalama.

Kwa mujibu wa Bi. Dunduli, shughuli hiyo huchukua kati ya dakika 45 hadi saa moja, huku watalii wakitakiwa kuwa watulivu na kuzungumza kwa sauti ya chini ili kutowasumbua wanyama.

Watumishi hao pia walielezwa kuwa Hifadhi ya Taifa ya Lake Manyara inatoa fursa za shughuli mbalimbali za utalii, zikiwemo walking safari, kuangalia machweo ya jua (sunset viewing), kupiga makasia, utalii wa ndege pamoja na utalii wa usiku.

Aidha, watalii wanaweza kufanya matembezi marefu kwa miguu yanayoweza kuchukua kati ya saa moja hadi saa nne, kulingana na aina ya shughuli wanayochagua. Kwa watalii wenye mahitaji maalum ya usafiri, pia kuna uwezekano wa kutumia helikopta kutembelea maeneo mbalimbali ya hifadhi.

Ziara hiyo imewapa watumishi hao fursa ya kujifunza kwa vitendo umuhimu wa utalii wa ndani, uhifadhi wa mazingira na matumizi endelevu ya rasilimali za asili, huku ikiwahamasisha kutambua na kuthamini utajiri wa vivutio vilivyopo nchini.

Ziara hiyo ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha watumishi kujifunza nje ya mazingira ya kazi, kujenga uelewa mpana na kuendelea kuutangaza utalii wa ndani kwa kutembelea na kufahamu vivutio mbalimbali vinavyopatikana nchini.

Afisa utalii wa Lake Manyara, Afande Crala Temu akitoa elimu ya hifadhi kwa watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo  Dodoma baada ya kuwasili katika hifadhi hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto) akiwa na Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe Suleiman Hassan mara baada ya kuwasili katika Hifadhi ya Lake Manyara.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Joachim Tiganga, (wa tatu kutoka kulia)akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi waliotoka Mahakama pamoja na Hifadhi ya Lake Manyara, wa nne kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe Suleiman Hassan, anayefuatia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Upendo Ngitiri, akifuatiwa ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Mhe. Zabibu Mpangule, wa kwanza kulia ni Kaimu Mtendaji wa Mahakama Dodooma, Bw. Stanslaus Makendi na wa pili kulia Afisa Utalii wa Hifadhi ya Lake Manyara, Afande Crala Temu.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kuwasili katika hifadhi hiyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akifurahia jambo mara ya kutembelea katika daraja hilo.

Jaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Suleimani Hassan akitembea katika daraja pamoja na watumishi wengine.

Watumishi wa Mahakama Kuu Dodoma wakifurahia jambo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe Upendo Ngitiri, akifurahia jambo wakati akimaliza kutembea katika daraja hilo.

Afisa Utalii, Afande Crala Temu (aliyepo katikati) akitoa shukran kwa Jaji wa Mahakama Kuu Dodoma, Mhe. Suleimani Hassan (wa kwanza kulia )baada ya kukabidhiwa zawadi kutoka kwa watumishi hao.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.


WATUMISHI IJC DODOMA WAFANYA ZIARA YA MAFUNZO HIFADHI YA NGORONGORO

Na ARAPHA RUSHEKE – Mahakama, Dodoma

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo Doodoma, Mhe. Joachim Tiganga, hivi karibuni aliwaongoza watumishi kufanya ziara ya mafunzo katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Lengo la ziara hiyo lilikuwa kujifunza kuhusu uhifadhi wa mazingira na wanyamapori, historia, utamaduni pamoja na vivutio mbalimbali vya utalii vinavyopatikana katika eneo hilo.

Ziara hiyo ilijumuisha pia Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Suleimani Hassan, Naibu Wasajili na Watumishi wa Mahakama kutoka Mkoa wa Dodoma na Wilaya zake za Kongwa, Chamwino, Mpwapwa, Chemba na Kondoa.

Wakiwa kwenye ziara hiyo, watumishi hao walipatiwa elimu kuhusu historia ya Hifadhi ya Ngorongoro, wanyamapori wanaopatikana katika eneo hilo, shughuli za uhifadhi pamoja na changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika kulinda mazingira na wanyamapori.

Elimu hiyo imewasaidia watumishi kupata uelewa mpana kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira na wanyamapori, pamoja na nafasi ya Hifadhi ya Ngorongoro katika kulinda urithi wa Taifa na kukuza utalii nchini.

Watumishi hao walitembelea eneo lenye mchanga unaohama, ambapo walipata maelezo kutoka kwa Bw. Ndengere Ngisaruni kuhusu hali hiyo ya kipekee ya kimaumbile ambayo imekuwa miongoni mwa vivutio vinavyowavutia watalii kutoka sehemu mbalimbali duniani.

Aidha, watumishi hao walitembelea Olduvai Gorge, eneo maarufu kwa historia ya mwanadamu wa kale, ambapo walipata fursa ya kujifunza kuhusu ugunduzi wa mabaki ya viumbe wa kale na historia ya mwanadamu.

Katika eneo hilo, watumishi walielezwa pia kuhusu historia ya Faru Fausta, aliyefariki akiwa na takribani miaka 57, pamoja na taarifa mbalimbali zinazohusiana na historia ya wanyamapori na urithi wa eneo hilo.

Ziara hiyo pia iliwapa watumishi hao fursa ya kutembelea Boma la Kimasai, ambapo walijifunza kuhusu maisha, mila, desturi na utamaduni wa jamii ya kimasai, pamoja na namna utamaduni huo unavyohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine.

Akitoa shukrani kwa niaba ya watumishi hao, Mhe. Tiganga aliushukuru uongozi wa Hifadhi ya Ngorongoro kwa mapokezi mazuri, ushirikiano na elimu waliyopewa wakati wa ziara hiyo.

Mhe. Tiganga alisema ziara hiyo imekuwa fursa muhimu kwa watumishi kujifunza mambo mapya nje ya mazingira yao ya kawaida ya kazi, huku ikiwapa nafasi ya kujenga mshikamano, kubadilishana uzoefu na kuongeza uelewa kuhusu historia, mazingira na utamaduni wa Tanzania.

Kwa ujumla, ziara hiyo imekuwa sehemu ya kujenga maarifa na mshikamano miongoni mwa watumishi wa Mahakama, sambamba na kuwapa fursa ya kutambua kwa undani zaidi utajiri wa historia, mazingira, wanyamapori na tamaduni zinazopatikana nchini.

Ziara hiyo imehitimisha kwa mafanikio, ikiwaacha watumishi hao na maarifa mapya kuhusu umuhimu wa kuhifadhi mazingira, wanyamapori, historia na utamaduni wa Tanzania kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Masjala Bdogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiwa katika picha ya pamoja na watumishi baadaya ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akifafanua kitu mara baada ya kuwasili katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akifafanua kitu mara baada ya kufika katika mabaki na masalia ya vitu vya kale.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakipatiwa elimu wakati walipofika katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiendelea na utalii katika Hifadhi ya Ngorongoro.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga, akiwa na watumishi wakiangalia mabaki ya Faru Fausta aliishi miaka 57.

Watumishi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma wakiongozwa na Jaji Mfawidhi wakiwa katika picha ya pamoja katika sehemu ya mchanga unaohama uliopo Hifadhi ya Ngorongoro. 

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma.

MAJAJI, MAHAKIMU MBEYA WANOLEWA JINSI YA KUKABILIANA NA MSONGO WA MAWAZO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Majaji, Naibu Wasajili na Mahakimu wa Mahakama Masjala Ndogo ya Mbeya wametakiwa kutambua, kudhibiti na kukabiliana na msongo wa mawazo kwa wakati, wakizingatia kuwa afya njema ya akili ni msingi muhimu wa kufanya maamuzi yenye umakini, weledi na ya haki katika utekelezaji wa majukumu yao.

Wito huo umetolewa katika mafunzo maalumu yaliyowakutanisha Majaji na Mahakimu wa Masjala Ndogo ya Mbeya, yaliyofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Lake Nyasa, iliyopo katika fukwe za Ziwa Nyasa, Wilaya ya Kyela, ambapo washiriki walipata elimu kuhusu chanzo, madhara na namna bora ya kukabiliana na msongo wa mawazo katika maisha na mazingira ya kazi.

Mafunzo hayo yaliendeshwa na mtaalamu wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Kilutheri ya Matema, Wilaya ya Kyela, Dkt. Ebenezer Richard Minja, ambaye aliwaeleza washiriki kuwa msongo wa mawazo ni hali inayoweza kumpata mtu kutokana na changamoto mbalimbali za maisha na mabadiliko ya mazingira au mtindo wa maisha na kwamba hali hiyo inapopuuzwa inaweza kuleta madhara makubwa kwa afya ya mtu.

Dkt. Minja alisisitiza umuhimu wa mtu kutambua mambo yanayoweza kumletea msongo wa mawazo na kuchukua hatua stahiki mapema, akiwataka washiriki kuzingatia ulaji unaofaa, kufanya mazoezi mepesi mara kwa mara na kuepuka tabia ya kujilinganisha na watu wengine.

Aidha, alieleza kuwa kufanya ibada ni miongoni mwa njia zinazoweza kumsaidia mtu kupata utulivu wa akili, kwa kuwa humwezesha mtu kujenga imani na kumweleza Mungu changamoto anazokabiliana nazo.

Kwa mujibu wa Dkt. Minja, msongo wa mawazo unapokomaa unaweza kuathiri kwa kiasi kikubwa afya ya mtu na kusababisha matatizo mbalimbali, yakiwemo shinikizo la juu la damu, magonjwa ya moyo, kupoteza kumbukumbu, kupungua uzito na kushuka kwa kinga ya mwili, hali inayoweza kuongeza hatari ya kupata magonjwa mengine kama kisukari.

“Ukihisi mambo yanaenda mrama, tafuta msaada mapema. Njiti moja ya kiberiti inaweza kuangamiza msitu mzima, hivyo chukua hatua mapema kupambana na msongo wa mawazo kabla matatizo makubwa hayajajitokeza,” alisema Dkt. Minja, huku akisisitiza umuhimu wa kutafuta msaada mapema pale mtu anapohisi kuzongwa na msongo wa Mawazo.

Akizungumzia suala hilo kwa mtazamo wa mazingira ya kazi za Mahakama, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya alisema kuwa, majukumu ya kimahakama yanaweza kuwa miongoni mwa vyanzo vya msongo wa mawazo kutokana na mlundikano wa mashauri, uzito wa maamuzi yanayofanywa pamoja na mazingira mbalimbali yanayowazunguka watendaji hao.

Bw. Chonya aliongeza kuwa, changamoto hizo zinahitaji usimamizi mzuri wa muda, kutenganisha majukumu ya kikazi na maisha ya nyumbani pamoja na kutafuta ushauri wa kitaalamu pale mtu anapohisi amelemewa.

“Akili iliyochoka inashindwa kuchuja ukweli na uwongo kwa wakati, hivyo tujitahidi kudhibiti msongo wa mawazo. Kwani afya ya watendaji wa Mahakama ina uhusiano wa moja kwa moja na uwezo wao wa kutekeleza wajibu wa kutoa haki kwa jamii,” alisema Bw. Chonya.

“Ili uweze kutoa haki kwa jamii ni lazima ujitendee haki mwenyewe kwa kulinda afya ya mwili na akili. Jamii inatuhitaji tukiwa na afya njema na akili timamu,” alisema Mtendaji Chonya

Katika mafunzo hayo pia washiriki walijifunza umuhimu wa kuzuia changamoto kabla hazijawa kubwa kwa kujadili umuhimu wa mpango wa malezi kwa mahakimu “mentorship programe”

Akizungumzia suala hilo, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, alisema ‘Mentorship Programme’ ni muhimu katika kuwasaidia Mahakimu kukua kitaaluma, kuboresha utendaji wao na kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza katika safari yao ya kiutumishi.

Mhe. Mtulya alisema kuwa, malezi ya kitaaluma yanaweza kuwa nyenzo muhimu ya kumsaidia Hakimu kupata ushauri mapema kabla changamoto anazokabiliana nazo hazijawa kubwa na kuathiri utendaji wake au kufikia hatua ya kushughulikiwa na Kamati za Maadili.

“Mahakimu wengi wanaharibikiwa kwa kutopata mlezi wa kumsaidia kabla changamoto haijawa kubwa hadi kufikia kwenye Kamati ya Maadili,” alisema Mhe. Mtulya.

Kwa upande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Mbeya, Mhe. Teddy Mlimba, alisisitiza umuhimu wa kuwa na viongozi, walezi na wasimamizi wanaoweza kuwasaidia watendaji kukabiliana na changamoto za kazi na maisha kwa wakati.

“Kazi zetu ni ngumu sana na ukipata mtu wa kumtolea mambo au changamoto zako ni jambo kubwa sana, hivyo ni muhimu kupata kiongozi, mlezi na msimamizi wa kukusimamia,” alisisitiza Mhe. Mlimba

Mafunzo hayo yameweka wazi kuwa mjadala kuhusu afya ya akili kwa Majaji na Mahakimu haupaswi kuangaliwa kama suala binafsi pekee, bali kama sehemu ya kujenga mazingira bora ya utoaji wa haki.

Majukumu ya kimahakama yanahitaji umakini mkubwa, uwezo wa kuchambua hoja kwa kina na kufanya maamuzi kwa usawa na bila kuyumbishwa. Kwa msingi huo, kulinda afya ya akili na mwili, kusimamia muda, kutafuta msaada pale inapohitajika na kuwa na mfumo imara wa malezi na ushauri wa kitaaluma ni miongoni mwa hatua zinazoweza kuimarisha ustawi wa watendaji na ufanisi wa kazi za Mahakama.

Hatua hiyo pia inalinda dhamira ya kujenga Mahakama yenye watendaji wenye weledi, maadili na utayari wa kutekeleza wajibu wao kwa uadilifu. Afya ya akili ya watendaji wa Mahakama ni uwekezaji katika haki na kulinda akili iliyo imara ni sehemu ya kulinda haki ya mwananchi.

Mtaalamu wa afya ya akili kutoka Hospitali ya Kilutheri ya Matema, Wilaya ya Kyela Dkt. Ebenezer Richard Minja (aliyesimama) akitoa mafunzo ya kukabiliana na Msongo wa Mawazo kwa Waheshimiwa Majaji na Mahakimu (hawapo pichani).

Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Mahakimu ambao walioshiriki katika mafunzo hayo ambao ni wananchama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Ndogo ya Mbeya wakifanya zoezi kwa vitendo.

Sehemu ya washiriki katika mafunzo hayo ambao ni Mahakamu wananchama wa Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Tawi la Masjala Ndogo ya Mbeya wakifuatilia mafunzo hayo kwa makini.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Roster Mofuga akichangia jambo katika mafunzo hayo, (katikati) ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba na (kushoto) ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer.

Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (aliyesimama) akizungumza jambo katika mafunzo hayo, kulia ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Viongozi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa katika mafunzo hayo (wa kwanza kushoto) ni Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya, (katikati) ni Jaji wa Mahakama kuu masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angaza Mwipopo na Jaji wa Mahakama Kuu Masijala Ndogo ya Mbeya Mhe. Mussa Pomo (wa kwanza kulia)

(Habari Hii Imehaririwa na INNOCENT KANSHA - Mahakama)




TMJA MBEYA WAHIMIZWA KUIMARISHA WELEDI, MAADILI NA MSHIKAMANO

Na MUKSINI NAKUVAMBA – Mahakama, Mbeya

Majaji na Mahakimu wa Mahakama ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mbeya, wametakiwa kuendelea kudumisha weledi, maadili, mshikamano na mahusiano mema katika utendaji wa kazi, huku wakihimizwa kuongeza maarifa na kufanya tafiti za kitaalamu kwa ajili ya kuimarisha weledi katika utoaji haki.

Wito huo umetolewa katika kikao cha Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya, kilichofanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 7 hadi 9 Agosti 2026, katika fukwe za Ziwa Nyasa, Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

Akizungumza katika kikao hicho, Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Fahamu Mtulya, amewakumbusha wanachama kuzingatia malengo ya chama hicho, hususan kudumisha hadhi na heshima baina ya Majaji na Mahakimu, pamoja na kuimarisha maarifa, uelewa na uwezo wao katika kufanya tafiti za kitaalamu.

“Miongoni mwa malengo ya TMJA Mbeya ni pamoja na kudumisha hadhi na heshima baina ya Majaji na Mahakimu na kuimarisha zaidi maarifa, uelewa na uwezo wetu katika kufanya tafiti za kitaaluma. Hivyo, tupo hapa ikiwa ni sehemu ya kutekeleza malengo hayo. Tuwe tayari kuzingatia na kujifunza ili tukitoka hapa tuwe Mahakimu wenye weledi zaidi,” alisema Mhe. Mtulya.

Mhe. Mtulya pia alisisitiza umuhimu wa kuthaminiana, kujaliana, kuheshimu viongozi, kuzingatia nidhamu na kuepuka ubaguzi, huku akiwataka wanachama kuendelea kushikamana kupitia vikundi vilivyoanzishwa kwa ajili ya kusaidiana wakati wa shida na raha.

Kwa upande wake, Naibu Msajili Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Benard Mpepo, alisisitiza umuhimu wa maadili, mawasiliano na mahusiano mazuri katika mazingira ya kazi.

“Ili uwe na utendaji kazi mzuri, ni lazima muwe na mahusiano na mawasiliano mazuri na viongozi wenu,” amesema Mhe. Mpepo, akiongeza kuwa ni muhimu kujenga mahusiano mazuri kati ya Majaji, Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama ili kuboresha utendaji kazi.

Naye, Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya, amewataka watumishi kuepuka ubinafsi, kuzingatia taratibu na itifaki, pamoja na kujenga utamaduni wa upendo, kujali na kusaidiana, kadhalika amewataka watumishi kuendelea kumuunga mkono Jaji Mfawidhi katika utekelezaji wa majukumu yake ya kiuongozi.

Aidha, Mwenyekiti wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Mhe. Asha Njovu, amewashukuru wanachama wanaotekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji, akiwahimiza kuendelea kudumisha viwango hivyo katika utumishi wao.

Kikao hicho pia kiliambatana na mafunzo kuhusu mbinu za kukabiliana na msongo wa mawazo pamoja na umuhimu wa malezi ya kitaaluma kwa Mahakimu (Mentorship Programme) yaliyolenga kuimarisha uwezo na ustawi wa kitaaluma wa washiriki.

Mbali na kikao na mafunzo hayo, wanachama walipata fursa ya kuburudika na kushiriki shughuli za utalii katika fukwe za Ziwa Nyasa, hatua iliyosaidia kuimarisha zaidi mahusiano na mshikamano miongoni mwa wanachama.

Kikao hicho ni sehemu ya jitihada za TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya katika kuimarisha weledi, maadili, mshikamano na uwezo wa kitaaluma wa Majaji na Mahakimu, kwa lengo la kuendelea kuboresha utoaji wa haki na huduma kwa wananchi.

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa kwenye kwenye picha ya Pamoja na viongozi na wanachama wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya wakati wa mafunzo na kikao hicho.

Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye kikao kilichoambatana na mafunzo ya Mentorship Programme


Sehemu Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika Kikao hicho cha TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya. 

Chama cha Majaji na Mahakimu Tanzania (TMJA) Masjala Ndogo ya Mbeya wakiwa kwenye kikao kilichoambatana na mafunzo ya Mentorship Programme

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wa pili kushoto) akiwa na viongozi wengine wa Mahakama  wakiwa kwenye picha ya pamoja na wanachama wapya wa TMJA Mbeya

Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (wapili kushoto) akiwa na viongozi wengine wakikata keki kwa pamoja kuwakaribisha wanachama wapya wa TMJA Masjala hiyo.

Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya, Bw. Festo Chonya (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho (katikati) ni Naibu Msajili Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Benard Mpepo.

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mbeya Mhe. Tedy Mlimba (aliyesimama) akizungumza katika kikao hicho, kulia ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Kyela Mhe. Roster Mofuga na kushoto ni Naibu Msajili Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya Mhe. Zawadi Laizer.

Mwenyekiti wa TMJA Mbeya Mhe. Asha Njovu (aliyesimama wapili kushoto) akifungua kikao hicho, (wa kwanza kushoto) ni katibu wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Angela Byera na Mlezi wa TMJA Masjala Ndogo ya Mbeya, Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Mbeya Mhe. Fahamu Mtulya (Katikati)

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

 

Jumatatu, 10 Agosti 2026

JAJI KIONGOZI ATEMBELEA NA KUFANYA UKAGUZI MAHAKAMA YA WILAYA CHAMWINO

Na ARAPHA RUSHEKE & JAMES BUSANYA - Mahakama

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani, amefanya ziara katika Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo, huku akitoa maelekezo mbalimbali yanayolenga kuimarisha utoaji wa huduma za haki kwa wananchi.

Ziara hiyo imefanyika leo tarehe 10 Agosti 2026 wakati alipotembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino iliyoanza kutoa huduma rasmi kuanzia tarehe 24 Julai 2026, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Mahakama ya Tanzania za kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi. Kabla ya kuanzishwa kwa Mahakama hiyo, huduma za kimahakama kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino zilikuwa zikitolewa na Mahakama ya Wilaya Dodoma mjini.

Katika ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani alikagua jengo na miundombinu ya Mahakama hiyo pamoja na kuzungumza na watumishi, ambapo alieleza kufurahishwa na jengo hilo na kuwapongeza waliokuwa wakisimamia ujenzi wake.

Nimefurahi leo tuna jengo zuri lenye viwango. Nawapongeza waliokuwa wanasimamia ujenzi huu. Tumesogeza huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Chamwino. Mahakama hii itawaletea nafuu, kuwaokolea muda na gharama,” alisema Jaji Kiongozi.

Alisema kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ni hatua muhimu katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma za haki karibu na maeneo yao, akiwataka viongozi wa Mahakama kuendelea kufikiria namna ya kusogeza huduma kwa wananchi bila kuathiriwa na mipaka ya kijiografia.

Jaji Kiongozi aliutaka Uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kushirikiana na viongozi wa Kata katika maeneo yanayohudumiwa na Mahakama hiyo, ili kuhakikisha wananchi wanapata taarifa kuhusu huduma zinazotolewa na Mahakama, ikiwemo kupitia njia za mtandao nakufanya vipindi kwa njia ya Radio.

Aidha, alisisitiza matumizi ya TEHAMA katika utoaji wa huduma za Mahakama, akieleza kuwa teknolojia inaweza kusaidia kurahisisha upatikanaji wa haki kwa wananchi na kupunguza utegemezi wa matumizi ya makaratasi.

Katika kusisitiza matumizi ya TEHAMA, Mhe. Dkt. Siyani aliagiza timu ya wataalum kuhakikisha huduma za mtandao ziunganishwe haraka katika Mahakama hiyo ili ziweze kusadifu ubora wa jengo na huduma za kimahakama kwa wananchi, akieleza kuwa uwepo wa Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ni fursa inayopaswa kutumika kikamilifu katika kuboresha huduma za Mahakama.

Alibainisha pia kuwa, ushahidi unaweza kutolewa katika Mahakama kwa njia ya Mahakama Mtandao, pale ambapo utaratibu huo unaruhusiwa kisheria, hatua ambayo inaweza kusaidia kurahisisha mwenendo wa mashauri na kupunguza usumbufu kwa wananchi.

Katika hatua nyingine, Jaji Kiongozi alisisitiza umuhimu wa Mahakama kuweka mazingira rafiki na wezeshi kwa wananchi wanaofika kupata huduma, akionya watumishi dhidi ya kuweka vikwazo visivyo vya lazima, hivyo mwananchi anapofika mahakamani anapaswa kuhudumiwa kwa wakati.

Mhe. Dkt. Siyani pia alitoa maelekezo kuhusu utunzaji wa vielelezo na kuvirejesha kwa wahusika mara baada ya mashauri kukamilika mahakamani, akitaka kuwepo kwa utaratibu maalum wa kuhakikisha vielelezo hivyo vinatunzwa kwa usalama na kwamba wenye mali wanarejeshewa kwa kufuata sheria na taratibu zinazokubalika.

Akizungumzia utunzaji wa mazingira, Jaji Kiongozi alisisitiza kuwa, majengo ya Mahakama yanapaswa kwenda sambamba na mazingira safi na yanayovutia, akiwataka watumishi kupanda miti na maua pamoja na kuhakikisha uchafu unaondolewa katika maeneo ya Mahakama.

Tusikubali jengo letu na miundombinu yetu ichakae kwa wepesi. Watumishi tushirikiane kulitunza jengo letu na kulifanyia usafi. Mazingira yetu ya ndani na nje ya Mahakama yawe vizuri,” alisema Dkt Siyani.

Aliagiza uongozi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kusimamia utekelezaji wa mpango wa utunzaji mazingira na upandaji miti katika maeneo ya Mahakama, akieleza kuwa taasisi jirani zinapaswa kuvutiwa na mazingira bora yatakayowekwa na Mahakama hiyo.

Katika kuimarisha utendaji kazi, Jaji Kiongozi aliwataka watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino kuwa na utamaduni wa kujifunza, kukumbushana na kufundishana, akisema kuwa mafanikio yanahitaji watumishi wenye utayari wa kujifunza mambo mapya kila wakati.

Kama mnataka mafanikio muwe na utaratibu wa kukumbushana kwa kufundishana. Watu bora ni wale wanaojifunza. Msibweteke na mnachokijua, vipo vingine hamvijui. Mnaweza kufundishana wenyewe mambo mengi na muhimu,” alisema Jaji Kiongozi

Akihitimisha ziara hiyo, Mhe. Dkt. Siyani aliwataka watumishi kujitathmini mara kwa mara kuhusu namna wanavyowahudumia wananchi na kuhakikisha kila anayefika mahakamani anapata huduma kwa heshima, weledi, uadilifu na kwa wakati.

Mahakama ya Wilaya Chamwino inahudumia wananchi wapatao 486,176, Wilaya hiyo inayoundwa na tarafa tano (5), Kata 36, Vijiji 107 na Vitongoji 814. Kuanzishwa kwa Mahakama hiyo ni hatua muhimu katika kusogeza huduma za haki karibu zaidi na wananchi, kuwaokoa muda na gharama, pamoja na kuimarisha imani ya wananchi katika mfumo wa utoaji haki nchini.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyeketi kiti cha mbele), akipokea taarifa fupi ya Mahakama ya Wilaya ya Chamwino Kutoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (wa pili kulia) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo leo tarehe 10 Agosti, 2026.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kulia) akitete jambo na Waendesha Mashitaka wa Serikali wakati alipotembelea Ofisi hiyo ya wadau wanaotoa huduma mahakamani hapo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto), akikagua sehemu ya miundombinu jengo la Mahakama ya wilaya Chamwino huku akiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (kulia aliyenyoosha mkono) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (kushoto) akizungumza na kupata maelekezo kutoka kwa mtumishi wa mahakama hiyo kwenye dirisha la Mapokezi.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino wakikagua sehemu ya miundombinu ya jengo la Mahakama ya wilaya Chamwino huku akiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga. 
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (aliyenyoosha mkono) akimuonesha eneo la vielelezo Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama wakati wa ziara hiyo.
Mtendaji wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dodoma Bw. Bedson Mariba (wa kwanza kushoto) akimuonesha Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani eneo la mipaka ya Mahakama ya Wilaya Chamwino wakati alipokuwa na Viongozi mbalimbali wa Mahakama wakati wa ziara hiyo.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (aliyenyoosha mkono) akitoa maelekezo kwa Viongozi wa Mahakama juu ya utunzaji wa mazingira ya Mahakama ya Wilaya Chamwino.
Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati), akisisitiza jambo wakati alipokuwa akiongea na watumishi na viongozi wa Mahakama (hawapo pichani) wakati wa ziara ya kutembelea Mahakama ya Wilaya Chamwino na kukagua miundombinu ya Mahakama hiyo. Wengine ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dodoma Mhe. Joachim Tiganga (wa kwanza kushoto) na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Eva Kiaki Nkya wa kwanza kulia.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama ya Wilaya Chamwino mara baada ya ziara ya ukaguzi wa jengo hilo.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania alioambatana nao katika  ziara ya ukaguzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

Muonekano wa jengo la Mahakama ya Wilaya Chamwino.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama)

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)